Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo

Hon. Francis Kumba Ndulane

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kilwa Kaskazini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

2

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo

MHE. FRANCIS K. NDULANE: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru kwa kunipa nafasi kwa mara ya pili leo kuinuka kwenye kiti changu na kuweza kuzungumza na kuweza kuchangia bajeti ya Wizara ya Michezo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mimi kwanza ninapenda kujikita kwenye michezo na baadaye kama nafasi itaruhusu basi nitaongelea pia upande wa habari.

Mheshimiwa Naibu Spika, Kwanza nashukuru na kuwapongeza uongozi mzima wa Wizara ya Michezo kwa namna ambavyo imekuwa ikishirikiana vizuri na Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF) na ningependa nijitambulishe uhusika wangu kwenye michezo, mimi ni Mjumbe wa Kamati ya Utendaji ya Shirikisho wa Mpira wa Miguu Tanzania (TFF), lakini pia ni Makamu Mwenyekiti wa Kamati ya Mipango na Fedha ya Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania. Na nimekuwa Mjumbe wa Mkutano Mkuu wa TFF kwa miaka 14 hivi sasa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo napenda kwanza kupongeza ushirikiano uliopo kati ya Serikali na TFF, Serikali imetusaidia mambo mengi katika kuboresha mpira wetu wa nchi hii ya Tanzania. Tumeshuhudia mwaka juzi wakati tunajiandaa na mashindano ya Under Seventeen Barani Afrika iliweza kujitolea jumla ya shilingi bilioni moja, kwa kweli zilitusaidia sana na zimeboresha mambo mengi katika yale mashindano. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini kutokana na ushirikiano uliopo ndani ya miaka minne iliyopita tumeweza kushiriki mashindano ya CHAN pamoja na mashindano ya AFCON kwenye senior teams. Lakini vilevile tumetoa mataji tisa kwenye mashindano mbalimbali ya kimataifa ikiwemo mataji kwa timu za wanawake na vijnaa, lakini vilevile tumekuwa na mafanikio makubwa kwenye ligi yetu ya Tanzania Bara. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ligi yetu miaka minne iliyopita ilikuwa kwenye nafasi za ishirini huko, lakini kutokana na ushirikiano mzuri kati ya Serikali, wawekezaji kwenye football, lakini na TFF basi sasa ligi yetu inashika nafasi ya nane kwa ubora Barani Afrika. Tunazizidi nchi za Nigeria na Algeria ambazo kwa miaka mingi zilikuwa kwenye nafasi tano za juu, sasa zinashika nafasi ya tisa; ya kumi na kuendelea, sisi nafasi ya nane. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, na kutokana na maboresho ya ligi ambayo tunayo ndiyo maana vilabu vyetu ambavyo vinatuwakilisha katika mashindano ya kimataifa vya Simba na Namungo vimetuwezesha kufika katika hatua nzuri ya mafanikio kuliko kipindi chochote tangu Uhuru wa nchi hii. Hii inatokana na ubora wa ligi ambayo inaendeshwa katika nchi hii. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo napenda kuwapongeza Klabu ya Simba ikiongozwa na Mwenyekiti wake ambaye ni Mbunge wa Jimbo langu mstaafu, Ally Murtaza Mangungu pamoja na Mwenyekiti wa Bodi ya Wakurugenzi ya Simba, pamoja na Mtendaji Mkuu wa Club ya Simba, Dada yangu Barbara Gonzalez. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini nitakuwa mchache wa fadhila kama nisipoipongeza timu ya Namungo kwa kazi nzuri ambayo wamefanya hasa msimu huu uliopita, katika msimu wake wa kwanza klabu ya Namungo imeweza kufanya vizuri katika ligi kuu pamoja na mashindano ya FA na hatimaye ikaweza kutuwakilisha katika mashindano ya kimataifa kwenye kombe la shirikisho kwa mafanikio makubwa na mafanikio haya yaliongozwa na kaka yangu, rafiki yangu Mbunge wa Jimbo la Tunduru Kaskazini, Mheshimiwa Hassan Zidadu, hongera sana Mheshimiwa Hassan Zidadu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini vilevile ningependa sasa kushukuru kwa namna ambavyo hotuba ya Wizara, lakini pia hotuba ya Mheshimiwa Rais wetu alipofika hapa Bungeni kwa kuonesha nia ya dhati ya ku-support timu zetu za Taifa. Katika nchi za jirani ambazo zimepiga hatua kuliko sisi kwenye rank za sifa na mambo mengine tumeshuhudia zikiwa zina- support timu zao kwenye mambo mengi kwenye training session zao, lakini vilevile zinapokwenda kushiriki mashindano mbalimbali katika maeneo ya kuwapa usafiri wa kwenda kwenye mashindano hapo Kenya tu na Uganda wamekuwa wakifanya hivyo kwa miaka mingi hivi sasa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, vilevile kwenye masuala ya accommodation wanapokwenda kucheza mashindano nje ya nchi, lakini pia kwenye posho za kujikimu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo ningeomba tu kwa kuanzia Serikali yetu niishauri iwekeze kwenye hayo maeneo katika kuzi-support timu zetu za Taifa. Lakini vilevile pamoja na mafanikio ya timu ya Simba kulikuwa na wimbi la watu wengi kujaribu kuipiga vita timu ile, wamekuwa wakipokea wageni jambo ambalo mimi sijawahi kuliona katika nchi yoyote wakati nilipokuwa naongozana na timu ya Simba kwenda katika mashindano mbalimbali. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mwaka juzi nilipata nafasi ya kuwa head of delegation wakati timu ya Simba ilipokwenda kucheza na timu ya Nkana FC, lakini pia ilipokwenda kucheza na timu ya Saura kule Algeria, tulipofika Algeria tulioneshwa vidole saba, kwa sababu mwaka uliotangulia timu yetu ya Taifa ilifungwa goli saba kule Algeria, Algiers. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini tulipofika Zambia kule Kitwe tulivyotua na ndege tu pale Ndola tulikuwa tunaonyeshwa vidole vinne kwa sababu kwa mara ya mwisho Simba ilipokwenda Zambia ikacheza katika uwanja wa Ndola ilifungwa goli nne, lakini cha ajabu na cha kusikitisha katika nchi hii wametokea watu hivi sasa timu ngeni zikija zinapata kupokelewa na ukiangalia yale mapokezi huwa yanaratibiwa na watu ambao wana akili zao, siyo wale washabiki wa kule Uzuri kwa Mfugambwa au kule Somanga, Kilwa. (Makofi)

MHE. SEIF K. S. GULAMALI: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nimpe Taarifa.

MHE. FRANCIS K. NDULANE: Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo mimi ningeomba Serikali ijikite katika kuwafundisha uzalendo wananchi wetu ili mwakani tunapokwenda kucheza timu nne basi hizi vurugu vurugu zisiwepo timu zetu ziweze kufanikiwa vizuri.

T A A R I F A

MHE. SEIF K. S. GULAMALI: Mheshimiwa Spika, Taarifa.

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Ndulane kuna taarifa kutoka kwa Mheshimiwa Gulamali.

MHE. SEIF K. S. GULAMALI: Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kumpa Taarifa mzungumzaji anayezungumza sasa hivi kwanza moja atumie lugha ya Kibunge anapochangia na kuzungumzia juu ya kutoa lugha ambazo zinaonesha kama vile hao wanaounga timu zingine, lugha hizo ambazo anatumia si nzuri. Lakini kingine…

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Gulamali ngoja lugha gani iliyotumiwa, kwa sababu mimi hapa nasikiliza Wabunge wote wanaochangia, lugha gani ya Kibunge aliyoisema?

MHE. SEIF K. S. GULAMALI: Mheshimiwa Naibu Spika, lugha ambayo imetumika ni kuonesha kama vile timu ambayo wanayoizungumzia kwa mapenzi yake yeye ni kama timu ya Taifa ya Tanzania. Kwa hiyo, timu ni moja tu ya Tanzania ambayo ni uzalendo kwa watu wote …

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Gulamali nisikilize kwanza, nisikilize kwanza, ulipewa nafasi ya kuchangia wewe kuhusu timu yako na yeye anachangia kuhusu timu yake kwa hiyo wewe ulisema unataka kumpa taarifa sasa sioni kama unataka kutoa taarifa naona unataka kukosoa uchangiaji wake. (Makofi)

Alikuwa amekaa hapa Mheshimiwa Spika wewe ulipata fursa ya kuchangia ukamaliza mchango wako, kuhusu timu yako kwa hiyo muache na yeye amalizie kuhusu timu yake hakuna lugha ambayo si ya kibunge aliyoizungumza.

Mheshimiwa Ndulane malizia mchango wako. (Makofi)

MHE. FRANCIS K. NDULANE: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana, mimi siipokei taarifa yake kwanza, nazungumza kama Mbunge, lakini pili nazungumza kama mmoja kati ya wanafamilia ya mpira katika nchi hii, kwa hiyo na-balance story yangu, nai-balance. (Makofi/Kicheko)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo ningependa…

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Ndulane kuna taarifa nyingine simuoni Mbunge akisimama, ni wapi.

T A A R I F A

MHE. YAHAYA O. MASSARE: Mheshimiwa Naibu spika, nipo hapa.

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Massare.

MHE. YAHAYA O. MASSARE: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante, naomba nimpe taarifa mzungumzaji anayezungumza kwamba siku zote unaposema ukweli unauma sana hasa kwa mtu ambaye anaguswa na jambo lake. (Makofi)

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Ndulane unapokea taarifa hiyo?

MHE. FRANCIS N. NDULANE: Mheshimiwa Naibu Spika, nimeipokea kwa mikono miwili. (Makofi/Kicheko)

Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na mafanikio yote ambayo tumeyapata vilevile kunachangamoto kwenye utambuzi wa mchezo wa mpira wa miguu kama profession na nina fikiri hapa ndipo tunapokwama. Mpira ni profession kama zilivyo profession nyingine kwa hiyo zinatakiwa zitengenezewe msingi imara wa kufundishwa, lakini vifaa vya ufundishaji vipatikane na vilevile mafunzo yawezwe kuendeshwa kama mafunzo ya profession zingine, hapa ndipo tunapo-fail. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo ningeiomba Serikali yangu pamoja na kuwekeza kwenye national team pia iweze kuwekeza kwenye mafunzo kuanzia watoto wadogo kule wanakosoma kwenye shule za msingi na shule za sekondari, twende tukafundishe walimu wengi wa mpira na michezo mingine, lakini vilevile twende tukahakikishe kwamba watoto wanafundishwa angalau kila Halmashauri kuwe na kituo kimoja cha uendelezaji wa soka la vijana ili vipaji vyote viweze kukusanywa na viweze kuendelezwa na hatimaye tuweze kupata wachezaji ambao wanafaa kutusaidia kutuvusha katika mashindano mbalimbali. (Makafi)

Mheshimiwa Naibu Spika, wachezaji ambao tunao hivi sasa wanatokea from nowhere, wanaokotwa okotwa tu halafu mwisho wa siku unasikia tayari wanacheza national timu kwa hiyo hawana zile ethics za uchezaji mpira. Kwa hiyo, naomba Serikali iwekeze kupeleka fedha kwenye halmashauri kwa kusudio maalum kama tulivyofanya kwenye miradi mingine na kwenye mradi huu maalum uwepo wa kuendeleza vipaji vya watoto. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, vilevile ningependa vilevile kuchangia kwenye changamoto. Shirikisho letu la mpira Tanzania limekuwa likiendeshwa kwa shida sana, wakati fulani Shirikisho letu lilikuwa na deni la jumla ya shilingi milioni 10.18 wakati wa utawala wa Tenga, Malinzi na hata sasa wakati wa utawala wa Wallace Karia. Deni limelipwa kwa kiasi cha kutosha kama nusu ya deni sasa hivi TFF inadaiwa kodi jumla ya shilingi bilioni 5.009, ndani ya deni hilo lipo deni la shilingi bilioni 4.55 linalotokana na kodi zilizotokana na michezo mbalimbali ambayo ilifanyika hapa Tanzania ya kimataifa na kitaifa.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa mfano, mwaka 2010 timu yetu ya Taifa ya Tanzania ilipocheza na timu ya Taifa ya Brazil ile mechi aliyeialika timu ya Taifa ya Brazil haikuwa TFF na hata mapato yaliyopatikana pale uwanjani ambayo yalivunja rekodi ya mapato hayakwenda TFF, lakini mwisho wa siku lile deni la VAT lilipelekwa TFF.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini kuna fedha za kuwalipwa makocha zimekuwa zikilipwa na Hazina tangu enzi za akina Marcio Maximo, kuna mkusanyiko wa pay as you earn kulikuwa na jumla ya shilingi bilioni 1.3, lakini TFF imehangaika kulilipa limebaki jumla ya shilingi bilioni 1.049.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa kwa kawaida ya malipo ya mishahara kwa watumishi wa Serikali ambao vilevile wale makocha walikuwa wanapitia kama Marcio Maximo alikuwa analipwa na Hazina, lakini wakawa wanalipa ile net figure halafu deni bado linabaki la kodi na yale makato mengine ya kisheria yalikuwa yanabaki kwa TFF, kwa hiyo total sasa hivi ya deni lililobaki ni jumla ya shilingi bilioni 5.809. Kwa hiyo, ningeiomba Serikali ijitahidi kuifutia TFF deni hili ili waweze kuongeza ubora wa kusimamia mpira wa nchi hii, ili tuweze kusonga mbele. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwenye upande wa habari ningeomba kwanza niishukuru Wizara yetu kwa kufanya kazi nzuri, nikianza na Mkurugenzi wetu wa Habari, kwanza Waziri, Mheshimiwa Waziri na Naibu wake, Mheshimiwa Bashungwa pamoja na Mheshimiwa Gekul. Lakini vilevile kuna Mkurugenzi Mkuu wa Habari Ndugu Gerson Msigwa kwa kweli amekuwa akifanya kazi kubwa ya kutujuza taarifa mbalimbali zinazohusu Serikali. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini vilevile nivipongeze vyombo vya habari vya TBC, ITV, Azam Tv, Redio Abood, Redio Mashujaa kule Lindi na Mtwara, Millard Ayo, pamoja na Clouds FM. (Makofi)

NAIBU SPIKA: Ahsante sana, kengele ya pili imeshagonga Mheshimiwa, ahsante sana.

MHE. FRANCIS K. NDULANE: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana, naunga mkono hoja. (Makofi)