Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Nishati

Hon. Selemani Moshi Kakoso

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mpanda Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

2

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Nishati

MHE. MOSHI S. KAKOSO: Mheshimiwa Spika, nishukuru sana kunipa nafasi ya kuwa miongoni mwa wachangiaji wa kwanza asubuhi hii.

Mheshimiwa Spika, kwanza, niipongeze sana Serikali kupitia kwa Waziri mwenye dhamana kwa kazi nzuri ambazo wanazifanya, hasa kwenye mradi mkubwa wa Bwawa la Mwalimu Nyerere ambapo naamini mradi huu ukikamilika utatua tatizo la umeme kwa nchi nzima.

Mheshimiwa Spika, lakini nimpongeze sana Mheshimiwa Waziri kwa ajili ya Mradi wa Standard Gauge. Sisi kama Kamati ya Miundombinu tumeikagua reli, tumeshuhudia jinsi Serikali ilivyoanza kujenga vituo vya kupozeshea umeme kupitia Shirika la TANESCO ambalo naamini kabisa ndiyo tunategemea huo umeme uweze kuendesha Shirika hilo la Reli kupitia reli ya mwendokasi. Tunawapongeza sana.

Mheshimiwa Spika, nizungumzie sana mradi wa Grid ya Taifa, hasa kwa Mkoa wa Katavi. Mkoa wa Katavi unakua, una mahitaji makubwa lakini kwa bahati mbaya sana tunatumia umeme wa ma-generator ambao kimsingi haukidhi mahitaji ya watumiaji. Namuomba sana Mheshimiwa Waziri afanye mikakati ya haraka kuhakikisha Mradi wa Umeme wa Grid ya Taifa kutoka Mkoa wa Tabora kupitia Wilaya ya Sikonge uweze kukamilika haraka na ule mradi ambao unatokea Mkoa wa Mbeya, Songwe, Sumbawanga kuja Katavi nao ukamilike. Pia naomba ule Mradi wa Malagarasi, sisi Mkoa wa Kigoma ni jirani naamini ukikamilika utasaidia sana wananchi.

Mheshimiwa Spika, nizungumzie Mradi wa REA. Tunaishukuru sana Serikali imeleta Mradi wa REA kwenye maeneo ya Jimbo langu, Wilaya ya Tanganyika lakini vipo vijiji vingi ambavyo bado havijapata umeme. Nimuombe Mheshimiwa Waziri aweze kukamilisha miradi kwenye Kata ya Mishamo, Kata ya Bulamata, Ipwaga na Ilangu ambapo kwa ujumla vijiji vilivyobaki vipo 26 kwenye Jimbo la Wilaya ya Tanganyika. Nimuombe sana Mheshimiwa Waziri, pamoja na kutuletea mkandarasi ni vyema akawa na usimamizi wa karibu sana ili kuhakikisha miradi hii inakamilika. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini pamoja na kuleta wakandarasi, vipo viko vijiji ambavyo kwenye Mradi wa REA II vilisahaulika, hasa kwenye Tarafa ya Karema, kipo Kijiji cha Kasangantongwe. Naomba Mheshimiwa Waziri watakapokuwa wanakuja kukamilisha kwa sasa na vile vijiji vilivyokuwa vimesahaulika viwekwe kwenye mpango ili viweze kuwasaidia wananchi.

Mheshimiwa Spika, vipo vijiji ambavyo vilishapelekewa umeme. Kwa bahati mbaya sana vimepelekewa umeme lakini kwenye maeneo ya mitaa na vijiji, vitongoji vimekuwa havipati umeme wa kutosha. Naomba Mheshimiwa Waziri aweze kukamilisha taratibu za kupeleka umeme kwenye vitongoji kwani tunapopeleka umeme kwenye vijiji, tusipeleke tu pale kijijini, tunahitaji uwafikie wananchi kwenye mitaa mbalimbali. Naomba suala hili alishughulikie, naamini Mheshimiwa Waziri ni msikivu, ni Waziri pekee ambaye anawasikiliza sana Wabunge na anaenda kila sehemu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, amefanya ziara kwenye jimbo langu, naamini vijiji vingi ambavyo naviongelea yeye anavifahamu. Amefika pale Kasekese, Mchakamchaka, Ifukutwa, sehemu zote hizo amezindua miradi ya maendeleo ya REA Phase III. Kwa hiyo, naomba hivyo vijiji vilivyobaki avifanyie kazi.

Mheshimiwa Spika, ahsante. (Makofi)