Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Nishati

Hon. Joseph Michael Mkundi

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Ukerewe

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

2

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Nishati

MHE. JOSEPH M. MKUNDI: Mheshimiwa Spika, nashukuru sana kwa nafasi hii ya kusema maneno machache kwenye hotuba ya Mheshimiwa Waziri wa Nishati.

Mheshimiwa Spika, kwa kuanza nimpongeze sana Mheshimiwa Waziri, Naibu Waziri na watendaji wote wa Wizara. Wamefanya kazi kubwa sana kwa kipindi hiki.

Mheshimiwa Spika, na kwa mfano mdogo ukiangalia usambazaji wa umeme kimsingi kumekuwa na ufanisi kwa sababu kwa kipindi cha miaka takribani mitano, vijiji zaidi ya 8,000 vimepewa umeme kama nyongeza kwenye vijiji vya awali vilivyokuwa na umeme. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwenye eneo hili nitoe ushauri tu; pamoja na kwamba tumepeleka umeme kwenye vijiji zaidi ya 10,000 lakini ukiangalia wigo wa maeneo yaliyopelekewa umeme kwenye kijiji chenye vitongoji saba, umeme umepelekwa makao makuu ya kijiji na katika makao makuu ya kijiji umeme unapelekwa kwenye kaya zisizozidi 20. Bado wigo ni mdogo sana.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, utakuta vitongoji zaidi ya vitano, vitongoji sita kwa mfano kwa Ukerewe, vijiji vyenye vitongoji saba, kitongoji kimoja kwa kaya 20 pekee ndizo zimepata umeme, sehemu kubwa ya wanakijiji wanakuwa hawajapata umeme.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, bado tunahitaji kuwekeza pesa nyingi kwa TANESCO ili mradi unapofikisha umeme kwenye makao makuu ya kijiji basi TANESCO wabaki na jukumu la kusambaza umeme kwenye eneo la vitongoji ili mwisho wa siku basi wananchi wapate umeme na lile lengo tunalolitarajia la wananchi kunufaika na nishati hii, kujiletea maendeleo, tuweze kulifikia.

Mheshimiwa Spika, eneo la pili ambalo ninataka kuliongelea – nitaendelea kuongelea suala la umeme – ni juu ya kukatikakatika kwa umeme; Ukerewe tumekuwa na shida kubwa ya kukatikakatika kwa umeme kwa takribani miaka miwili sasa. Na chanzo cha kukatikakatika kwa umeme ni tatizo la submarine cable inayotuunganisha kati ya Kisiwa cha Ukerewe na Bunda.

Mheshimiwa Spika, ile cable imechoka na kwa maana hiyo imekuwa mara kwa mara maji yakigusa inakatika. Sasa imesababisha adha kubwa sana kwa wananchi wa Ukerewe, wawekezaji wanakimbia, wenye dhamira ya kuwekeza wanashindwa kuwekeza.

Mheshimiwa Spika, inaathiri kwa ujumla uchumi wa wananchi wa Ukerewe. Na wakati mwingine wananchi wenye uwekezaji wao kwenye Visiwa vya Ukerewe wanapata hasara kwa sababu vifaa vyao vingi vinaharibika.

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Waziri na timu yako niwapongeze; mmekuwa na jitihada kadhaa ambazo mmekuwa mnazifanya. Na hivi tunavyoongea ninashukuru angalau sehemu fulani ya kipande cha cable ile mmeweza kuipata. Lakini niombe; ile sehemu ya kipande kingine cha cable iweze kupatikana haraka, tuweze kupata suluhisho la kudumu la umeme kwenye Visiwa vya Ukerewe na hasa Kisiwa kikubwa cha Ukerewe.

Mheshimiwa Spika, wakati wa kusoma hotuba hapa Mheshimiwa Waziri kwenye hotuba yako ukurasa wa 51 umeongelea umeme wa maeneo ambayo yapo nje ya Gridi ya Taifa, pia maeneo ya visiwa. Ukerewe tuna visiwa 38, katika hivyo, kisiwa kikubwa kile, sawa tuna umeme wa Gridi ya Taifa; visiwa 37 vinavyobaki vyote tunategemea umeme wa jua na umeme mwingine kama ambavyo mtautoa kwenye maeneo yaliyo nje ya Gridi ta Taifa.

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Waziri, unajua katika visiwa 37 vya Ukerewe, ni visiwa vitatu pekee vidogo vyenye umeme; Kisiwa cha Ukara ambacho kinakuwa-supplied na watu wa Jumeme; Kisiwa cha Ilugwa ambacho kiko supplied na watu wa Jumeme na Kisiwa cha Liegoba ambacho kinakuwa supplied na watu wa Power Gen.

Mheshimiwa Spika, hawa watu wa Liegoba kwa umeme wanaopewa wanatozwa shilingi 1,000 kwa siku, wananunua umeme kwa bundle, bundle lile inanunuliwa shilingi 1,000, haijalishi yule mteja ametumia umeme ule au hajatumia mwisho wa siku lile bundle inakuwa haifanyi kazi tena na matokeo yake kesho yake yule mteja anatakiwa kununua tena bundle lingine la shilingi 1,000, kitu ambacho ni gharama sana kwa mwananchi wa kawaida. Mheshimiwa Dkt. Kalemani, nimekuwa ninakueleza jambo hili. Hii si sawa kwa mwananchi wetu wa kawaida, mwananchi wa Taifa hili. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwenye eneo la Ilugwa na Kisiwa cha Ukara ambapo wako supplied na watu wa Jumeme, ni kweli walikuwa wanatiozwa shilingi 3,500 kwa unit. Ulisema hapa Bungeni ukatoa maelekezo wakapunguziwa mpaka shilingi 100, lakini baada ya kupunguziwa na kuanza kulipa shilingi 100 wananchi hawa wakawa wanapata umeme kuanzia saa nne asubuhi mpaka saa 12.00, baada ya saa 12.00 usiku mzima wananchi hawana umeme.

Mheshimiwa Spika, nimeendelea kupiga kelele na hatimaye mwezi Machi wananchi wakaingia makubaliano mapya na watu wa Jumeme kwamba wako tayari kulipa shilingi 2,000 kwa unit ili tu waweze kupata umeme kwa saa zote 24. Hivi ninavyoongea pamoja na wananchi hawa kuendelea kulipa shilingi 2,000 lakini hawapati umeme kama inavyotarajiwa.

Mheshimiwa Spika, niombe sana Serikali iliangalie jambo hili, nimekuwa ninalisema mara kwa mara hapa lakini ifike mwisho sasa tuone kwamba huu mradi wa kusambaza umeme kwenye maeneo yaliyo off-grid angalau basi Visiwa vya Ukerewe viweze kunufaika na mradi huu. Vile ambavyo havijapata umeme moja kwa moja viweze kupelekewa umeme.

Mheshimiwa Spika, kwenye Visiwa kwa mfano vya Ghana, Bulubi n.k. mkandarasi alipeleka nguzo tokea mwaka 2016 akaziacha pale. Mpaka leo hakuna chochote kilichofanyika. Niombe watu wa Ukerewe wanahitaji huduma hii ya umeme, wanahitaji kuchochea maendeleo na maisha yao kwa ujumla wake, basi wapate nishati hii ya umeme. Hasa watu wa visiwa vidogo vile; watu wa Jumeme ule mgogoro wa bei uliopo uweze kutatuliwa na mwisho wa siku waweze kupata huduma hii ya umeme na waweze kufanya shughuli zao za kiuchumi kama tunavyowatarajia.

MHE. ERIC J. SHIGONGO: Mheshimiwa Spika, taarifa.

SPIKA: Ndiyo, endelea na taarifa hiyo.

T A A R I F A

MHE. ERIC J. SHIGONGO: Mheshimiwa Spika, nataka tu kumueleza mzungumzaji kwamba tatizo la watu wa kwenye visiwa kutozwa gharama kubwa ya umeme halipo kwenye visiwa vyake peke yake. Natoka kwenye Visiwa vya Maisome pamoja Zilagula ambako kwa hivi sasa tunavyoongea wananunua unit moja ya umeme kwa shilingi 2,400; nilitaka kuzungumzia jambo hilo. (Makofi)

SPIKA: Mheshimiwa Mkundi, unaipokea taarifa hiyo?

MHE. JOSEPH M. MKUNDI: Mheshimiwa Spika, napokea taarifa hiyo kwa mikono yote miwili. Na unaweza kuona namna gani wananchi wetu wanavyotaabika. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa mwananchi wa kawaida wa kijijini kununua unit moja kwa shilingi 2,000 au kama wanavyotoza kwenye Kisiwa cha Liegoba, ananunua unit kwa shilingi 1,000, bundle ile, halafu mwisho wa siku ile bundle iki-expire kesho yake anatakiwa kununua tena haijalishi ametumia au hajatumia, ni lazima Serikali i-intervene katika jambo hili. Ifike mahali wananchi hawa tuwape fursa ya kujiletea maendeleo kupitia nishati ya umeme.

Mheshimiwa Spika, baada ya kusema hayo, nilitaka kusema kwenye hayo maeneo matatu tu juu ya umeme. Lakini niombe sana Mheshimiwa Waziri; suala la cable inayotuunganisha kati ya Lugezi na Kisorya pale kupeleka umeme kwenye Kisiwa kikubwa cha Ukerewe, tupate ufumbuzi wa kudumu. Lakini suala la visiwa vidogo hasa kwenye eneo la bei vilevile tupate solution ili mwisho wa siku wananchi wa Ukerewe waweze ku-enjoy maisha na maendeleo ya Taifa hili. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, baada ya kusema hayo nashukuru sana kwa fursa. (Makofi)