Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki

Hon. Ng'wasi Damas Kamani

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki

MHE. NG’WASI D. KAMANI: Mheshimiwa Naibu Spika, na mimi nianze kwa kukushukuru kwa kunipa nafasi hii ya kuchangia katika Wizara hii. Lakini pili, nimpongeze Mheshimiwa Waziri na timu yake yote kwa kazi kubwa ambayo wamekuwa wanafanya kuendelea kuimarisha mahusiano yetu na nchi jirani. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nianze tu kwa kutoa takwimu ndogo iliyotolewa na Benki ya Dunia ambayo inaonesha kwamba kati ya mwaka 2018 mpaka mwaka 2030 idadi ya watu wenye uwezo wa kufanya kazi kwenye nchi zenye uchumi wa chini na uchumi wa kati itaongezeka kwa idadi ya milioni 552. Lakini idadi ya watu wenye uwezo wa kufanya kazi kwenye nchi zenye uchumi wa juu kwa kipindi hiki hiki, itashuka kwa idadi ya watu milioni 40.

Mheshimiwa Naibu Spika, maana yake ni kwamba nadhani ni wakati Serikali yetu, hasa Wizara hii tunayoichangia leo, ikaanza kuangalia ni namna gani tuta-tackle ongezeko hili la watu kwenye nchi yetu ambayo itakuwa ni general kwa Bara letu, lakini pia tutatumia vipi fursa ya upungufu wa watu wenye uwezo wa kufanya kazi kwenye nchi za wenzetu ili kuweza ku-facilitate Watanzania kwenda kuziba pengo hilo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, niombe tu kuishauri Wizara hii iangalie namna gani inaweza kushirikiana na Wizara ya Elimu kuhakikisha kwamba ifikapo muda ambao gap hili tunaanza kuliona kwa ukubwa basi watu wetu wa Tanzania wawe na skills za kutosha kuweza kukidhi nafasi hiyo, hasa vijana wa Tanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini pia takwimu hizi hizi zinaonesha kwamba kufikia mwaka 2050 mazingira ya Kiafrika yatakuwa uninhabitable kwa maana ya mabadiliko ya tabia nchi kama tusipochukua hatua za kutosha kurekebisha shida zilizopo katika mazingira. Maana yake hii pia inaiamsha Wizara hii kuangalia kwamba ni namna gani sasa tunatumia mahusiano yetu ya kimataifa kuhakikisha kwamba watu wetu wanaweza kufaidika na mahusiano hayo.

Mheshimiwa Naibu Spika, ningependa pia kutaka kujua kutoka kwa Wizara hii ina mikakati gani ya kuhakikisha kwamba ina-scout vya kutosha kupitia Balozi zetu zilizopo katika nchi mbalimbali, fursa mbalimbali, mikopo na grants ambazo zinaweza zikatumiwa na vijana wetu wa Kitanzania kujinufaisha na mahusiano ambayo tumeendelea kuyajenga kwa gharama kubwa na kwa muda mrefu kati ya nchi yetu na nchi jirani. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pili, ni namna gani Wizara hii inajenga hamasa kwa Watanzania hata fursa hizi zinapopatikana wazichangamkie. Lakini si kuwahamasisha tu, bali kuendelea kuwajengea uwezo ili hata wanapopata fursa hizi wazitumikie ipasavyo na kuweza kuifaidisha nchi yetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, tunategemea kwamba mahusiano tuliyonayo kati ya nchi yetu na nchi zingine itufaidishe sawasawa na inavyowafaidisha wale tulio na mahusiano nao. Lakini pia sisi vijana wa Tanzania tunategemea sana kupata taarifa ya fursa zote zilizopo katika nchi nyingine kupitia Wizara hii.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini ni jambo la kusikitisha kwamba hata ukiingia kwenye website ya Wizara hii, fursa wanazoelezea ni zile ambazo zinapatikana ndani ya nchi yetu. Hakuna sehemu ambayo mimi kijana wa Kitanzania nitakwenda kwenye website ya Wizara hii nipate kujua fursa zilizopo nchi nyingine ili mimi niweze kuzifanyia kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini si tu kuona hizo fursa, hata nione kwamba kuna nini nchi gani, lakini hata niende kwa nani, niende wapi, niwasiliane na nani, ili niweze kupata fursa hizi. Kwa hiyo, sisi kama vijana wa Kitanzania tunaomba Wizara hii iboreshe mifumo yake ya taarifa ili tuweze kupata taarifa ya fursa zote zinazopatikana kule na tuzichangamkie. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ninaomba pia Wizara hii iangalie namna gani tunakuza wingi wa watu wetu wanaokwenda kufanya kazi katika nchi za wenzetu ili tuongeze mapato na si mapato tu, tuongeze pia skills, knowledge na technological transfer kutoka kwenye nchi za wenzetu kuja kwetu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sisi kama vijana tunasema sawa, pesa tunapata kama mapato, japo hata ukilinganisha remittances tunazopata Tanzania ni tofauti sana na zile ambazo nchi nyingine zinapata. Mfano mdogo mwaka 2018 Nchi ya Egypt imepata kipato cha USD bilioni 28.9 kama remittance kutoka nje. Nigeria mwaka huohuo wamepata dola bilioni 24.3. Wakati nchi yetu ya Tanzania kwa mwaka huo ime-register kipato cha dola milioni 365.

Mheshimiwa Naibu Spika, wenzetu wanaongelea dola bilioni ishirini na kitu, sisi hata bilioni moja hatujafika. Maana yake ni kwamba hatutumii vizuri mahusiano tuliyonayo na nchi nyingine, tunayoendelea kuyajenga kwa kutumia kodi za Watanzania kujinufaisha kama nchi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nadhani ni wakati sasa Wizara hii iangalie, mahusiano haya tunayoyajenga, je, yana manufaa kwetu? Je, ni mahusiano ya kimkakati? Na kama ni hivyo, basi kuanzia sasa tuanze kutengeneza mahusiano ya kimkakati ambayo tunajua as much as tunawafaidisha wengine na sisi Watanzania tunafaidika. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, na faida zinazopatikana zimguse Mtanzania, ikiwa ni pamoja basi na kuangalia namna gani tuna-bridge gap ya ajira kwetu kwa kuwachukua watu wetu waende ili wazidi kuturudishia mapato zaidi.

Mheshimiwa Naibu Spika, hatuongelei tu suala la mapato, tunaongelea pia suala la technology, suala la knowledge na skills. Nchi za wenzetu wanakwenda mbali kuanza kuchukua watu kuanzia ngazi ya chini wakiwa na umri mdogo kwenda kuwafundisha kwenye nchi za wenzetu ili wapate knowledge na technology waturudishie kwenye nchi zetu. Tanzania bado mpango huo uko chini kabisa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nadhani mahusiano tunayoyajenga tunayajenga na nchi husika lakini siyo na Watanzania walioko kwenye nchi husika. Inasikitisha sana kwa mfano nchi ya Finland kwenye Kampuni ya Nokia, zaidi ya asilimia 80 ya ma-engineer walioko pale ni Watanzania, lakini kitu kinachoonesha kwamba hatuna mahusiano nao mazuri ni kwamba mpaka leo hatuna hata kampuni ya simu kwenye nchi yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, na tungekuwa na mahusiano nao mazuri maana yake wangeweza ku-transfer technology hiyo, wakaja hapa na kutupa hiyo teknolojia basi tukazidi kutengeneza ajira na kukuza uchumi wa nchi yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ninashauri na Wabunge wenzangu wengi wameshauri tuwe na database ya kuonesha idadi ya Watanzania wetu waliko nje, na si kuwa na database ya ujumla, database hii tui-cluster kwa maana ya kutenga watu wenye profession fulani, watu wenye kazi zingine kulingana na umuhimu wao ili tujue tunawa-support vipi watu hao na watatuletea nini kwenye nchi yetu, hivyo ndivyo tunavyoweza kunufaika na mahusiano yetu na nchi zinazotuzunguka. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, niwapongeze, tumefungua Consulate General Lubumbashi, lakini utajiuliza taasisi zipi za Kitanzania au makampuni yapi ya Kitanzania yanasaidiwa na Wizara hii kwenda na yenyewe kufungua au kuanza kufanya kazi zake katika nchi za wenzetu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, wote tunajua kwamba tuna taasisi nyingi za kifedha, kwa mfano tuna CRDB, NMB, NBC, taasisi ambazo zina nguvu na uzoefu, hata nguvu ya kifedha pia inajitosheleza. Lakini taasisi za kifedha ambazo zinafanya kazi kwenye nchi zingine zote ni taasisi za Kikenya, tuna Equity Bank, KCB na hata Mtanzania akitaka kufanya kazi, japokuwa tuna Ubalozi Kenya, akifika mpakani anaachana na benki za Kitanzania anaanza kutafuta namna ya kufanya kazi na benki za kigeni. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa nini tusiwape nguvu hata taasisi zetu na zenyewe zisambae kwenda kwenye sehemu mbalimbali ambao tuna mahusiano nayo ili kukuza uchumi wa nchi. Kwa hiyo, bado rai yangu ni kwamba mahusiano tunayoyatengeneza yasiwe mahusiano tu ya diplomacy bali tuwe na faida kwenye mahusiano hayo. Na faida hizi basi tuzitengeneze kiuchumi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nipongeze pia Wizara hii na Mama yetu Samia Suluhu Hassan, juzi tumempokea mfanyabiashara mkubwa Dangote, hilo ni jambo zuri sana kwa sababu anasaidia kuwekeza na kujenga ajira. Lakini hii iwe ni kama wake up call. Tuna wafanyabiashara wakubwa sana kwenye nchi yetu, namna gani na sisi tunaweza kuwa-promote kwenda kuwekeza na kutambulika kwa ukubwa kwenye nchi zingine kama sisi tunavyowatambua wafanyabiashara wa nje. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, basi kama wamekwenda kuwekeza, je, Serikali ina mkono kwenye uwekezaji wao au wamekwenda kuwekeza kwa nguvu zao wenyewe, na hata baada ya wao kwenda kuwekeza kule, Serikali inawashika vipi mkono. Kwa hiyo haya yote ni mambo ambayo lazima tuyaangalie na tusiwe tu tunakaribisha wawekezaji wa nje kuja ndani bila sisi kutoa wawekezaji wetu wa Kitanzania waende wakawekeze nje, hiyo ndiyo namna ambayo tutakuza uchumi wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema hayo, naunga mkono hoja. Ahsante sana. (Makofi)