Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki

Hon. Jerry William Silaa

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Ukonga

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki

MHE. JERRY W. SILAA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi na mimi kuchangia bajeti hii ya Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa.

Mheshimiwa Spika, kwanza nichukue fursa hii kuwapongeza Mheshimiwa Balozi Libelata Rutageruka Mulamula kwa uteuzi wake wa kuwa Waziri wa Wizara hii, lakini na Mheshimiwa Naibu Waziri, Mheshimiwa Balozi Mbarouk Nassor Mbarouk.

Mheshimiwa Spika, nichukue fursa hii vilevile kuwapongeza Watendaji Wakuu wa wizara, kaka yangu na rafiki yangu Balozi Joseph Edward Sokoine na Mheshimiwa Balozi Fatma Mohammed Rajabu kwa kuteuliwa kuwa Naibu Katibu Mkuu wa Wizara hii ya Mambo ya Nje. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini nichukue fursa hii kumpongeza sana Mheshimiwa Rais, Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan kwa kuteua wanadiplomasia wabobezi kwenye Wizara hii, lakini kwa kuzingatia si tu mgawanyiko wa Muungano wa nchi yetu lakini vilevile na jinsia kwenye teuzi zake. (Makofi)

Mimi naamini kama wachangiaji wengine kwamba ubobezi wa wana diplomasia hawa kwenye Wizara hii utaleta matokeo chanya kwenye utendaji wa kazi wa Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa na kazi yetu sisi ni kuwaunga mkono, kuwatia moyo na kuendelea kuwasadia kuhimiza Serikali kutenga fedha za kutosha kama walivyoomba kwenye bajeti yao. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nimeisikiliza kwa makini hotuba ya Mheshimiwa Waziri na mimi niungane na wenzangu kupongeza kazi kubwa Wizara hii inayofanya kwenye eneo la economic diplomacy, wamefanya kazi kubwa, miradi mingi inatekelezwa na Wizara hii inaratibu na yapo mambo mengi baadhi ya Wabunge walioanza kuchangia wametoa wito, namie nitoe wito kwa Wizara hii kuongeza nguvu kwa kuisemea na kuitangaza nchi yetu. Na mimi naamini kama Serikali itachukua ushauri wa Mheshimiwa Mbunge Balozi Pindi Hazara Chana na kufungua Balozi nyingi zaidi, lakini si tu kufungua Balozi na kuziweka strategic, umetolewa mfano mzuri sana hapa, leo watanzania wengi wanakwenda China kufanya biashara, lakini ukimuuliza mtanzania wa kawaida kama amewahi kufika ubalozini Beijing hata hafahamu ni eneo gani. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Watanzania wangi wanafanya biashara kweye Miji ya Guangzhou, Shenzhen, Yuan na hata kama tutashindwa kupata Balozi mdogo basi hata ukipata Honorary Consular maslahi ya Watanzania kibiashara yatalindwa kwenye maeneo yale. (makofi)

Mheshimiwa Spika, ningeomba Wizara imefanya kazi kubwa kwenye utalii, lakini iongeze kazi kubwa ya kutangaza utalii kwenye balozi zetu kwa sababu utalii ni moja ya kati ya sekta ambazo inategemewa sana kwenye uchumi wetu kutuingizia pato la kigeni.

Mheshimiwa Spika, katika mchango wangu ningeomba kuchangia kwenye eneo la itifaki, ukurasa wa 87 wa hotuba ya Mheshimiwa Waziri. Na ningemuomba Waziri pamoja na ubobezi wao wa diplomasia nimrudishe kwenye sheria, kwenye Katiba ambayo ndio sheria mama ya nchi yetu. Nimuombe Waziri nimrejeshe kwenye Ibara ya 4(2) ya Katiba yetu ambayo inaeleza utawala wa nchi yetu ulivyogawanyika katika mihimili yake mitatu; kwa maana ya Serikali, Bunge na Mahakama. (Makofi)

Lakini nimrudishe kwenye Ibara ya 62 ya Katiba yetu ambayo inalitaja Bunge na kuelezea kazi na mamlaka ya Bunge letu. Lakini Ibara ya 66 inayowaelezea Waheshimiwa Wabunge, Ibara ya 84 inayomwelezea Spika wa Bunge letu hili la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Lakini na Ibara ya 85 inayomwelezea Naibu Spika na Ibara ya 105 inayoelezea Baraza la Wawakilishi la Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa nini naeleza ibara hizi? Kumekuwa na dhana na wenzetu wanaosimama itifaki ya shughuli zetu za kitaifa. Unakwenda kwenye shughuli ambayo Mheshimiwa Spika amehudhuria, unafanyika utambulisho Mheshimiwa Spika hatambulishwi. Si tu kutokumtambulisha ni fedheha kwake yeye binafsi, maana inawezekana Spika wetu Job Ndugai wote mnafahamu ni mtu rahim na mtu ambaye hana makuu. Lakini usipomtambulisha Spika maana yake umeamua wewe mwenyewe kuandika Katiba yako mpya na kuondoa Bunge ambalo linawakiwalisha wananchi wa Tanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini haiishii kwa Spika, zipo shughuli nyingi wanakwenda Waheshimiwa Wabunge na Waheshimiwa Wabunge wakienda vilevile tusiangalie wao kwa majina yao, wanakwenda kuwawakilisha wananchi wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwenye shughuli zile. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ziko shughuli anakwenda Mheshimiwa Naibu Spika, ziko shughuli wanakwenda Wenyeviti wa Kamati za Kudumu za Bunge. Ziko baadhi ya shughuli ambazo uratibu wa itifaki una-fail na Waheshimiwa Wabunge wanakuwa kama ma-gate crasher kwenye shughuli zile. Kuingia tabu mpaka watu waulizane wee mtu asimame pale mlangoni kila anayepita anakushangaa, bwana vipi! Tupo tumekuja kwenye shughuli. Kila anayepita anakuonea imani, wamekuona? Enhee wameniona wanashughulikia. Mpaka itokee hisani ama kiongozi wa itifaki afike aseme basi andika jina lako uingie. Lakini ndani ya shughuli ile utambulisho utatambulishwa sisemi kwa sababu Babu Tale hapa hayupo mpaka wasanii watatambulishwa, Mheshimiwa Mbunge hajatambulishwa.

Sasa hatusemi haya kwa maana tu ya kusema labda Wabunge wanataka makuu, hapana. Nayasema haya kwa kuwa Katiba inatambua nafasi hizi. Shughuli inapoandaliwa, viongozi wanapoalikwa, wanapofika wapate heshima na stahiki inayostahili. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nikiri Mheshimiwa Waziri ameliona, Mheshimiwa Naibu Waziri ameliona na Mheshimiwa katibu Mkuu ameanza kulifanyia kazi, ni Mabalozi wazuri wanafanya kazi vizuri sana. Nalisema kuweka kumbukumbu sahihi kwa kuwa nawaamini sana viongozi hawa niliowapongeza mwanzo wa mchango wangu. Kulikuwa na dhana kwamba shughuli hii inaandaliwa na Ofisi ya Waziri Mkuu, shughuli hii inaandaliwa na TPDC, shughuli hii inaandaliwa na TANESCO, ukisoma vizuri utaratibu wa shughuli za Kitaifa na za Kimataifa huwezo ukaondoa majukumu ya Idara ya Itifaki ya Wizara ya Mambo ya Nje katika kusimamia itifaki ya shughuli zile. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo nimuombe Waziri bahati nzuri umekuja na mzee na nilidhani atatoka baada ya kutambulishwa, lakini amebaki. Kwa heshima yake, twende kwa utaratibu wa kushauri, naamini ukija kuhitimisha hotuba yako utahitimisha vizuri na kunyoosha itifaki ya shughuli zetu.

Mheshimiwa Spika, na nikuambie kwa dhati ya moyo wangu, ikitokea tena Spika wangu wa Bunge hili aidha kwa makusudi ama kwa bahati mbaya kwenye shughuli yoyote hakutambulishwa au hakupewa itifaki inayostahili Mheshimiwa Waziri utakutana na jambo linaitwa Azimio la Bunge na wala usitafute mchawi, mimi nimeamua kununua hiyo kesi. Lakini sina shaka na wewe, sina shaka na Naibu Waziri wako na watendaji wako, naamini mtajipanga vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, yako hayo na mengine madogo madogo tu, hata Rais wetu anaenda kwenye shughuli haijulikani gari linasimama wapi, anashuka watu wamejipanga upande huu anashukia upande mwingine. Ni majukumu yenu, chukueni role yenu ya itifaki na msikubali mtu yeyote akachukua majukumu ambayo sio ya kwake kwa kuwa majukumu ya itifaki ni majukumu yenu chini ya Wizara yenu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mimi naamini haya yakifanyiwa kazi na yale ambayo wachangiaji wenzangu wamechangia, Wizara hii ikawezeshwa kwa fedha sit u kutengewa fedha lakini kuhakikisha fedha zinapelekwa hasa katika uwekezaji wa majengo ya ubalozi kwenye nchi ambazo tuna uwakilishi na kufungua Balozi nyingine za ziada. Wizara hii ikija hapa mwakani itakuja na mafanikio makubwa kuliko ilivyofanya hivi sasa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana na naunga mkono hoja. (Makofi)