Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Nishati

Hon. Eng. Stella Martin Manyanya

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Nyasa

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Nishati

MHE. ENG. STELLA M. MANYANYA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi hii na mimi niweze kuchangia. Pia nimpongeze sana injinia mwenzangu Mheshimiwa Ulenge kwa mchango wake mzuri. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nianzie kuipongeza sana Wizara hii lakini kuwapongeza watanzania wote kwa jitihada za pamoja tulizofanya kuhakikisha kwamba Shirika la Umeme la Taifa (TANESCO) halipelekwi kuwa ni shirika la mtu binafsi limebakia kuwa ni shirika la Tanzania kwa ajili ya kuchochea maendeleo ya Watanzania. Kazi nyingi zinazofanywa na shirika hili kwa kweli ni za kuchochea maendeleo na siyo faida kama faida ilivyo. Ndiyo maana kwa muda mrefu limekuwa halizalishi faida kwa ajili ya kuangalia wananchi wote wenye uwezo na wasio na uwezo. Tunafurahi hali inavyokwenda sasa TANESCO wanaanza kutengeneza faida. Kwa hiyo, natoa pongezi sana kwa Wizara pamoja na shirika hili. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kumekuwa na suala la kwamba mpaka sasa tumeshindwa kufikia malengo tuliyojiwekea ya kupata megawatts 5,000. Niseme tu kwamba mimi naona tumekwenda vizuri nikiwa kama mjumbe wa Kamati hii ni kwamba kwa miaka takriban 60 ya toka Uhuru wetu tulikuwa tukiongeza wastani wa megawatts 26.7 tu katika grid yetu kwa maana kwamba tulikuwa na megawatts 1,605 tulizonazo sasa lakini hizo zimefikiwa baada ya miaka 60 sasa, umri wa mtu kustaafu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini kwa sasa kupitia hii mikakati tuliyojiwekea ya kuanza kuzalisha umeme wa Bwawa la Mwalimu Nyerere na maeneo mengine tayari mwaka 2022 tunaongeza megawatts 2,115 kwenye Grid ya Taifa. Jambo hili ni kubwa sana, unaweza ukawa na malengo lakini kuyafikia unayafikia kwa kiasi gani. Malengo haya yanatufikisha sisi kwa lengo tulilojipangia kwa asilimia 74 siyo kitu kidogo, ni kitu kikubwa lazima tujipongeze kwa kile ambacho tumeweza kukifanya. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, niwaombe TANESCO watu vijijini sasa hivi maendeleo yao yamejiwekeza sana kwenye umeme, haitoshi tu kupitisha laini halafu wananchi hawapati umeme lazima sasa lipatikane fungu la kutosha kwa ajili ya kuweka umeme wa laini ndogo yaani LV lines. Hilo ndilo eneo ambalo sasa hivi kwa kweli halipati fedha za kutosha. Wanakijiji hawapendi tu kuona kwamba line imepita hapa wanataka kutumia umeme. Kwa hiyo, kwa fedha hii inayotengwa lazima fedha za kutosha zipelekwe kwa ajili ya kuongeza wire hizi ndogo yaani LV lines. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, eneo lingine naomba niwasaidie ndugu zangu jana nilimsikia Mheshimiwa Mbunge Joseph wa Ukerewe akizungumzia juu ya vile visiwa vinavyopata umeme kwa bei kubwa sana takriban Sh.2000. Kwa muda mrefu shirika letu lilikuwa ndio shirika pekee linalosambaza umeme mijini na vijijini sasa sehemu moja wanapokuwa wanapata umeme kwa bei kubwa sana nimejiuliza kwa nini? Kumbe ni kwa sababu wale wana-independent power producer yaani wanapata umeme kupitia solar, ni mtu binafsi amewekeza, kwa hiyo, lazima umeme utakuwa ghali. Sasa niwaombe TANESCO kwa sababu wao wana umeme ambao unapatikana kutoka kwenye maji na vyanzo vingine na umeme huo waupe either ruzuku au waununue wao halafu wananchi wauziwe umeme kwa bei sana na watu wa maeneo mengine. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, jambo la mwisho, sheria ya EWURA irekebishwe iweze na yenyewe kuwa na vituo vya mafuta vijijini. Tumechoka kuona chupa za petrol kule vijijini halafu zitakuja kuleta madhara tutakuja kuulizana hapa. Watumie formula hii hii kwa sababu tuna Shirika letu la Kusambaza Mafuta Vijijini ili sasa nao waweze kuwa na vituo vidogo vidogo huko vijijini tuondokane na mafuta ya kwenye chupa kwa sababu pikipiki na fursa nyingi ziko huko. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ahsante sana naunga mkono hoja. (Makofi)