Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Viwanda Na Bishara

Hon. Abdallah Dadi Chikota

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Nanyamba

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Viwanda Na Bishara

MHE. ABDALLAH D. CHIKOTA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi na mimi niungane na wenzangu kwa kukupongeza kuteuliwa tena kuwa mwenyekiti na hatuna mashaka na wewe, tunaomba Mwenyezi Mungu akupe afya njema na hekima ili uendelee ku-chair katika kiti chako hicho. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nichukue nafasi hii pia nimpongeza Mheshimiwa Waziri Profesa Kitila Mkumbo kwa kazi nzuri anayoifanya pamoja na Naibu wake, lakini pia na watendaji wa Wizara wakiongozwa na Katibu Mkuu Dotto James pamoja na Wakurugenzi wa taasisi mbalimbali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi mchango wangu utaanza na kujikita na jinsi tunavyoshughulikia matatizo ya wawekezaji na kipekee nichukue nafasi hii kukushukuru na kukupongeza Mheshimiwa Profesa Kitila Mkumbo jinsi ulivyoshughulikia mgogoro wa kiwanda cha Dangote, hongera sana. Umechukua hatua za haraka, umefika site, ndugu zangu Dangote ni taasisi kubwa, isingefaa kwa kipindi kirefu iendelee kuachwa vilevile mgogoro unaendelea wakati Dangote ni taasisi kubwa, wakati mgogoro ule unaendelea hapa Tanzania, delegation ya Benki ya Dunia ilitoka Washington kwenda kuonana na Dangote kule Nigeria. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwetu huku tuone jinsi ukubwa wa taasisi ya Dangote. Kwa hiyo anapopatwa na tatizo naomba tulikimbilie kama ulivyofanya Mheshimiwa Waziri na uendelee kusikiliza matatizo ya kiwanda kile, kwa sababu kiwanda kile kuna ajira rasmi kwa Watanzania zaidi ya 500. Lakini kuna ajira zisizo rasmi zaidi ya 2,000, lakini kuna fleet ya magari pale zaidi ya 1,000. Sasa fanya lori moja lina wafanyakazi wawili ina maana kuna ajira 2,000 pale zipo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini si hivyo tu, kwamba kwa sisi Wana Mtwara kuna vijana wetu wengi, kuna akina mama, wanapata ajira pale na wanapata mkate wao wa kila siku kutoka katika kiwanda cha Dangote. Mheshimiwa Waziri, pale bado kiwandani kuna changamoto nyingi na naomba utenge muda mkawasikilize. Mimi nitazitaja chache tu, changamoto ya kwanza ni bei ambayo TPDC wanaiuzia Dangote ile gesi asilia. Lakini vilevile kuna changamoto ya meli kwa sababu wana mpango wa kusafirisha saruji sasa kwa kutumia Bandari yetu ya Mtwara, kwa hiyo, tuwasikilize kwa hilo, lakini kuna gharama za bandarini nazo tuziangalie vilevile ni kubwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini Tume ya Madini sasa hivi imekuja na hoja nyingine kwamba wana-categorize Kiwanda cha Dangote kama mining company na kutaka kodi nyingi walipe. Kwa hiyo, nalo Mheshimiwa Waziri ukalifanyie kazi. (Makofi)

Suala la pili, ni kuhusu soko la korosho, Mheshimiwa Waziri naipongeza Serikali kwa jinsi inavyochukulia kwa unyeti suala la korosho, lakini naomba iongeze nguvu zaidi. Itafute masoko mapya ya korosho. Tusiende na India kila mwaka, twende na masoko mapya na yapo mengi Vietnam, Japan na maeneo mengine.

Kwa hiyo, naomba sana kwamba tutumie taasisi yetu ya TMX ili kuhakikisha tunawapata wanunuzi wapya wa korosho, lakini vilevile tuhakikishe sasa kwamba korosho ambazo zinatoka mipakani kwa mfano kule kwetu mpaka wa Msumbuji Jimbo la Cabo Delgado wanaleta korosho zao Tanzania. Lakini mwaka juzi ilitokea sintofahamu tukazuia korosho zile zisiiingie kwamba ni chafu. Korosho za Jimbo la Cabo Delgado zina ubora kama korosho za Mtwara. Kama kahawa yetu inaingia Uganda kwa nini tusiruhusu korosho za Msumbiji ziingie kwetu.

Kwa hiyo, naomba zile korosho za Msumbiji ziingie ili ziongeze uzalishaji wetu kwa sababu Kaskazini mwa Msumbuji yanayoendelea mnayafahamu na wenzetu kule hakuna soko rasmi kama lilivyo sisi la korosho kwetu. Mheshimiwa Waziri ruhusu korosho kutoka Msumbiji ziingie nchini bila ya kuwa na vikwazo vyovyote kwa sababu wafanya biashara wetu wadogo wanafanya biashara hiyo lakini wakulima wa Msumbiji wanaingiza korosho kusiwe na vikwazo ambavyo sivyo vya lazima. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini pili, niungane na wenzangu kuzungumzia Mradi wa Mchuchuma na Liganga. Ni mradi wa muda mrefu, basi sasa hivi utekelezwe na ukitekelezwa mradi huu tunatimiza ile dhana ya Mtwara corridor. (Makofi)

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha muda wa Mzungumzaji)

MWENYEKITI: Ahsante sana Mheshimiwa Chikota.

MHE. ABDALLAH D. CHIKOTA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja. Ahsante sana. (Makofi)