Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Nishati

Hon. Kilumbe Shabani Ng'enda

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kigoma Mjini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Nishati

MHE. KILUMBE S. NG’ENDA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru na mimi kunikumbuka na kuniona na hasa baada ya kuzungumza ndugu yangu Mheshimiwa Kavejuru.

Mheshimiwa Spika, suala la umeme wa Gridi ya Taifa katika Mkoa wa Kigoma ni ajenda ya mkoa, ni ajenda ya Wabunge wote hata wengine ambao ni Mawaziri hawawezi kusema lakini ni ajenda yetu. Hii ni kwa sababu kama mnavyojua Kigoma ni miongoni mwa mikoa ya pembezoni na ambayo imechelewa sana katika maendeleo na moja ya jambo lilituchelewa ni kukosa umeme. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, leo tunapozungumzia changamoto za umeme tunazungumzia mafanikio makubwa yaliyofanyika kutokana na kazi iliyofanywa na Wizara hii. Kwa hiyo, nimpongeze sana Waziri, Naibu Waziri pamoja na watumishi wote wa Wizara hii na mashirika kama TANESCO na watu wa REA, kwa kweli tunazungumza changamoto zinatokana na mafanikio. Sisi zamani huko Kigoma ilikuwa umeme ukiwaka maana unaweza ukawaka hata mara moja kwa wiki ukiwaka unasikia watu wote eee, utafikiri labda Timu ya Wananchi imeingiza goli kwenye nyavu za Simba. Yaani wala hili sikudanganyi... (Makofi/Kicheko)

MBUGE FULANI: Rudia.

MHE. KILUMBE S. NG’ENDA: Mheshimiwa Spika, yaani ukisikia kelele wakati ule ilikuwa sababu ni mbili; ni Yanga kafunga goli kwenye lango la Simba au umeme umewashwa. (Makofi/Kicheko)

Mheshimiwa Spika, nataka nitumie nafasi hii kumshauri Mheshimiwa Waziri mwenye dhamana kwamba pale Kigoma mmeingia mkataba na wale wawekezaji wa solar ili wazalishe umeme wa megawatt 4.8 mpaka sasa wanazalisha megawatt 2. Tatizo la wale wawekezaji ni kwamba ule mradi wao ulichelewa kuanza ukakumbana na misukosuko mingi hata mlipokuja kukubaliana na kuingia mkataba baadhi ya vifaa vilikuwa vimeibiwa. Kubwa kuliko yote hizo megawatt 2 zinapatikana mchana tu ikishaingia saa moja jioni ni zero, umeme haupatikani kabisa kutoka kwa watu wale wa solar. Kwa maana hiyo wanachosaidia pekee ni kupumzisha mashine za TANESCO mchana ili ziweze kuwaka usiku. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tatizo la pale inaonekana vifaa vyote; panel, inventor, step-up transformer vipo sawasawa lakini hawana zile betri kubwa za ku-store energy, kwa hiyo, inapofika usiku hawezi kuzalisha chochote. Kwa sababu mmeingia mkataba na mnawalipa naomba wapeni hata government guarantee wakope benki waweze kuweka mradi wa vizuri. Sisi tukipata ile megawatt 4.8 tatizo letu sisi Wilaya ya Buhigwe na maeneo mengine linakwisha kabisa kabisa. Kwa hiyo, naomba sana Mheshimiwa Waziri muone jinsi ya kusaidia. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini hebu chukueni utaratibu kama wanaouchukuwa TAMISEMI au Wizara ya Afya, wanapofika mahali wakaamua kuna hospitali ya shirika la dini wanaitumia kama Hospitali ya Wilaya basi hupeleka madaktari wa Serikali kusaidia supervision na kutoa huduma. Hebu kwenye kituo hiki kwa vile mmeingia mkataba na wale watu peleka mainjinia wako wa TANESCO wasaidiane na wale watu pale kuhakikisha kwamba kazi inakwenda vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, jambo lingine ambalo nataka kulizungumza ni kwenye nishati ya mafuta, tofauti ya bei kutoka mkoa mmoja kwenda mwingine. Leo hii asubuhi nimefuatilia Dar es Salaam lita moja ya petrol shilingi 2,249, lita ya diesel ni shilingi 2,073 lakini Kigoma leo hii lita ya diesel ni shilingi 2,481 tofauti ya shilingi 232 na Dar es Salaam sasa hapa ukinunua lita 1,000 tu kuna tofauti ya shilingi 232,000, gharama za uzalishaji lazima zitakuwa kubwa kwa Mkoa wa Kigoma.

Mheshimiwa Spika, mimi ni mtu ambaye namuamini sana Mheshimiwa Waziri, hebu ajaribu kuangalia hivi hatuwezi kuwa na bei moja ya petrol na diesel kwa nchi nzima. Ni jambo ambalo linawezekana, mkaona wapi pakufidia tukawa na bei moja, ukienda Kigoma, Mbeya au sehemu nyingine kila sehemu iwe moja.

Mheshimiwa Spika, la mwisho limezungumzwa suala la vinasaba hapa…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

SPIKA: Bahati mbaya muda hauko upande wako.

MHE. KILUMBE S. NG’ENDA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana lakini kwenye vinasaba nilitaka tu kumsaidia ndugu yangu pale aliyekuwa anaomba ulinzi kwamba mimi nimeshamuandalia ulinzi kule Kigoma asiwe na wasiwasi. (Kicheko/Makofi)