Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Maliasili na Utalii

Hon. Zuberi Mohamedi Kuchauka

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Liwale

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Maliasili na Utalii

MHE. ZUBERI M. KUCHAUKA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa nafasi mchana huu nami nichangie Wizara hii mahususi kwa uchumi wa Taifa letu. Awali ya yote kama ilivyo ada nawapongeza Mheshimiwa Waziri, Naibu Waziri na Watendaji wote. Pamoja na ugumu uliopo kwenye Wizara hii, wanajitahidi kadri ya uwezo wao, kadri Mwenyezi Mungu alivyo wajaalia. Vile vile napenda kusema kwamba mchango wangu leo nitauanza moja kwa moja kwenye uhifadhi wa wanyamapori. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kweli Taifa letu kama mchangiaji aliyepita alivyosema, Serikali ya Awamu ya Tano imedhibiti ujangili, uhifadhi umeongezeka, lakini matokeo ya udhibiti huu ndiyo haya malalamiko ambayo sasa hivi kila kona ya nchi yetu tunayapata, hasa wanyama hawa wanaoitwa tembo.

Mheshimiwa Naibu Spika, mfano kwenye Halmashauri ya Wilaya yangu ya Liwale ambako sehemu kubwa ndiyo tunaozungukwa na hifadhi ya Selous, wako wananchi wamehama kutoka mashambani wamerudi vijijini baada ya mazao yao kuharibiwa au kulima na wanyama hao wanaoitwa tembo. Kuna Kijiji kama Ngumbu, Milui, Kikulyungu, Mkutano, Mtawatawa, Barikiwa, Ndapata, Mpigamiti, Lilombe na Kimambi; baadhi ya wananchi wa vijiji hivi tayari wapo vijijini, wamerudi kutoka mashambani baada ya wanyamapori hasa hao jamii ya tembo kumaliza mazao yao. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naiomba Serikali, pamoja na kwamba tumeongeza uhifadhi, lakini bado sasa turejee kwa wananchi tuangalie ni namna gani wananchi wetu tunawakinga na ongezeko hili la tembo? Ongezeko la tembo ni zuri, tunapata mapato mengi, lakini lazima turejee, tuwe na mipango mikakati safi ya kuwanusuru wananchi wetu ili wasiendelee kuteseka na hatimaye kupata majanga ya njaa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo lingine, naomba nizungumzie suala la kifuta machozi. Sheria ya Kifuta Machozi ni ya muda mrefu sana. Hivi kama mwaka 1974 mtu alikuwa anapewa shilingi 500/= labda kutokana na umbali wa mazao yake yalivyoliwa au shilingi 1,000/=, hivi kweli kiwango kile tunaendelea kukitumia mpaka leo! Nawaomba sana kwa kipande hicho tuongeze kiwango hicho angalau tuangalie namna tunavyoweza kuwasidia wananchi wetu. (Makofi)

MHE. ESTER A. BULAYA: Mheshimiwa Spika, taarifa.

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Kuchauka kuna taarifa kutoka kwa Mheshimiwa Ester Bulaya.

T A A R I F A

MHE. ESTER A. BULAYA: Mheshimiwa Naibu Spika, nilikuwa nampa Mheshimiwa Kuchauka taarifa katika mchango wake; hili tatizo la fidia ni kero maeneo mengi; na siyo tu ni kidogo, haitoki kwa wakati. Mfano, ni wananchi wa Jimbo la Bunda Mjini, Kata ya Nyatwali; Natwali, Tamau, Serengeti, mbali ya kwamba tembo wanaharibu mazao yao, wanaomba fidia na fidia yenyewe hiyo ndogo haitoki kwa wakati. Kwa hiyo, nilikuwa taarifa. (Makofi)

NAIBU SPIKA: Waheshimiwa Wabunge, niwakumbushe tena. Muda wa kutoa taarifa siyo muda wa kuchangia. Mheshimiwa Kuchauka endelea na mchango wako.

MHE. ZUBERI M. KUCHAUKA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Naipokea taarifa yake kwa sababu hata mimi kwangu kuna malalamiko, wananchi wameliwa mazao yao, sasa hivi wana mwaka wa tatu hawajapata fedha. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo lingine ni hapo hapo kwenye uhifadhi wa Selous. Sasa hivi Serikali imeimarisha utalii wa picha zaidi kuliko utalii wa uwindaji. Naiomba Serikali, ukanda huu wa Selous upande wa kusini kuanzia Kilwa, Liwale mpaka Tunduru, hatuna lango la utalii wa picha, matokeo yake baada ya kupunguza utalii wa uwindaji, umebakia utalii wa picha, lakini sisi kwetu tumebaki hatuna watalii na hatupati mapato yoyote yale.

Kwa hiyo, uwepo wetu wa hifadhi ya Selous tunakuwa kama vile hatuoni yale manufaa ya moja kwa moja. Kwa hiyo, naiomba Serikali kufikiria kuanzisha lango la utalii wa picha kwenye maeneo hayo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, jambo lingine nizungumzie kwenye WMAs. Waziri kwenye ukurasa wa 47 aya ya 59 ndiyo amezungumzia kidogo kuhusu WMAs. Lengo la Serikali kuanzisha WMAs hizi ni kushirikisha wananchi kwenye uhifadhi. Sasa tunawashirikishaje kama kwenye hotuba nzima umetaja kwenye aya moja, tena kamstari kamoja tu? Yaani hawa watu tunawashirikisha vipi? Kwa kweli kama Serikali ilikuja na lengo zuri kuimairisha WMAs ili kushirikisha wananchi kwenye uhifadhi ili wananchi wanaozunguka hifadhi hizo waone faida ya kuwa hifadhi zile, basi naiomba Serikali kuimarisha WMAs na kuona ni namna gani wanazisaidia hata kuwatafutia wawekezaji kwenye vitalu hivi ambavyo wamewekeza hao WMAs. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, vile vile fedha zao zinachelewa, hata pale wanapopata mtalii au mwekezaji mwenye Kitalu X, lakini bado mapato yao kutoka Serikalini yanachelewa sana. Hapo naiomba Serikali kuangalia upande wa WMAs. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo lingine nije kwenye uhifadhi wa TFS. Bunge lililopita niliuliza swali hapa kuhusu mpango wa uvunaji wa kitalu cha Nyelakipelele. Nashukuru Serikali wameshaleta mpango wa uvunaji wa msitu ule wa Nyelakipelele, lakini uvunaji wa pale ni wa holela. Ukipita hii njia kutoka Nachingwea kwenda Liwale, unapishana na malori usiku, yanabeba magogo. Mengine yana vibali, mengine hayana vibali, mengine yamegongwa na mengine hayajagongwa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kweli naiomba Serikali, pamoja na nia njema ya kufungua uvunaji kwenye hifadhi hii ya msitu wa Nyelakipelele, bado tunaomba itupie macho uvunaji wa msitu huu, kwani ni wa ovyo mno na wala hauzingatii mazingira. Sidhani kama uvunaji ule ni endelevu, kwa sababu uvunaji endelevu ni kwamba watu wanavuna kwa mpango na miti ile lazima ipandwe mingine, lakini kwenye uvunaji wa msitu huo hakuna uvunaji endelevu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nirejee kwenye ikama ya wafanyakazi kwenye Halmashauri zetu. Kwenye Halmashauri zetu utakuta mhifadhi au Afisa wa Wanyamapori yuko mmoja tu. Jambo hili ndiyo linaloleta mgogoro mpaka tunapata matatizo ya wanyamapori, tunashindwa kupata msaada kwa sababu Afisa wa Wanyamapori kwenye wilaya au kwenye Halmashauri, anakuwepo mmoja.

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MHE. ZUBERI M. KUCHAUKA: Mheshimiwa Naibu Spika, naiomba Serikali, Serikali ni moja… (Makofi)

NAIBU SPIKA: Ahsante sana. Kengele ya pili imeshagonga Mheshimiwa.

MHE. ZUBERI M. KUCHAUKA: Ahsante sana kwa kunipa nafasi. Nami naunga mkono hoja. (Makofi)