Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Nishati

Hon. Tabasamu Hamisi Hussein Mwagao

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Sengerema

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Nishati

MHE. TABASAM H. MWAGAO: Mheshimiwa Spika, nakushuru sana kwa niaba ya jina la Jimbo la Sengerema naomba kuchangia mchango wangu katika bajeti hii ya nishati.

Mheshimiwa Spika, kazi ya uspika ni kazi ya ngumu sana, nilikuwa sijui wakati huo sijawa Mbunge lakini nimeona kwamba una kazi ngumu kiasi gani cha kwanza ni kwamba kuhakikisha Wabunge wako wote wana uwezo wa kufanya kazi katika maeneo gani katika hizi kamati. Mimi tu Mwenyezi Mungu alikuonesha maono kwamba mpeleke MheshimiwaTabasamu katika Kamati ya Nishati na Madini hongera sana kwa hilo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwanza lazima nikusifie wewe mwenyewe binafsi kuona Mheshimiwa Tabasamu ninafiti pale lakini ninachotaka kukuambia kitu kingine cha msingi sana kilichopo ni Mwenyekiti wa Kamati hii ni mzalendo wa kwelikweli. Yaani haya yote unayoona Waziri anafanikiwa ni kutokana na kamati hii ikiwa na mwenyekiti na msaidizi wake Naibu Mwenyekiti na sisi wajumbe kuwa wazalendo katika kamati hii. Tumezunguka katika kamati kuangalia hii miradi yote ya kimkakati miradi ya umeme mikubwa iliyopo na bado ndo tukaja na maono kuja kukusaidia kwamba tuangalie katika vina saba. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sheria ya mafuta na gesi ya mwaka 2015 nyinyi mmepitisha Bungeni hapa mnajua inazungumzia nini kuhusiana na suala la usalama wa mafuta kama ni usalama wa nchi, usalama wa Taifa. Lilikuwa ni kosa sana kuachiwa mtu binafsi aendeshe muhimili mkubwa kama huu kwa kuweka vina saba hili lilikuwa ni kosa tusilirudie tena katika nchi hii naomba Hansard iweke hiyo na ukiona mtu anakuja kuzungumza hapa kwamba GFI basi ujuwe kabisa halitakii mema Taifa hili tunahitaji uzalendo wa kweli kutoka moyoni katika jambo hili. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kampuni ya wajanja wawili watatu wanaondoka na milioni 168 kwa siku kwa miaka 6 poleni sana watanzania katika jambo hili inaumiza sana raia yoyote wa Tanzania ambaye ana machungu kwa ajili ya uzalendo wa nchi hii mkaja hapa mnakuja kuzungumza GFI kwanza hatujui amelika kodi kiasi gani kwa sababu ameanza kufanya kazi hii mwaka 2015 anachukuwa bilioni tano kila mwezi kwa mwaka ni bilioni 60 bajeti karibu ya wizara tatu kosa kubwa sana katika nchi hii.

Mheshimiwa Spika, huyu mtu kachukuwa bilioni 60 mpaka 72 kwa miaka 6 karibu bilioni 450 hatakiwa kumzungumza mtu huyu kweli tunakuja Wabunge tunakuja kuzungumzia habari ya GFI sasa hivi badala ya kuja kujipa pole kwa kazi hii vina saba ni nini? Vina saba ni mafuta hayahaya petroli hii, diseli hii, mafuta ya taa kinachowekwa ni chemical tu kidogo wajanja fulani bei ya dola moja anauza huyu SWISCAP wamekuja wawili kama partner mmoja SWISCAP anauza vina saba GFI anaweka vina saba halafu EWURA anakuja kukugua hivi vina saba kwa miaka sita.

Mheshimiwa Spika, leo tunaleta mawazo ya kizalendo kwamba TBS anatosha kuja kufanya kazi hii tuweze kupata pesa kuokoa hizi pesa ambazo walikuwa wanachukuwa wajanja wawili watatu kuna watu wanataka kuja kusema GFI aendelee kuweka haya mafuta jamani tunaitakia mema nchi hii. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ninachotaka kukuambia hapa kinachobakia ni uzalendo wa Waziri husika uzalendo wa kwako wewe kama Spika uzalendo wa sisi kama kamati tukushauri vizuri juu ya jambo hili huyu mtu sijui katika hii bilioni 60 alilipa kodi alilipa payee hatujui ulipaji wake wa kodi tunamuomba Waziri wa Fedha kwanza afuatilie watu waende wakaangalie GFI alilipa kodi kiasi gani na hili jambo lije lielezwe bunge haiwezekani huyu mtu tena aje arudi hapa mkataba wake umeisha mwezi wa tisa akaongezea kwa cotetion kazi ya bilioni 60 inaweza ikaongezwa kwa cotetion akaongezewa miezi mitatu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mwezi wa Kumi na Mbili, mkataba umeisha wa miezi mitatu akaongozewa miezi mitatu, tarehe 28 mwezi wa pili kaongezewa miezi mitatu inaumiza sana katika roho leo tunasema aweke TBS watu wanakuja kusema hapa sheria kwamba TBS hana sheria maana yake ni nini kuitwa TBS tunaomba tafsiri ya neno TBS ni nini?

Mheshimiwa Spika, hili shirika la viwango la Taifa viwango vya aina yoyote iwe gesi iwe mafuta kila kitu iwe dawa ndio kazi ya TBS. Sheria gani ije iundwe tena kwa ajili ya TBS na TBS huyu naomba kwa manufaa ya nchi niongezewe dakika kidogo naomba nakwenda kwa sababu nakwenda mbele huko kuna jambo kubwa nakuomba sana maana yake nasikia kengele inalia hii. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, hivi tunavyozungumza huyu TBS sasa hivi akiwezeshwa, akiwezeshwa wafanyakazi, miundombinu, akanunua hizi machine zinauzwa Finland zinauzwa Uturuki, machine zinauzwa China na hivi vinasaba ni vitu vinatengenezwa maabara tukatengeneza wataalam wetu wakaja wakafanya hii kazi kwa ajili ya uzalendo hili ni suala la usalama wa nchi hatakiwi kuachiwa mtu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwanza hatujui huyu GFI hii vina saba alivyokuwa anaviweka yeye katika hizi kampuni za mafuta katika nchi hii depo 22 amewauzia kiasi gani, ya kuwapa kwa sababu hana haki mali ni ya kwake…

MHE. AHMED M. SHABIBY: Mheshimiwa Spika, taarifa.

SPIKA: Taarifa unapewa na Mheshimiwa Shabiby.

T A A R I F A

MHE. AHMED M. SHABIBY: Mheshimiwa Spika nataka nimpe taarifa Mheshimiwa mzugumzaji kwamba hata kama TBS itafanya kwa bei kubwa bado ile pesa itaingia kwenye taasisi ya Serikali. Kuliko kufanya mtu binafsi nataka nimpe taarifa kwa sababu pesa itaingia kwake.

SPIKA: Unaipokea taarifa hiyo Mheshimiwa Tabasamu.

MHE. TABASAM H. MWAGAO: Mheshimiwa Spika kwa mikono sabini. (Makofi/Kicheko)

Mheshimiwa Spika, ni kwamba hivi vina saba SWISSCAM alikuwa anamuuzia GFI kwa dola saba kwa cubic 5 lakini sasa hivi baada ya kuonekana GFI kakosa kazi SWISSCAM anamuuzia vina saba TBS kwa dola 3.5 na mimi kwa ajili ya uzalendo nimekwenda kumfuata Mkurugenzi wa TBS DG nikamwambia hata hiyo bei bado umewapa kubwa agiza wewe mwenyewe Finland Uturuki utapata kwa 0.8. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, haya maneno ya wizi ukome katika nchi hii ninachotaka kuwaambieni kama Mheshimiwa Tabasamu nimetishiwa kuuwawa kwa ajili ya hawa watu wa GFI, kuleta habari hizi tu hapa Bungeni nikatishiwa kuuwawa nimemwambia Mheshimiwa Spika na kesi hii iko hapo kwa RPC Dodoma, na hatujapata majibu walionipigia simu na namba zao ziko pale kwa ajili ya kunitisha kazi hiyo umefanyiwa wapi.

Mheshimiwa Spika, naomba na hili unisaidie kunilinda kwa ajili ya uzalendo nimeleta jambo hili kwa sababu tunatafuta pesa za barabara za TARURA, hivi ninavyozungumza na wewe ukiondoa kodi iliyopo hapa kwenye mafuta kwa mfano kwa mwezi huu mambo haya ni madogo sana kwa mwezi huu tu peke yake kodi ya petrol ilikuwa ni shilingi 792, kodi ya diesel ilikuwa ni shilingi 600 kama sikosei hapa kwa lita 666, kodi ya mafuta taa ilikuwa ni shilingi 615 lakini tozo zilizoko hapa nitakuprintia karatasi kesho nikuletee vikampuni vidogo vidogo ambavyo viko kwenye idara zetu mpaka zimefika pamoja na huyu GFI alivyokuwepo tumefikisha shilingi 92 tozo peke yake. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ukichukuwa kodi ya shilingi 790 Mheshimiwa Waziri wa Fedha nisikilize upo hapa hii ndio inayoingia hazina na katika hiyo shilingi 790 kuna shilingi 100 kwa ajili ya petrol fee hii ni kwa ajili ya utafiti wa petrol na mambo mengine. Pesa inayobakia 690 ndio kodi. Hii shilingi 92 hii inaenda tena kama tozo kwa sababu tunakuja kwenye bajeti kuu ntakuja kukukaba huko hawa kwa nini wanaleta tozo kodi nyingine hii tozo ikatwe kule iende TARURA habari ya kutuambia kwamba TARURA imepewa bilioni 150 kwamba kila halmashauri imepewa milioni 500 ni kuja kutufunga mdomo hili tusisema hili jambo haiwezekani Wabunge katika jambo hili. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, katika jambo hili hii shilingi 92 chukueni calculator zenu shilingi 92 hizi ambazo zinapotea hapa wanachukuwa huko zinakwenda kwenye tozo kutumika vibaya hizi zikipigiwa hesabu kwa siku tunauza petrol peke yake. Lita 5,600,000. Diesel tunauza lita 6,200,000, mafuta ya taa kama lita 100,000 kwa siku ukichukua hapa hizi shilingi mabilioni ya shilingi kwa kila siku hizi zinatosha kwenda TARURA, jamani inakuwaje haya maneno leo mimi nakuja kutishiwa kuuwawa kwa sababu nimeleta jambo hili heri nife kwa ajili ya Tanzania Spika utanilinda. (Makofi)

MHE. EDWIN E. SWALLE: Mheshimiwa Spika, taarifa.

T A A R I F A

MHE. EDWIN E. SWALLE: Mheshimiwa Spika, napenda kutoa taarifa kwa mzungumzaji Mheshimiwa Tabasamu kwamba kwa ukubwa wa hoja ambayo anaizungumza inayohusu uzalendo wa nchi nimemwomba Mheshimiwa Tabasam nimpe taarifa kwamba ni vizuri Waziri wa Nishati atakapokuja ku-wind up atoe commitment ya kumpa ulinzi kwa ajili ya usalama wake pia.

SPIKA: Bahati mbaya hahusiki sana na masuala ya usalama; endelea kuchangia Mheshimiwa Tabasam, Serikali imesikia.

MHE. TABASAM H. MWAGAO: Mheshimiwa Spika, naendelea kukushukuru. Ninachotaka kukwambia ni kwamba hapa tuna mambo mengi sana kuhusiana na hili suala la vinasaba. Hivi vinasaba inaweza ikaandaliwa bajeti tu ya kununua vinasaba vya mwaka mzima ambavyo haviwezi kuzidi bilioni 10 au 15, huyu TBS akaendelea kuweka na ile hela ambayo ilikuwa inakwenda TBS au GFI yote iletwe TARURA. Haya maneno gani haya? Kwa sababu lile ni shirika la Umma linawajibika kufanya kazi ya Umma. Hizi pesa tuziokoe ziende huko. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, hivi ninavyozungumza na wewe naomba tu nitoe ushauri wangu mdogo sana kuhusiana na hili suala la umeme. Hili suala la umeme kwa mfano sasa hivi tunapata shida sisi ya kusambaza umeme vijijini, nguzo zipo. Haya, utengenezaji wa nguzo TANESCO sasa ifikie mahali inunue mashine yake ya kokoto, inunue mashine ya kutengeneza nguzo, iwe na mashine yake itengeneze nguzo migogoro hii iishe.

Mheshimiwa Spika, lakini suala hili la kufanya kazi hizi kwa kutumia wakandarasi, tunashukuru Mungu tunakwenda kwa kasi, vifaa vingine vinatakiwa viwe vyetu. Nakushukuru Mheshimiwa Waziri wa Nishati kwa uzalendo wako, endelea kuwa mzalendo hivyo hivyo; Naibu Waziri, endelea kuwa mzalengo; Katibu Mkuu, endelea kuwa mzalendo. Simamieni hii hali ya mafuta.

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Waziri Mkuu, tunakuomba utuuonge mkono katika hili suala sisi Kamati ya Nishati na Madini kwa kazi nzuri tuliyoifanya kuishauri Serikali kuwaondoa GFI. Tupigiwe makofi ndani ya hili Bunge. Lakini habari hii hapana. (Makofi)

SPIKA: Ahsante sana.

MHE. TABASAM H. MWAGAO: Mheshimiwa Spika, naomba kuunga mkono hoja; ahsante sana. (Makofi)