Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Viwanda Na Bishara

Hon. Prof. Patrick Alois Ndakidemi

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Moshi Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

2

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Viwanda Na Bishara

MHE. PROF. PATRICK A. NDAKIDEMI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana, na mimi nianze kumpongeza sana Waziri wa Viwanda na Biashara pamoja na Mwenyekiti wa Kamati ya Viwanda, Biashara na Mazingira kwa kuwasilisha hotuba zao za bajeti na ile ya Kamati ya Kudumu ya Bunge vizuri sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi nitajikita kwenye kuangalia mchango wa Mkoa wa Kilimanjaro kwenye sekta ya viwanda na biashara. Historia inaonesha kwamba Mkoa wa Kilimanjaro kwa muda mrefu umekuwa na historia ya kuwa na viwanda vikubwa ambavyo vimeshachangia sana kwenye kulipatia Taifa letu kipato kikubwa na mkoa wetu pamoja na watu ajira za kutosha. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika Jimbo langu la Moshi Vijijini kiwanda ambacho kinafanya kazi vizuri sana sasa hivi ni kiwanda cha TPC ambacho kinaajiri watu kwa wingi sana na kinachangia kikamilifu kwenye pato la Mkoa wa Kilimanjaro na Taifa kwa ujumla. Kuna viwanda ambavyo vimefungwa havifanyi kazi na viwanda hivi ambavyo vimefungwa vimeshasababisha matatizo makubwa sana kwenye mkoa wetu wa Kilimanjaro kiuchumi na kijamii kwa ujumla wake. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, orodha ya viwanda ambavyo vimefungwa kule Kilimanjaro na vimetuletea matatizo makubwa sana ni kama ifuatavyo; kiwanda cha kwanza ni kiwanda ambacho kiko jimboni kwangu, Kiwanda cha Kukoboa Mpunga kilichoko Kijiji cha Chekereni, Kata ya Mabogini; hiki ni kiwanda cha kukoboa Mpunga. Kiwanda cha pili, ambacho kipo jimboni kwangu ni kiwanda cha viatu cha Uru Kaskazini kinaitwa Kiwanda cha Viatu cha Msuni. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, viwanda vingine ambavyo ni vya Moshi DC vya jirani yangu ni Kibo Match Corporation Limited, kiwanda cha kutengeneza viberiti; kuna Kiliwood Product ambacho hata Mheshimiwa Musukuma amekitaja, kuna Kibo Papers Limited, kuna Kiwanda cha Maguni Moshi, kuna Kiwanda cha Twiga Chemicals ambacho kinazalisha bidhaa za kilimo na vipo vingi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sababu ya viwanda hivi kufa, mimi niseme tu sababu zingine ni za ajabu ajabu na sikubaliani nazo sana. Mojawapo ni kwamba wawekezaji ambao walipewa viwanda hivi hawakuwa na nia thabiti ya kuviendeleza hivi viwanda kwa maana nyingine hawakuweza kwenye kuendeleza hivi viwanda. Sababu ya pili ni kwamba teknolojia zimebadilika na hao wenye hivi viwanda hawakuwekeza kwenye teknolojia mpya na sababu ya tatu, ambayo ninayoomba Serikali iliangalie hili, ni kuruhusu bidhaa za nje. Nitatoa mfano, Kiwanda cha Magunia kilishindwa kuzalisha kwasababu Serikali iliruhusu kuingiza jute bags ambazo zilikuwa na bei rahisi na yule mtu wa magunia akashindwa kuzalisha. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na viwanda hivi kufa, niipongeze Serikali ya Awamu ya Tano na ya Sita kwa juhudi kubwa ya kuanzisha tena upya viwanda kule Kilimanjaro. Kuanzia mwezi Disemba, 2017 mpaka mwezi Machi, 2020 Mkoa wa Kilimanjaro ulikuwa na viwanda 113 vipya ambavyo vilianzishwa kwa juhudi ya Serikali. Katika viwanda hivi, viwanda 80 vilikuwa viwanda vidogo sana, viwanda 26 vilikuwa viwanda vidogo, viwanda vinne vilikuwa vya kati na viwanda vitatu vilikuwa ni viwanda vikubwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kutokana na umuhimu wa viwanda, ninaushauri kwa Serikali kwamba kwanza kabisa tufufue tuwe na programu maalum ya kufufua viwanda ambavyo nitavielezea hapa chini kwasababu vinatija kubwa sana kwa mkoa wetu wa Kilimanjaro. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pili, naiomba Serikali ihamasishe wawekezaji hasa wazawa wa Kilimanjaro najua mko huko mliko, rudini nyumbani mje tuijenge Kilimanjaro yetu, tuweke viwanda ili hadhi ya mkoa wetu iwe kama zamani. Nasema haya kwa sababu Mkoa wa Kilimanjaro kuna miundombinu rafiki sana ya kufanya biashara na kuwekeza viwanda. Viwanda muhimu vyenye tija ambavyo vimeshafungwa ni kama vifuatavyo; cha kwanza, kinaitwa Kiwanda cha Kukoboa Mpunga cha Kilimanjaro ambacho kipo Mabogini. Kiwanda hiki Serikali iliwapa KNCU (Chama cha Wakulima wa Kahawa) nafikiri hapa kulikuwa na kosa kidogo badala ya kuwapa CHAWAMPU (Chama cha Wakulima wa Mpunga) kule Mabogini ili wakiendeshe. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, na kuanzia Septemba, 2014 kiwanda hiki hakijawahi kufanya kazi. Mimi naishauri Serikali nakuomba waziri kwasababu kiwanda kimesharudishwa Serikalini kupitia kwa Msajili wa Hazina naomba ikiwezekana tuwape CHAWAMPU wale watu wa Mabogini ndio wanaolima mpunga tuwawezeshe ili waweze kuendesha kiwanda chao. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kiwanda cha pili, Kiwanda cha Viatu Msuni, hiki pia kipo jimboni kwangu na kinamilikiwa na Kata ya Uru Kaskazini, kilifunguliwa miaka ya 1970 na Baba yetu wa Taifa Mwalimu Nyerere kwa sasa kimekufa. Tunaiomba Serikali, Mheshimiwa Waziri upeleke wataalam wa TRDO pale wakawape utaalam namna ya kufufua hiki kiwanda ili tuunge juhudi za hawa watu wanaokimiliki. Ni kata tu inamiliki hiki kiwanda. Tunaomba sana, tuwaunge mkono wana Kata ya Uru Kaskazini ili kiwanda hiki kifufuliwe.

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha muda wa Mzungumzaji)

MHE. PROF. PATRICK A. NDAKIDEMI: Mheshimiwa Mwenyekiti, kiwanda kingine ni Kiwanda cha Magunia ambacho kipo…

MWENYEKITI: Mheshimiwa Patrick, muda wako umeisha.

MHE. PROF. PATRICK A. NDAKIDEMI: Mheshimiwa Mwenyekiti, basi baada ya kusema hayo nimeshayapeleka kwa maandishi naomba kuunga mkono hoja. (Makofi)