Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Nishati

Hon. Jerry William Silaa

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Ukonga

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Nishati

MHE. JERRY W. SILAA: Mheshimiwa Spika, nami nakushukuru kunipa nafasi kuchangia bajeti hii ya Wizara ya Nishati. Kwanza, niungane na Wabunge wengine kuipongeza Serikali kwa kazi kubwa iliyofanya katika usambazaji wa umeme wa REA. Sisi Wabunge wa majimbo ya mijini tunanufaika na usambazaji wa umeme wa Mradi wa Peri- Urban kwenye kata zote za Jimbo la Ukonga na kazi inaendelea vizuri.

Mheshimiwa Spika, mchango wangu napenda kujikita kwenye maeneo mawili. La kwanza ni ujenzi wa LNG Plant kule Lindi.

Niipongeze Serikali na Mheshimiwa Waziri kwenye hotuba yake ukurasa wa 68 ameelezea hatua zilizofikiwa na mipango ya Serikali ya kuhakikisha ujenzi huu unakwenda kwa kasi ama mazungumzo baina ya Serikali na wawekezaji yanakamilika kwa wakati kama vile Mheshimiwa Rais wetu Samia Suluhu Hassan alivyoelekeza. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, niipongeze Serikali kwa kutumia timu ile iliyopata uzoefu kwenye Mradi wa Bomba la Mafuta la Uganda ama East Africa Crude Oil Pipeline kuitumia katika negotiation ya mradi huu. Niiombe Serikali ifanye kila liwezekanalo kuhakikisha mazungumzo haya yanafanyika kwa wakati, lakini katika kuzungumza huko Serikali ijitahidi sana kutotumia haraka lakini kuweka mbele maslahi mapana ya Taifa. Kwenye hotuba ya Waziri ameelezea kwamba tayari fidia ya eneo imeshafanyika sasa zile hatua zilizobaki za pre- FEDD decision, FEDD decision yenyewe lakini final investment decision na mpaka mradi uanze zifanyike kwa utaratibu mzuri ili Taifa liweze kunufaika.

Mheshimiwa Spika, vilevile naomba kuishauri Serikali wakati negotiation zinaendelea ifanye micro and macroeconomic study ili kuweza kuona mradi ule pamoja na faida zile za kifedha zitazopatikana kwenye mradi lakini faida nyingine mtambuka kwenye maeneo yale ya Lindi na Mtwara na maeneo mengine ya Taifa letu. Faida hizo ni muhimu ziweze kufahamika na kujulikana ili Serikali inapoingia kwenye mradi ule iingie kwenye jambo ambalo ukiangalia mtazamo mzima wa negotiation kwenye open book economic model haziangaliwi basi ziweze kuwa covered kwenye micro and macroeconomic study.

Mheshimiwa Spika, lakini tujifunze kwa Mozambique, wenzetu wameanza wako katika hatua nzuri sana na hivi tunavyozungumza mnafahamu vinafanyika vikao vya SADC katika kuangalia hali ya usalama ya Msumbiji. Niiombe Serikali itumie vikao hivi hivi kuweza kujifunza kwa wenzetu ili na sisi tufahamu hivi tunavyo-negotiate hatuhitaji msaada wa utaalamu maeneo mengine, hatuhitaji ushauri wa majirani zetu ili mradi huu uweze kufikiwa na Tanzania iweze kupata mapato.

Mheshimiwa Spika, kwenye huu ukurasa wa 68 mradi huu utagharimu siyo chini ya dola bilioni 30 sawa na trilioni 70 za kitanzania. Mradi huu ukianza kuzalisha mapato yanakadiriwa kuwa siyo chini ya dola bilioni 3 kama trilioni 7 kwa taifa letu. Niombe kuungana na wachangiaji wa jana akiwemo Mheshimiwa Getere kama itaipendeza Serikali akina Mheshimiwa Kalemani hawa wakipatikana wawili mmoja akahangaika na huu umeme wa REA akapatikana Kalemani mwingine kuhangaika tu na mradi huu wa gesi asilia itasaidia taifa kuweza kuongeza kasi na ufanisi katika kutekeleza mradi huu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, vilevile napenda kuchangia kama walivyosema wachangiaji wenzangu, niipongeze Waziri, Naibu Waziri na uongozi wa Wizara kwa kushirikisha Shirika la Viwango Tanzania (TBS) katika kufanya kazi adhimu ya kulinda kodi na mafuta ya nchi yetu. Ziko dhana nyingi wakati mwingine sisi wenyewe Watanzania tunapenda kujidharau na kuthamini vitu vya nje. Naomba Serikali katika jambo hili ilitilie mkazo na ilifanye kwa ufanisi.

Mheshimiwa Spika, naomba niseme Waziri wa Viwanda na Biashara ama Serikali kwa ujumla TBS iwezeshwe iweze kufanya kazi hii kwa ufanisi. Nasema hivyo maana hivi tunavyozungumza vifaa vidogo tu vya detection ya vinasaba bado TBS hawajapeleka EWURA. Wizara ya Viwanda na Biashara iko hapa, Serikali iko hapa iweze kuongeza nguvu, jukumu walilopewa ni kubwa iongeze nguvu TBS ifanye kazi hii kwa ufanisi kwanza kwa usalama wa Mtanzania lakini pili kwa usalama wa Taifa letu lakini tatu tunaamini Shirika hili ni la kizalendo na ni la Tanzania ambapo manufaa yoyote yatayopatikana yatakuwa kwa Watanzania. Serikali ifungue macho zaidi maana inawezekana Shirika hili likakwamisha mradi huu ili kuonekana tumefeli kuweza kujenga hoja maeneo mengine.

Mheshimiwa Spika, naunga mkono hoja, nakushukuru sana. (Makofi)