Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Viwanda Na Bishara

Hon. Joseph Zacharius Kamonga

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Ludewa

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Viwanda Na Bishara

MHE. JOSEPH Z. KAMONGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana kwa kunipa nafasi niweze kuchangia bajeti hii muhimu ya Viwanda na Biashara, lakini vilevile nimpongeze sana Mheshimiwa Waziri, bajeti yake imekaa vizuri na inaleta matumaini na pia niipongeze Kamati ambayo inaongozwa na Mheshimiwa Kihenzile kwa sababu walifanya ziara jimboni kwangu kuangalia miradi mikubwa ile ya Mchuchuma na Liganga. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kweli bajeti inaleta matumaini, tunamuomba tu Mheshimwa Waziri aendelee kuisamimia ili iweze kutekelezwa. Na bahati nzuri nimekaa naye jana kwa muda mrefu kidogo akiwa na Naibu wake na wiki iliyopita baada ya kumuomba aweze kutembelea Jimboni Ludewa aliridhia kwamba atakwenda baada ya kuwasilisha bajeti hii ili aweze kuzungumza na wananchi. Mheshimiwa Waziri nakushukuru sana na wananchi wa Ludewa wanakusubiri sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini hali kadhalika siku chache zilizopita Waheshimiwa Madiwani wa Jimbo la Ludewa walikuwepo hapa Bungeni na waliweza kukutana na Mheshimiwa Biteko, nako walileta mawazo yao mbalimbali Mheshimiwa Waziri aliweza kufafanua vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini niwashukuru pia Waheshimiwa Wabunge mbalimbali ambao nao wamekuwa wakiona kwamba miradi hii ya Mchuchuma na Liganga ni muhimu sana na ni kitovu kwa uchumi wa nchi yetu. Wabunge wengi sana wamechangia juu ya miradi hii, kwa hiyo, wanaonesha kwamba wanaona umuhimu wa miradi hii. Kwa hiyo naomba sana Serikali iweze kuwa sikivu iwasikilize Waheshimiwa Wabunge wote waliochangia umuhimu wa miradi hii maana na sauti za Wabunge ni sauti za wananchi moja kwa moja.(Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, wananchi wa Jimbo la Ludewa wanapoona miradi inazinduliwa maeneo mengine wanajisikia wanyonge sana, wanasononeka, wanafadhaika, lakini kwa mpango huu wanakuwa wana imani kwamba miradi hii sasa itakwenda kutekelezwa, hasa hasa suala la fidia kwa wananchi wa Mchuchuma pale vijiji vya Nkomang’ombe, Kipangala, Iwela wanadai fidia na wamesubiria kwa muda mrefu sana. Wananchi wa Kijiji cha Amani na Mundindi wamesubiria fidia hizi tokea mwaka 2015.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, naamini kwa fedha hizi zilizotengwa Mheshimiwa Waziri atakwenda kuwalipa fidia wananchi wale mapema iwezekanavyo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna mzee mmoja alikuwa anaitwa Mzee Machupa, mwaka 2017 aliwahi kuwaeleza wananchi wa NDC kwamba hizi fidia Serikali inashindwa kutulipa wanataka ije ijenge makaburi yetu, tutakufa tutaziacha hizi fedha, bahati mbaya mzee yule Mwenyezi Mungu amemchukua bila kulipwa zile fedha. Kwa hiyo Mheshimiwa Waziri naomba sana utekelezaji wa jambo hili na kukumbusha ile ziara ya Ludewa kwenda kuzungumza na wananchi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, na vilevile tutambue kwamba katika madini haya tunazungumzia tu makaa ya mawe na chuma, kwenye chuma cha Liganga ambacho kinaonekana kwamba kuna mashapo ya chuma ambayo ni tani milioni 126, kwa eneo la kilometa 10 tu ambao walijaribu kufanya uchunguzi. Lakini kwa eneo lote linakadiriwa na tani milioni 700 mpaka milioni 1,400 za chuma ambazo ndani yake kuna madini mengine ya titanium, ya vanadium na madini haya ni muhimu sana kwa sababu mengine yanatumika kutengeneza vitu vya thamani sana, kama laptop, computers na ndege. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo kuna madini mengine ambayo yanathamani kubwa, kwa hiyo, hii ni utajiri mkubwa kwa nchi yetu, ni Serikali haina sababu ya kutoanza miradi hii. (Makofi)

Vilevile miradi hii naomba Serikali izidi kuwasiliana, Wizara za Serikali, kwa sababu uwekezaji huu tunavyosema kwamba ni mradi kielelezo, miundombinu nayo inapaswa iendane na miradi hii. Bahati mbaya sana nilisoma bajeti ya Wizara ya Ujenzi nikaona uwanja wa ndege wa Njombe haumo kwenye mpango, wakati Mheshimiwa Rais wa Jamhuri mama Samia Suluhu Hassan alivyokwenda kwenye...

MHE. NEEMA W. MGAYA: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa.

MWENYEKITI: Taarifa, Mheshimiwa Neema Mgaya.

T A A R I F A

MHE. NEEMA W. MGAYA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi. Nilikuwa napenda kumpa taarifa kaka yangu Joseph Kamonga, Mbunge wa Ludewa, nilikuwa napenda kumwambia kaka yangu Joseph kwamba Serikali pia itueleze imejiandaa vipi kwenye mradi huu wa Liganga na Mchuchuma kuwatayarisha wananchi wetu wa Ludewa kuupokea mradi ule, kuwapa elimu namna gani ambayo wananchi wataweza kwenda kunufaika na fursa mbalimbali zitakazotokana na mradi huu wa Liganga na Mchuchuma. (Makofi)

MWENYEKITI: Mheshimiwa Joseph.

MHE. JOSEPH Z. KAMONGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naipokea taarifa hii kwa sababu ananikumbusha NDC walianzisha mradi wa kuelimisha jamii unaitwa PAKA. Mradi ule haupo tena, nina imani Mheshimiwa Waziri atatoa taarifa na atasema bajeti iliyotengwa kwa ajili ya kuwapa elimu wananchi wa Jimbo la Ludewa na maeneo jirani ili waweze kujiandaa na miradi hii. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo uwanja wa ndege nayo ni sehemu ya uwekezaji, bahati mbaya Wizara ya Ujenzi nimeona wameondoa wakati ilikuwa ni ahadi ya Mheshimiwa Rais, ipo kwenye Ilani ya Uchaguzi na wananchi wa Njombe kiasili ni wafanyabiashara kwa hiyo uwanja ule ni muhimu sana na unaendana na miradi hii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo, nashukuru sana naunga mkono hoja. (Makofi)