Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Nishati

Hon. Maimuna Salum Mtanda

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Newala Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

2

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Nishati

MHE. MAIMUNA S. MTANDA: Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa kunipatia fursa hii ili nami niweze kuchangia katika Wizara hii muhimu ya Nishari.

Mheshimiwa Spika, awali ya yote, nimshukuru Mwenyezi Mungu, lakini pia nitoe pongezi nyingi kwa Waziri mwenye dhamana ya Nishati pamoja na watendaji wake wote. Pia niipongeze Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kuasisi suala la mradi wa umeme vijijini kwani umepunguza kwa kiasi kikubwa sana kero ya umeme ambayo ilikuwa inavikumba vijiji vyetu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, niende kwenye Jimbo la Newala Vijijini. Wote tunajua kwamba umeme ni ajira, biashara, ulinzi lakini pia ni afya. Jimbo la Newala Vijijini lina jumla ya vijiji 107, kati ya vijiji hivyo ni 54 tu ndiyo vyenye umeme, vijiji 53 havina umeme sawa na asilimia 49.53. Kuna Kata sita katika hivyo vijiji 53 ikiwemo Kata ya Chitekete ambayo Mbunge mimi natoka haina umeme niko gizani. Kata nyingine ni Nakahako, Mpwapwa, Nandwahi, Mkoma 2 na Nambali, kata hizi hazina kabisa umeme. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kuna suala la ujazilizi wa vijiji vile ambavyo mradi wa REA umepita. Mheshimiwa Waziri una kazi kubwa ya kufanya kwa sababu kama walivyotangulia kusema katika vijiji ambavyo umeme umepita vingi wanauona umeme umekaa kama kamba ya kuanikia nguo, haujashuka kwenye nyumba za wananchi. Ukienda Kata ya Mdimba inahesabika kwamba ina umeme lakini Mdimba pale ambapo ndipo Makao Makuu ya Kata umeme haujashuka kabisa na ni kero kubwa wanasumbua kila siku. Tunashukuru tumepata mkandarasi, niombe sana Mheshimiwa Waziri msimamie kwa karibu kwa sababu hali iliyopo inahitaji usimamizi otherwise ile miaka miwili ambayo tumejipangia kwamba vijiji vyote vitakuwa vimepata umeme kwa hali iliyopo Newala Vijijini tunaweza tusifanikiwe. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini pia tunamshukuru Mwenyezi Mungu Mtwara sasa ameshusha neema ya madini. Tumesikia kuna graphite kule Chiwata ambayo na mimi pia inanigusa kwa namna moja au nyingine. Ili mradi ule uweze kufanyiwa kazi vizuri tunahitaji umeme wa uhakika. Kulikuwa na mpango ule wa kujenga power station ya megawatt 300 pale Mtwara, tunaomba wakati unakuja kuhitimisha hoja yako utuambie mpango hule umefikia wapi kwa sababu kupitia mpango ule tutakuwa na uhakika kwamba umeme wa kutosha utapatikana na miradi mingine mikubwa ya maendeleo kama viwanda pamoja na machimbo vitaendeshwa bila bugudha yoyote. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pia na mimi niongelee suala la kukatikakatika kwa umeme, hali ilikuwa mbaya sana kwa Mkoa wa Mtwara lakini niishukuru Serikali ilifanya juhudi kubwa sasa hivi umeme unakatika lakini nafuu hipo. Watu wa TANESCO Makao Makuu, watu wa Kanda, TANESCO Wilaya waliweka kambi kuhakikisha kwamba tatizo la kukatika kwa umeme katika Mkoa wa Mtwara linapata ufumbuzi.

Kwa hiyo, nashukuru sana Mheshimiwa Waziri kwamba tulikwambia suala hilo na wewe ukalifanyia kazi na tunashukuru ulikuja ukaona ile hali ukatuma hiyo timu ikaja kuhakikisha kwamba suala la kukatikakatika kwa umeme basi linaisha Mkoani Mtwara. Niendelee kukuomba juhudi ziendelee kufanyika ili kukomesha kabisa suala la ukatikaji wa umeme ikiwa ni pamoja na kuboresha miundombinu ya umeme.

Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa kunipa nafasi, naomba kuunga mkono hoja. (Makofi)