Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Nishati

Hon. Issaay Zacharia Paulo

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mbulu Mjini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Nishati

MHE. ZACHARIA P. ISSAAY: Mheshimiwa Spika, nachukua nafasi hii kuungana na viongozi, Watanzania wenzangu wote kumshukuru sana Mwenyezi Mungu kwa kutujalia baraka zake katika nyanja mbalimbali za ustawi wa kijamii, kiuchumi, kidiplomasia na kisiasa. Kama Taifa tuendelee kusema ahsante sana Mungu wetu.

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya wananchi wa Jimbo la Mbulu Mjini nachukua nafasi hii kuungana na Watanzania wenzangu kumpongeza sana Mheshimiwa Samia Suluhu Hasan, Rais wa Jamhuri ya Mungano wa Tanzania kwa kupokea uongozi wa Taifa letu kwa amani na utulivu. Ninamwombea baraka, ulinzi na mafanikio makubwa kwa Mwenyezi Mungu.

Mheshimiwa Spika, aidha, nawaombea watendaji na wateule wote wa Serikali ya Awamu ya Sita, Mwenyezi Mungu awajalie mafanikio mema katika utume wao Taifa letu lipate kufikia malengo makuu.

Mheshimiwa Spika, nachukua nafasi hii kuungana na Watanzania kuendelea kuwaombea Mheshimiwa Hayati Dkt. John Pombe Magufuli aliyekuwa Rais wa Serikali ya Awamu ya Tano na Watanzania wote waliotangulia mbele ya haki kwa Mwenyezi Mungu awapokee katika Ufalme wake usio na mwisho. Kwa kweli kama Taifa mchango wake utakumbukwa daima. Kwa vielelezo hivi, Bwawa la umeme, SGR, Busisi Bridge, Bomba la Mafuta na mengine mengi sana.

Mheshimiwa Spika, sasa naomba kutoa mchango wangu kupitia mapendekezo ya bajeti ya Wizara hii ya Nishati. Kwanza Wizara kupitia Mpango wa REA lll unaoendelea, ije na mkakati wa kuwatambua walengwa kwa kuwa wako wateja wengi sana waliofanya uwekaji wa waya katika makazi yao lakini umeme haujaunganisha.

Mheshimiwa Spika, kumekuwa na ugumu wa utekelezaji wa maagizo ya Mheshimiwa Waziri katika Jimbo langu la Mbulu Mjini kupitia ziara zake mbalimbali katika Jimbo letu. Kwa kauli ya watendaji wa TANESCO na REA kuwa hawana fedha, mifano hiyo iko katika Kata za Murray 2016, 2018, Gunyoda, Nahasey 2018 hadi sasa umeme haujaenda, hali iliyotupa wakati mgumu kuomba kura za CCM wakati wa Uchaguzi Mkuu Oktoba, 2020.

Mheshimiwa Spika, kutokana na maeneo mengi ya vijijini kuwa na uhitaji mkubwa wa nguzo na nyaya za umeme, Serikali iangalie uwezekano wa kufanya uhakiki wa maeneo hayo ili kupeleka kifaa cha utayari (UMETA) wakati majengo yakiendelea kuongezeka. Hivyo basi, naomba kauli ya Serikali kuhusu hali hii umeme kwamba utaenda lini?

Mheshimiwa Spika, mwisho, naunga mkono hoja kwa asilimia mia moja na naomba kuwasilisha.