Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Nishati

Hon. Dr. Hamisi Andrea Kigwangalla

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Nzega Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Nishati

MHE. DKT. HAMISI A. KIGWANGALLA: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa fursa hii ya kuchangia asubuhi hii ya leo.

Mheshimiwa Spika, kwanza nimpongeze ndugu yangu Mheshimiwa Dkt. Kalemani na Naibu wake pamoja na Wizara kwa ujumla wake kwa kazi nzuri wanayofanya kwenye Wizara yao. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mchango wangu utakuwa na sehemu mbili, sehemu ya kwanza napenda kuchangia kuhusu uchumi wa gesi kwa sababu imekuwa bahati mbaya sana hatuzungumzii tena uchumi wa gesi katika nchi yet una nilidhani kwamba uchumi wa gesi pengine ungekuwa neema. Miaka ya 2010 wakati naingia hapa Bungeni tulizungumza sana kuhusu uchumi wa gesi.

Mheshimiwa Spika, kipindi kile matarajio kwenye uchumi huu wa gesi yalikuwa bei zingefika takribani dola 16 kufikia mwaka 2020 ilikuwa ni kipindi cha miaka kumi, lakini leo tunavyozungumza hapa bahati mbaya sana bei zimeshuka badala ya kwenda mbele kwenye hiyo dola 16 tuliyokuwa tunafikiria per one British Thermal Unit, leo hii bei zimeshuka mpaka dola nane. Ukitazama bei ya gesi kwenye soko la Japan, Korea ya Kusini na Ulaya unaona bei zinashuka tu badala ya kupanda na hapo nimeangalia takwimu za kabla ya mwaka 2020 ambapo hapa duniani tulikuwa hatujakumbwa na baa la COVID 19 maana yake tungetarajia pengine bei zingekuwa zinapanda badala ya kushuka. Sasa ukiweka na impact ya COVID 19 maana yake bei zitazidi kushuka.

Mheshimiwa Spika, lakini nimetazama makadirio ya bei kwa miaka 15 inayokuja yatakuwaje. Miaka 15 inayokuja bei ya milimita moja ya BTU ya gesi itakuwa dola 14 tu. Hii kwa sisi wana mazingira inatupa mtazamo tofauti kwamba pengine kizazi kinachokuja cha watoto na wajukuu zetu hakitozungumza aina ya nishati ambazo tunazizungumza leo, kwa sababu tungetarajia pengine gesi ingezungumzwa miaka kumi na tano, ishirini ijayo kama ndiyo source pekee ya energy lakini bahati mbaya haitokuwa hivyo. Kwa hivyo, sisi kwa bahati mbaya sana tusipoitumia ipasavyo gesi yetu leo, hii resource ya gesi tuliyoipata leo itapotea bure na haitokuja kuwa na faida yoyote ile. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nalisema hili kwa kutoa ushauri kwa Serikali kwamba tufikirie kwa namna yoyote ile kuanza kuitumia gesi tuliyojaliwa na Mwenyezi Mungu leo badala ya kudhani kwamba tunaweza tukafaidika sana huko mbele kuliko ilivyo sasa. Hii ni kwa sababu hata yale matarajio tuliyokuwa nayo miaka kumi na moja iliyopita hayakuwa. Kwa hivyo, tunakoenda huko mbele tunaweza tukajikuta hatupati faida yoyote kutokana na hii gesi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ushauri wangu ni kwamba tutazame zaidi faida tutakayoipata kutokana na uwekezaji kwenye sekta ya gesi kwa kutazama zaidi value chain impact ya gesi kwenye uchumi, lakini pia kwa kutazama zaidi local content kwamba tunafaidikaje, wananchi wanafaidikaje kwa uwepo wa uwekezaji mkubwa kwenye sekta ya gesi kuliko kuwaza zaidi kupata mapato ama mgao kutoka kwenye ile actual gesi inayopatikana.

Mheshimiwa Spika, miaka kumi na moja iliyopita tuliokuwepo hapa Bungeni tuliona kilichotokea na pengine miaka kumi na moja inayokuja siku za mbele tutajaliwa kuwepo wengine bado wadogo tu, tutaweza kuyaona haya na tutakumbushana hapa ndani kwamba wakati huo uchumi wa gesi hautokuwa na maana yoyote ile kama tusipoamua leo ku-tap into the potential that the gas economy is going to bring to our country na badala yake tukawaza zaidi mapato. Nalisema hili kutokana na sheria tulizozitunga miaka miwili, mitatu iliyopita hapo ambazo zinazidi kuweka ugumu kwenye majadiliano ya uwekezaji kwenye sekta ya gesi badala ya kuzitazama zile PSA kibiashara zaidi, kuzitazama kwa mawanda mapana zaidi ya impact ya gesi kwenye value chain ya uchumi wetu, kwenye local content ya uchumi wetu tutajikuta tunapitwa na wakati. Hakuna uwekezaji utakaotokea na hatutokuja kupata faida ya hii gesi ambayo tumejaliwa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, baada ya kulizungumza hilo, naomba kumshukuru Mheshimiwa Waziri Dkt. Kalemani, miezi miwili iliyopita alikuja pale Jimboni kwetu Nzega Vijijini na akatuzindulia mradi katika Kata ya Isanzu wa kuweka umeme vijijini. Bahati mbaya sana alisema baada ya siku kumi umeme ungewaka leo imepita miezi miwili umeme haujawaka. Kwa hiyo, namuomba ahadi aliyoitoa kwa wananchi wale itekelezwe na Serikali. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sambamba na Kijiji cha Isanzu kuna Kata nyingine kama za Tongi, Mizibaziba bado hazijawa na umeme na zote hizi walishafanya tafiti na zinahitaji kupata umeme.

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

SPIKA: Ahsante sana.

MHE. DKT. HAMISI A. KIGWANGALLA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru, naomba kuunga mkono hoja. (Makofi)