Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo

Hon. Anthony Peter Mavunde

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Dodoma mjini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo

MHE. ANTHONY P. MAVUNDE: Mheshimiwa Spika, ninakushukuru sana kwa nafasi hii; la kwanza ambalo ninataka nianze nalo naiomba Serikali sasa ni wakati muafaka kwa kuanza kutenga bajeti kuzisaidia timu zetu za Taifa. Ukienda duniani kote Serikali inazibeba timu za Taifa, ni Tanzania peke yake kwa sisi hapa Afrika ambapo timu ya Taifa inakwenda kwenye mashindano makubwa pasipokuwa na utaratibu maalum wa kuwasaidia kufika huko, wanakwenda kwa kuunga unga. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, hivyo ninaiomba Serikali ione haja ya kuanza kutenga bajeti kubwa wafanye uwekezaji mkubwa msiishie kuwapa bendera tu wakati wanaondoka lakini msimamie pia na maandalizi yao. Nchi nyingi zinasaidia timu zao, Mheshimiwa Waziri nikuombe katika hili kama kweli tunataka Taifa Star na timu nyingine zifanya vizuri lazima tuwekeze, wakienda hivi wanavyoenda kila siku tutakuwa tunawaita kichwa cha mwendawazimu na vilevile tutakuwa hatuwatendei haki kwa sababu maandalizi yao hayaendani na kile ambacho sisi tunakitarajia. Kwa hiyo, nikuombe Mheshimiwa Waziri katika hili mjitahidi sana kuhakikisha kwamba tunatenga fedha kwa ajili ya timu zetu mbalimbali za Taifa, hii itatusaidia sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, la pili naomba niungane na hoja ya Mheshimiwa Sanga na Wabunge wengine wote waliochangia juu ya miundombinu ya viwanja vyetu. Ninaanza kwa kuwapongeza kwanza Azam kwa uwekezaji mkubwa sana ambao wameufanya, Azam hivi sasa ukiangalia mpira ukioneshwa Azam kwenye HD ni kama unaangalia ligi ya Uingereza kwa namna ambavyo kamera wanazozitumia na uwekezaji mkubwa ambao wameufanya ni uwekezaji mkubwa sana, lakini ukienda katika aina za viwanja vyetu ukiondoa uwanja wa Benjamin Mkapa, Dar es Salaam; ukiondoa uwanja wa Kaitaba, Kagera, hivyo ndivyo viwanja ambavyo mpira unaweza ukachezwa watu wakauona vingine vyote mpira una kuwa unpredictable kwa sababu mchezaji huwa anajua mpira ukidunda hapa unadondokea pale, lakini kwa aina ya viwanja tulivyonavyo huwezi kujua mpira unadondokea wapi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, na muda mwingine unaweza ukawalaumu watu wa viwango vibovu kwa sababu ya aina ya miundombinu ya viwanja tulivyonavyo. Haiwezekani tukawa tunaonesha ligi ambayo viwanja vyake vina vumbi hatueleweki, niiombe Serikali la kwanza kabisa kama Mheshimiwa Sanga alivyochangia tuiombe Wizara mkae na Chama cha Mapinduzi ambao ndio wanamiliki viwanja hivi mzungumze kwa pamoja ili tuone namna nzuri ya ujenzi wa viwanja hivi kupitia nyasi za bandia. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hivi sasa hakuna mtu anaweza kuleta nyasi za bandia hapa nchini isipokuwa Azam, Mo Dewji na watu wengine wenye uwezo mkubwa kwa sababu ya gharama kubwa. Kodi ya nyasi za bandia zinawavunja watu moyo na ukiangalia katika vyanzo vya mapato, mapato ya kodi ya nyasi bandia siyo ni chanzo kikuu sana kwa Serikali, hata leo mkiondoa haina athari hasi katika mapato ya Taifa letu, kwa sababu katika miaka mitano anaweza akaingiza mtu mmoja nyasi bandia, lakini leo mtu akiingiza nyasi bandia hapa nchini Tanzania za shilingi 200,000,000 ikiwa gharama yake hiyo maana yake lazima alipe asilimia 42 ya tozo ikiwemo excise duty na VAT.

Mheshimiwa Spika, excise duty ni asilimia 25 ya manunuzi ya ile bidhaa, lakini na VAT ni asilimia 18, kwa hiyo, mtu akitaka kuingiza leo majani ya nyasi bandia kwa ajili ya uwanja maana yake ni lazima akiwa na shilingi milioni 200 atafute shilingi milioni 84 nyingine kwa ajili ya kodi tu, hakuna mtu anayeweza kufanya hii.

Niiombe Serikali na bahati nzuri Wizara ya Fedha ipo chini ya Mheshimiwa Mwigulu mwana michezo, Naibu Waziri vilevile Masauni ni mwana michezo kaeni mliangalie hili, twendeni tukatoe kodi kwenye nyasi bandia. (Makofi)

MHE. FESTO R. SANGA: Mheshimiwa Spika, Taarifa.

SPIKA: Mheshimiwa Sanga.

T A A R I F A

MHE. FESTO R. SANGA: Mheshimiwa Spika, nilikuwa naomba kumpa taarifa mzungumzaji anachokizungumza ni kitu sahihi na bahati nzuri ni kwamba kwenye sera ya michezo ukurasa namba 43 unasema vifaa vya michezo pamoja na malighafi za kutengenezea michezo zitozwe kodi nafuu, kwa hiyo, ninampa taarifa kwamba hili linawezekana Wizara ya Michezo na Wizara ya Fedha zikiamua.

SPIKA: Taarifa hiyo unaipokea Mheshimiwa Anthony.

MHE. ANTHONY P. MAVUNDE: Mheshimiwa Spika, ninaipokea kwa mikono miwili niiombe sana Serikali iliangalie hili ili tuboreshe viwanja vyetu vya michezo hapa nchini.

Mheshimiwa Spika, la tatu ni sports arena Mheshimiwa Waziri na mimi nilitegemea ningeona kwenye hotuba yako, dunia ya leo ndio imekwenda huko Mheshimiwa Waziri na
bahati nzuri Mheshimiwa Innocent wewe una exposure kubwa sana umekaa Marekani unafahamu hizi vitu, duniani kote ndio tunaelekea huko hivi sasa, leo Kigali arena yenye uwezo wa kuingiza watu 10,000 tu leo ndio mashinano ya ligi ya basketball ya Afrika yanafanyikia pale Rwanda ambayo yameitangaza Rwanda dunia nzima inaijua Rwanda kwa sababu ya arena tu ya watu 10,000 pale Amahoro. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Rwanda wamejenga kwa kutumia kampuni kutoka Uturuki, ni PPP, ni Shirika la Nyumba la Rwanda Wizara na ile kampuni wamejenga arena hiyo leo Rwanda inafahamika dunia nzima kwa sababu ya basketball na NBA wale wanaoandaa mashindano kule Marekani wametia mkono wao, kwa hiyo, hivi sasa zaidi ya viewers milioni 450 wanafuatilia mashindano ya basketball pale Rwanda. Hii ni sehemu yetu pia na sisi kujitangaza kama tunalipa fedha nyingi kwa ajili ya kujitangaza kwenye utalii huu ndio utalii wenyewe. Nikuombe Mheshimiwa Waziri tuone namna sasa ya kwenda huko na sisi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, amesema Mheshimiwa Babu Tale hapa, matamasha yetu mengi yanafanyikia katika viwanda vya wazi na Mheshimiwa Waziri bahati nzuri tulikuwa wote siku zile katika Urithi Festival, mvua ilitunyeshea Uwanja wa Jamhuri tukakimbia wote, tulijibanza wote Mheshimiwa Waziri kwenye vibanda vya maonesho kwa sababu ya mvua, tutoke huko tuingie katika sposts arena na mimi nitafurahi kuona katika bajeti hiiā€¦

MHE. DOROTHY G. KILAVE: Mheshimiwa Spika, Taarifa.

SPIKA: Pokea taarifa Mheshimiwa Anthony.

T A A R I F A

MHE. DOROTHY G. KILAVE: Mheshimiwa Spika, mdogo wangu Mheshimiwa Anthony Mavunde ninasema kwamba lile eneo la kujenga sports arena liko Temeke pale Mwembe Yanga, lipo tayari, karibuni sana.

SPIKA: Mheshimiwa Anthony taarifa hiyo.

MHE. ANTHONY P. MAVUNDE: Mheshimiwa Spika, nimepokea taarifa niiombe Serikali kwa ajili ya utekelezaji. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kupitia hivi vitu ndio tunaitangaza nchi yetu hata kwenye utalii leo nataka niwapongeze sana timu ya Simba Sports Club kwa kuvaa tu visit Tanzania, Afrika wameiona Tanzania. (Makofi)

Kwa hiyo, Serikali mnayo nafasi kubwa sana mkikaa pamoja katika kuhakikisha kwamba hata kwenye utalii tutumie michezo pia na wasanii wetu leo Diamond ana followers milioni 12 kwenye instagram, Diamond ndio msanii pekee Tanzania amefanya Tamasha Ouagadougou, Burkina Faso ya kuzaja watu 100,000 akarudia mara mbili ndani ya masaa 24; huyu akienda pale na nembo ya Tanzania. Tanzania inajulikana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Waziri naomba mliangalie hili, mkae pamoja katika kuhakikisha kwamba pia michezo inakuwa sehemu ya utalii. ouagadougou

Lakini Mheshimiwa Waziri nimeangalia katika hotuba yako ukurasa wa 46 umesema kwa uchache sana kuhusu uwanja wa mpira wa miguu Dodoma pale Nzuguni. Mheshimiwa Waziri ilikuwa ni ahadi ya Mheshimiwa Rais, lakini pia mambo yote ya michoro yamekamilika, ujenzi wa uwanja mkubwa wa mpira wa miguu pale Nzuguni, uwanja huu ukijengwa utakuwa mkubwa kuliko yote Afrika Mashariki na Kati, kwa hivi sasa ni viwanja viwili tu vinauwezo wa kubeba watu 60,000 kwa wakati mmoja ni uwanja wa Moi Kasarani pale Kenya na Uwanja wa Benjamin Mkapa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini uwanja wa Dodoma ukijengwa utakuwa una uwezo wa kuwakalisha watu 80,000 kwa wakati mmoja. Nikuombe Mheshimiwa Waziri sijaona namna yoyote ambapo jambo hili linakwenda kutekeleza isipokuwa tu mmesema mnaratibu katika ukurasa 46 wa hotuba yako. Wananchi wa Dodoma wana hamu sana kusikia hatua ya uwanja huu imefikia wapi, nitakuomba ukija ku-windup utuambie sisi wananchi wa Dodoma tujue uwanja huu wa mpira wa miguu umefikia wapi ili tupunguze adha ya uwanja wa Jamhuri ambao hivi sasa tunavyozungumza hivi sasa kuna maonesho pale ya NACTE na TPSF. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, majukwaa yamekaa mpaka katika pitch ya kuchezea mpira ambayo ni changamoto kubwa sana kwa sisi kwetu ambao tunaosimamia uwanja ule. Kwa hiyo, Mheshimiwa Waziri uwanja huu ukijengwa mwingine utakuwa na manufaa makubwa sana, lakini vilevile itafanya nchi nyingine zije zicheze hapa kufanya mazoezi; Brazil walishakuja kucheza katika uwanja wa Benjamin Mkapa mkiwa mna viwanja vizuri maana yake pia ni sehemu ya kutangaza nchi yetu ya Tanzania na watu wakaja kutumia viwanja hivyo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini pia nataka nichukue fursa hii kuendelea kutoa rai kwa watu wengi zaidi kuwekeza kwenye michezo, uwekezaji wa kwenye michezo ndio utakaotutoa hapa kutupeleka mbele, ni ukweli ambao upo dhahiri kabisa kwamba hatuwezi kuendelea pasipo uwekezaji mkubwa.

Mheshimiwa Spika, nataka nichukue fursa hii niwashukuru wafuatao ambao wameleta chachu kwenye uwekezaji hapa nchini, wa kwanza nataka niwashukuru sana kampuni ya Azam kupitia Said Salim Bakhresa kwa uwekezaji mkubwa sana ambao ameufanya, lakini la pili nataka nimpongeze sana Mohamed Dewji kwa uwekezaji mkubwa ambao ameufanya kupitia Klabu ya Simba. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini pia nataka nimpongeze sana Ghalib Said Mohamed wa GSM kwa uwekezaji mkubwa sana alioufanya katika Klabu ya Yanga, lakini pia nataka niipongeze jiji la Dodoma kwa uwekezaji mkubwa sana walioufanya katika timu ya Jiji la Dodoma ambalo leo ninaiona timu yetu inacheza vizuri sana na kwa kweli katika timu ambazo zinakuwa hivi sasa katika kandanda safi ni Dodoma Jiji na hata mechi yetu ya mwisho kule uwanja wa Taifa wa Dar es Salaam mnaweza mkaona Simba walipata taabu kidogo ingawa walituzidi mbinu tu, lakini timu ipo vizuri ni kwasababu ya uwekezaji mkubwa ambao unafanyika. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini pia nimpongeze sana Mheshimiwa Waziri Mkuu kwa nguvu kubwa aliyoweka pale Namungo, ingawa juzi mlitupa furaha mpaka dakika 78 kuendelea mbele ikawa majanga. (Makofi/Kicheko)[Maneno Haya Siyo Sehemu ya Taarifa Rasmi za Bunge]

Mheshimiwa Spika, lakini pia niwapongeze sana KMC kwa uwekezaji mkubwa sana ambao wameufanya lakini vile vile nimpongeze Mbunge mwenzetu Mheshimiwa Alexander Mnyeti kijana mdogo amefanya jambo kubwa sana pale Gwambina pale Misungwi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nimeyasema haya makusudi kwamba ili michezo iendelee lazima tufanye uwekezaji leo ligi yetu imebadilika, mimi ni mshabiki wa Yanga, lakini nitakuwa sijitendei haki kama sitasema ukweli, uwekezaji wa Mo Dewji umeibadilisha Simba, unaiona Simba leo jinsi ilivyo wanajitahidi wanacheza vizuri, lakini na sisi pia kupitia GSM tunakuja. Tunakuja na lengo letu ni kuleta ushindani mkubwa kwa sababu michezo haiwezi kuendelea bila uwekezaji. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, niyaomba makampuni mengine pia izibebe hizi timu, hizi timu hizi ukiacha tu fedha wanazopata kutoka Azam kuendesha timu ni gharama kweli kweli, mimi kipindi fulani nilikuwa ninaimiliki hapa nilikuwa ninaisimamia Dodoma jiji hapa niliwahi kuweka reheni nyumba yangu kwa ajili ya kulipa mishahara, ni jambo gumu kweli kweli mpaka Mheshimiwa Kunambi amekuja kunisaidia kupita Jiji la Dodoma. Lakini tunaomba wawekezaji waje wengi zaidi ligi iwe ya ushindani, Simba akienda kucheza na Gwambina watu wasiyajue matokeo, uwe mchezo ambao hautabiriki, lakini leo ni gumu sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naunga mkono hoja, nakushukuru sana. (Makofi)