Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Nishati

Hon. Daimu Iddi Mpakate

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Tunduru Kusini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Nishati

MHE. DAIMU I. MPAKATE: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi jioni hii na mimi nichangie kwenye Wizara hii ya Nishati. Naungana na wenzangu waliowapongeza Mawaziri pamoja na watendaji wote wa Wizara hii.

Mheshimiwa Spika, mimi nitaongelea point mbili ambazo ni muhimu kwa Wilaya ya Tunduru na Jimbo la Kusini kwa ujumla. Moja, nashukuru kwa kuletewa mkandarasi, Wilaya ya Tunduru ina vijiji 157 lakini kati ya hivyo 83 havina umeme. Kwa kuwa mkandarasi amekuja basi tunaomba ajitahidi kazi hii ianze mapema, maana ilitakiwa ianze mwezi wa tatu huu ni mwezi wa sita naamini ndani ya mwezi ujao ataanza kazi ili kukamilisha hivyo vijiji 83 ambavyo havina umeme kabisa.

Mheshimiwa Spika, katika hivyo vijiji 83 Jimbo la Tunduru Kusini kuna Kata 10 ambazo hazina umeme kabisa, ziko gizani. Kuna Kata ya Nalasi Mashariki na Magharibi, Mchoteka, Marumba, Mbati, Mtina, Mchesi, Lukumbule na Masakata pamoja na Misechela. Kata hizo zote hazina kabisa umeme, kwa hiyo tunaomba mkandarasi afanye chini juu aweze kuwahi kufanya kazi hiyo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, la pili nitazungumzia suala la kukatika kwa umeme Wilaya ya Tunduru. Sisi tuna majibu, kwa hiyo, namuomba Waziri ayafanyie kazi majibu ambayo tumeyaona. Tunashukuru Serikali imeleta umeme Gridi ya Taifa lakini umeme ule kutoka Songea mpaka Tunduru ni kilometa 265 Kv 33, kwa hiyo, umeshindwa kuhimili vishindo. Umeme huo huo unaenda mpaka Mang’aka, Masasi mpaka Nachingwea kilometa 600 Kv 33. Kwa hiyo, majibu tuliyoyapata ni kwamba tunatakiwa tuweke substation pale Tunduru na Masasi ili ku-boost umeme uweze kufika kwa kiwango kili ambacho kinatakiwa, lakini bado mnatakiwa muongeze ile nguvu kwa maana kutoka Kv 33 mpaka kufika Kv 132. Jambo hili limekuwa ni kero kubwa sana Tunduru, umeme unakatika kila siku na kila wakati. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa kuwa Tunduru inapita Namtumbo, Namtumbo ina barabara mbili; ina barabara inayopita Namtumbo Mjini na ina barabara inayopita Lusewa ambako nako umeme umekwenda basi ikiwezekana mfanye utaratibu wa kuweka line mbili za kupeleka umeme Tunduru ambao unaenda moja kwa moja mpaka Masasi na Nachingwea. Mkatumia line ya Lusewa, Nalasi, Mbesa mpaka Tunduru Mjini ili iweze kufanya kazi ile ambayo imekusudiwa. Kwa hiyo, naomba sana suala hili mliangalie, mtuwekee extention nyingine ya line ambayo itaenda Tunduru kupitia Nalasi ili ihakikishe kwamba inaleta umeme ule na usumbufu unapungua kwa asilimia kubwa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, jambo lingine ambalo napenda kuzungumzia ni suala la gesi. Kwa kweli kwa taarifa ya Wizara magari 700 yanayotumia gesi ndani ya miaka mitatu ni madogo sana. Naomba tuweke mkakati mahsusi, hasa sisi Wabunge walete wale wataalam watufungie yale matanki ya gesi ili magari yetu yatumie gesi kwa sababu ni gharama nafuu sana.

Nawashauri TPDC waweke kituo cha gesi hapa kwa ajili ya kujanza kwenye magari ya Wabunge pamoja na wananchi waliopo Dodoma ili kupunguza adha hii ya kutumia mafuta ya diesel na petrol. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, hii itatusaidia moja, kuongeza mauzo ya gesi na pili itawapunguzia watumiaji gharama ya kutumia mafuta ya petrol pamoja na diesel, haya yatatusaidia sana. Wenzetu Dangote kama ulivyozungumza wale wana magari 600, mpaka sasa magari 250 tu tena maroli ndiyo yanatumia gesi. Hili ni jambo nzuri sana na ni funzo kwa Serikali kutumia magari yanayotumia gesi ili kuhakikisha tunatumia gesi kwa uadilifu zaidi kwa ajili ya maendeleo ya nchi yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, jambo lingine ambalo nilikuwa napenda tuliangalie ni suala la LNG pale Lindi. Kwa kweli suala la LNG ni kizungumkuti na ni la muda mrefu, naomba sasa mhakikishe ila kazi inaanza kwa maendeleo ya watu wa Kusini ili watu wa Mtwara na Lindi waone kwamba gesi yao inathaminiwa na ule mradi unaanza kwa sababu utatupatia fedha nyingi sana kwa ajili ya maendeleo ya wananchi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hayo machache, naunga mkono hoja kwa asilimia mia moja. (Makofi)