Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Maliasili na Utalii

Hon. Nape Moses Nnauye

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mtama

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Maliasili na Utalii

MHE. NAPE M. NNAUYE: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi, nami nitumie dakika chake nichangie kwenye hotuba hii ya bajeti ya Wizara ya Maliasili na Utalii. Kwa kipekee nampongeza sana Mheshimiwa Waziri, Mwalimu wangu wa Sheria kwa kazi nzuri anayoifanya yeye na Naibu wake na pia watendaji kwenye Wizara hii, Katibu Mkuu na Taasisi wakiwemo Ngorongoro, TFS na wengine, hongereni kwa kazi nzuri. Wizara hii ilikuwa na kelele sana, lakini mmejitahidi kuituliza na nadhani mtasonga mbele vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nichukue nafasi hii Mheshimiwa Waziri kukushukuru kwa kukubali Naibu Waziri aje kufanya ziara Jimboni kwangu na kutembelea maeneo yale ambayo yameathiriwa na wanyamapori hasa Kata ya Mnara na Chiponda. Naibu Waziri karibu sana Mtama, tunakupenda na tutakupokea kwa mikono miwili, utembelee maeneo haya na kuona jinsi tulivyoathiriwa na wanyamapori. Nami sina mashaka kwamba tutachukua hatua za kurekebisha maeneo haya na kupunguza athari zake.

Mheshimiwa Naibu Spika, naipongeza na kuishukuru Kamati kwenye hotuba yao wamegusia jambo ambalo ndilo nilitaka nilizungumze hapa; Jambo la sekta ndogo ya uwindaji wa kitalii. Kamati wamekiri kwamba sekta hii kidogo imetikisika, imeyumba. Takwimu huwa hazidanganyi. Ukiangalia namba zinaonesha wazi kwamba liko tatizo. Bahati nzuri jambo hili tulianza kulizungumza ndani ya Bunge hapa miaka kama minne au mitatu iliyopita tukaanza kutoa mashaka yetu kwamba jamani mnapokwenda mtapata matatizo.

Mheshimiwa Naibu Spika, leo tukizingalia takwimu, zinakubaliana na ripoti ya kamati kwamba sekta hii tusipochukua hatua itakwenda kufa na hapa nipitie takwimu chache. Mwaka 2013 sekta hii ilikuwa na wawindaji wa kitalii 1,550, leo ukichukua takwimu za 2018/2019 wameshuka mpaka wamefika 473. Kutoka 1,550 mpaka 473, hili ni anguko kubwa sana, tusipochukua hatua tunakwenda pabaya. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, katika mapato ya Serikali, mwaka 2013 Serikali ilikuwa inapata mpaka dola milioni 27. Leo tumeshuka mpaka dola milioni nane. Hili ni anguko kubwa; 27 kwa 8. Mapato ya jumla ukikusanya tozo na vitu vingine tulikuwa tunakwenda mpaka dola milioni 100. Leo, milioni 25, maana yake tunaanguka. Mwaka 2013 tulikuwa na makampuni 60 yapo yanafanya kazi, leo yako chini ya 40. Maana yake tumeshuka kwa zaidi ya asilimia 50. Ukienda kwenye takwimu sasa za vitalu vyenyewe, vitalu ambavyo viko wazi sasa vinakaribia asilimia 50. Maana yake ni kwamba kuna anguko kubwa kwenye hii sekta na kama hatutachukua hatua za makusudi, Sekta hii itaanguka. Sekta hii kwenye Wizara ni eneo muhimu katika kufanya mchango wa Wizara kwenye uchumi wetu uendelee kukua.

Mheshimiwa Naibu Spika, nataka kuiomba Serikali, ondokeni kwenye kuona kwamba mkishaamua jambo, hata kama linafanya vibaya mnatakiwa kuendelea nalo, nadhani siyo sawa sawa. Kila mara mnakuja, tunawaonesha takwimu, tunaonesha mwelekeo ulivyo, lakini kwa sababu Serikali mmeshaamua, mnaamua kuendelea hivyo hivyo, hata kama tunakwenda kuanguka. Mheshimiwa Waziri mkiendelea hivi, maana yake mnahujumu sekta hii; na mkihujumu sekta hii, mnahujumu uchumi wa nchi. Kama mapato yameanguka kwa kiasi hiki na bado hatuchukui hatua, liko tatizo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa tumefikaje hapa? Kweli kuna mchango wa tatizo la Covid, lakini tulianza kuanguka kabla ya Covid na tukaanza kusema kwamba tunaanguka. Covid ilipokuja ikapiga msumari kwenye anguko. Sasa katika mazingira haya, mategemeo yangu ilikuwa ni kwamba tuchukue hatua, kwa sababu tukichukua hatua tutakwamua anguko hili. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, vitalu hivi vinavyobaki wazi kila siku ya Mungu vinapoteza thamani yake. Wewe unajua katika vitalu vilivyobaki wazi leo karibu vitalu 14 havifai, maana yake tumepoteza rasilimali ya nchi. Kazi kubwa ya Wizara hii ni pamoja na kuhifadhi ndiyo kazi kubwa. Sasa kama uhifadhi unaharibika, tunachukua hatua tunakwenda kuharibu zaidi, mimi nadhani iko haja ya kuchukua hatua. Kwa hiyo, tumefikishwa hapa na nini?

Mheshimiwa Naibu Spika, kuna maamuzi Serikali tuliyafanya ya kubadilisha mfumo wa ugawaji wa vitalu. Ni kwa nia njema na hata Kamati wamekiri; nia ile njema lengo ilikuwa ni kuongeza transparency, kupunguza rushwa, kuondoa maneno; nia njema, lakini Mheshimiwa Waziri ule mfumo mliouweka una upungufu ndiyo maana vitalu mnavipeleka mnadani vinakosa soko, vinabaki wazi, vinapoteza thamani. Kadri siku zinavyokwenda rasilimali hii inaharibika.

Mheshimiwa Naibu Spika, mapendekezo yangu; moja, nendeni mkapitie upya huo mfumo mliouanzisha. Kaupitieni upya mpunguze matatizo yaliyomo including kuongeza transparency. Hivyo mlivyoweka haitoshi, bado una upungufu mwingi ndiyo maana minada inafeli. Minada yote iliyofanyika, mnapeleka vitalu vingi, mnauza vichache, mnarudisha vingi. Hapa ni kuonesha kwamba kuna upungufu kwenye mfumo.

Mheshimiwa Naibu Spika, ya pili, wale ambao wana vitalu tayari msiwapeleke kwenye mnada. Kwanza wamepitia wakati mgumu wa Covid, wamewekeza kwenye hivi vitalu, wameweka miundombinu na wanavilinda kwa sababu vile ambavyo havina watu mmeviacha, ulinzi hakuna, miundombinu hakuna, vinapotea, vinaharibika, tunapoteza mapato. Kwa hiyo, wale ambao wako kwenye vitalu, ombi langu ni kwamba waongezeeni muda wa kuendelea kupanga kwenye hivi vitalu. Rekebisheni mfumo mlioleta, vile vitalu tupu vipelekeni mnadani, endeleeni na utaratibu baada ya maboresho. Mkifanya hivi, naamini tutakuwa tume- save sekta hii.

Mheshimiwa Naibu Spika, pendekezo la tatu. Mmesema vizuri kwenye bajeti yenu kwamba mnakwenda kupitia sera, sheria, taratibu na kanuni mbalimbali malizojiwekea. Serikali ya Awamu ya Sita moja ya lengo kubwa ni kuvutia wawekezaji. Hebu nendeni mkazipitie upya tuendane na wakati na wakati huo tuangalie na mazingira mengine. Mheshimiwa Waziri, hili kundi kubwa ambalo tumelipoteza maana yake moja, limekwenda kwenye maeneo mengine. Kwenda kule, linaweza lisirudi. Sasa tusiporekebisha tutaendelea kuanguka.

Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono hoja. Ni matumaini yangu Serikali itachukua hatua tuiokoe Sekta ya Uwindaji hapa nchini. (Makofi)