Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Kilimo

Hon. Prof. Adolf Faustine Mkenda

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Rombo

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Kilimo

WAZIRI WA KILIMO: Mheshimiwa Spika, kwanza nashukuru sana kwa fursa hii naomba kwanza niweke kumbukumbu sahihi, kwamba ninaomba Bunge lako Tukufu liidhinishe jumla ya shilingi 294,162,071,000 kupitia fungu namba 43, Fungu namba 5 na Fungu namba 24 kama ilivyoainishwa katika hotuba ya bajeti ambayo tuliwasilisha mbele yako. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naomba nitoe shukrani nyingi sana kwa Wabunge wote kwa michango yao mingi sana tumepata wabunge 87 waiochangia katika hotuba hii kati yao tumepata vile vile michango kwa maandishi kwa Wabunge tisa. Napenda kuwahakikishia Waheshimiwa Wabunge kwamba kila lililozungumzwa na tuliloletewa tutalitafakari kwa kina, tutalizingatia na pale inapowezekana tutalitekeleza kwa hiyo ninawashukuru sana kwa michango yenu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naomba nitoe shukrani za pekee kwa Kamati yako ya kudumu ya Kilimo Mifugo na Maji chini ya uongozi mahiri wa Mwenyekiti wetu Mheshimiwa Dkt. Ishengoma na Makamu Mwenyekiti Mheshimiwa Almas Maige na wajumbe wote kwa kweli tumefanya nao kazi kwa pamoja na nitatoa mfano mmoja tu. Hivi mnavyoona dodoso la umwagiliaji wakati tunapeleka taarifa yetu ya umwagiliaji kwenye Kamati ndio baadhi ya Wabunge wakatuambia hapa mbona kinachoelezwa hapa sicho hasa tunachokiona kule. Kwa hiyo, tulishapanga na Mheshimiwa Bashe tutawanyike nchi nzima lakini basi hapa katikati mara nzige, mara misiba nakadhalika. Lakini tutaanza safari baada ya Bunge na ninawaomba Waheshimiwa Wabunge naombeni mjaze haya madodoso tutayafanyia kazi kwa sababu tunahitaji kuwasikiliza.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo tulianza kuyasikia yale kwenye kama Kamati na tutayafanyia kazi. Kwa namna ya pekee napenda kumshukuru sana Mheshimiwa Hussein Bashe Naibu Waziri wa Wizara yetu ndio Mheshimiwa anasema mzigo mzito mpe Mnyamwezi aubebe ninamshukuru Mheshimiwa Rais kunipa Mnyamwezi kama Naibu, tunafanya kazi vizuri kwa ushirikiano ni mbunifu na kadri tunavyojua Mheshimiwa Bashe haja-change tulikuwa tunamsikia hapa Bungeni akiongea. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sasa hivi nafasi aliyopo mengine alikuwa anaongea anayafanyia kazi huku sio kila kitu anaweza akakisema kabla hakijakamilika ninawahakikisha kwamba Mheshimiwa Bashe ni yule yule ana moto ule ule na ubunifu ule ule ninashukuru sana na kumpongeza kwa kufanya nae kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, napenda sana kutoa shukrani kwa Katibu Mkuu Andrew Massawe, Naibu Katibu Mkuu Profesa Tumbo, watumishi wote wa Wizara na Taasisi kwakweli wanafanya kazi kubwa na mimi ninasema tu kama kuna matatizo, matatizo ni kwa Waziri kwa sababu tunachowaambia wanafanya. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ukiona hakijakwenda vizuri labda hatujawaambia kwa hiyo lawama anabeba Waziri wa Kilimo, wana roho nzuri sana mambo yakiharibika labda Waziri ndio atakuwa mwenye roho mbaya.

Mheshimiwa Spika, kilimo na hili ni muhimu sana lipo ASPD Ilani ya Chama, lipo kila document na hili lazima tulikumbuke tatizo la kilimo ni tija ndogo na Mheshimiwa Bashiru amelieleza vizuri sana na Waheshimiwa Wabunge wengi sana hapa, na nitalifafanua kidogo kwa sababu mikakati tuliyoichukua kwa bajeti ile ile haijaongezeka na nitawaeleza tumefanya nini kuhakikisha kwamba tunashughulika na suala la tija ndogo ni muhimu sana na sisi tunajitahidi tusishindwe kwa sababu tunachojaribu kukifanya tukishindwa pengine nguvu ya kujaribu kukifanya itapotea.

Mheshimiwa Spika, ngoja ianze ku-aggregate data ukiangalia pato la Taifa tunaona kwamba Kilimo kinachangia, kilimo kwa ujumla wake maana mifugo na kila kitu kinachangia asilimia 26-point somethings. Kwa sababu kilimo cha mazao tu ni takribani asilimia 18 lakini watu walioajiriwa kwenye Kilimo ni takribani asilimia 58 maana yake ni nini?

(i) Maana yake ni kwamba pato la Taifa ambalo uzalishaji wetu takribani theluthi mbili inazalisha theluthi moja tu maana yake uzalishaji ni mdogo sana kwa mtu mmoja mmoja, tija ni ndogo sana;

(ii) Umaskini ni mkubwa kwenye kilimo;

(iii) mgawanyo wa mapato ni mbaya, maana yake ni kwamba pato la taifa ndio keki tunayokula inapokuwa wakulima ambao ni theluthi mbili ya watu wote wanakula theluthi moja tu ya pato la Taifa anayekula theluthi mbili ni nani? Kwa hiyo huo ni mgawanyo mbaya wa mapato, na yote hayo ni kielelezo kwamba tija ni ndogo na Mheshimiwa Rais alivyohutubia Bunge lako Tukufu hapa alizungumzia cha kwanza tatizo kubwa ni tija na kama hatuchukui hatua za kunyanyua tija hatua nyingine sio sexy lakini lazima zichukuliwe ili tuweze kusonga mbele hiyo ni aggregate data. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, hebu twende kwa zao moja moja kabla ya hatujaangalia pale niwasomee hapa pamba, nadhani kuna Waheshimiwa walizungumza hapa sisi tunapolima kwenye hekari moja pamba tunapata kilo 200, 300, 350 kwa hekari moja West Africa kuna nchi zinapata kilo 1000 kwenye hekari moja. Kwa hiyo, hata tukizungumza masoko hapa tutazungumza masoko sana lakini tija ikiwa ndogo unaenda kushindana kwenye soko la Dunia na mtu ambaye kwenye hekari moja anapata kilo 1,000 halafu sisi tunapata hekari moja kilo 200,250 na ndio maana nitaeleza hatua ambazo tunazozichukua tena kwa undani zaidi.

Mheshimiwa Spika, hatuwezi kusogea ebu tuchukue michikichi na Mheshimiwa Waziri Mkuu atatusaidia sana kwenye hilo sasa hivi tuna matatizo ya mafuta ya kula wanasema michikichi ilitoka Kigoma. Sisi kwenye hekta moja ya michikichi tunapata mafuta ya mawese tani 1.6 lakini huko tunaponunua mafuta ya mawese sasa hivi kwenye hekta moja wanapata mpaka tani 10 za mafuta. Kwa hiyo, tunaweza tukazungumza masoko sana na tutayazungumza kwa hiyo, kipaumbele cha kwanza kitakuwa nini. Kwa hiyo, soko la mafuta lipo hapa nchini. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, siku zote tunatumia mafuta hapa hatujaacha kutumia mafuta shida iko wapi sio kwamba tu kila mara likiwepo soko basi uzalishaji unakwenda soko mafuta halijawahi kuondoka lakini uzalishaji ndio huo. Hatuwezi kushindana tumeongeza import duty kwenye mafuta wanasema bora kuletwe refine oil sasa import duty unaiongeza pale wananunua mafuta refine wanaleta hapo wanauza kwasababu kwenye hekta moja wanapata almost tani kumi ya mafuta hilo tatizo tusipolitatua hatuendi popote. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nachukua kitu kingine hapa juzi nilienda Kongwa, nilienda mchana kidogo nimeangalia mtama, sijui kama picha ipo hapa niliona mtama huwezi kuamini kwa utafiti wetu tu tumegundua mtama aina ya Masiha ambao kwa mkulima sasa hivi kwa hekta moja mtama anapata tani 0.9 akilima vizuri 0.9 kwa mbegu mpya tuliyoipata kwa utafiti wetu sisi hekta moja unapata tani 3 hadi tani 3.8. Kwa hiyo, ukiingia kwenye soko uzalishaji wako tija ni dogo utahangaika kweli kweli kama wenzako tija nzuri na sisi Mpango wa Maendeleo wa Miaka Mitano tumesema ni kujenga uchumi shindani. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, maana yake kuzalisha kwa gharama ndogo ili uweze kuuza, sasa naweza nikatoa mfano mmoja hadi mwigine hadi mwingine hadi mwingine. Lakini hili suala la tija ndio kubwa katika kilimo tusipolitatua tutaendelea kuzungumza kilimo ni uti wa mgongo kilimo ni oxygen tutalizungumza hilo lakini ufumbuzi upo hapa. (Makofi)

Mheshimiwa Spia, sasa tunafanya nini? Kwanza kwenye tija na hiki ni vizuri tukisema tunapokuwa tunataka kujenga uchumi wa Viwanda hapa nchini kwa kweli tunataka malighafi iwe ni bei ndogo maana yake ni kwamba tunataka tuweze kupata mazao kwa bei ndogo. Lakini tunataka mkulima apate fedha nyingi na njia pekee unayoweza kutimiza hilo ni kuwa na tija kubwa huyu mkulima wa Pamba tunataka kuanzisha Textile Industry tungependa aweze kuzalisha kilo 1,000 kwa ekari moja ili hata kama bei imeshuka yule mwenye Textile anunue pamba kwa bei nzuri bado kipato cha mkulima kiongezeke.

Mheshimiwa Spika, na hata mishahara sisi kilimo tunaweza tunaongeza mshahara tunaita mshahara halisi real wage tunaongezaje bei ya chakula ikishuka kwa kipato chako hicho hicho unaweza ukala na kununua vitu vingi zaidi kuliko kabla bei ya chakula haijashuka walio-industrialize wote walihakikisha bei ya chakula ndani ya nchi inashuka, tunafanyaje? Tija kwa njia zote hizo mbili; to pathways to industrialization; the cost of raw material that used in the country should go down, the price of food should go down lakini challenge yetu vile vile tunataka kipato cha Mkulima kiongezeke jibu lake tija. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sasa tunafanya nini? Kipaumbele cha kwanza utafiti na Mheshimiwa Rais alivyotoa hotuba hapa alizungumzia hicho hicho na niwaeleze ni kwa nini nimewaeleza hapa kilimo cha Mtama hapo Kongwa ninawaalika mkaangalie kuna mashamba yapo side by side kilimo ambacho ni tradition na kilimo kinachotumia utafiti agronomy nzuri na mbegu nzuri unaona kwa macho huna haja ya kuambiwa.

Mheshimiwa Spika, mihogo tunapata soko sasa hivi la Mohogo China lakini tuna mbegu pale Kibaha tumeigundua inaweza sasa hivi kwa hekta moja kupata kuanzia tani 22 hadi tani 50 na hauwezi kudanganya ule muhogo ukiushika unauona. Sasa hivi tunapata tani tatu tukienda sana tani nane. Kwa hiyo ninashangaa soko linafunguka soko lipo tunashindwa kulishika kwa sababu ya tija ndogo.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, utafiti ni kipaumbele cha kwanza na kitasaidia hata kwenye soko kwa sababu ni suala la ushindani tu. Hapa kuna nchi moja tulipata matatizo mpakani unasikia minong’ono labda wamenunua mahindi kutoka Latin America bei ndogo kuliko mahindi yaliyoko hapa na gharama yote ya usafiri, inakuwaje, tija ndogo, sasa tumefanyaje hapo? Bajeti ya Wizara ya Kilimo iko pale pale, haijaongezeka lakini sisi ndani ya Wizara kwa panga pangua tumeongeza bajeti ya utafiti kutoka shilingi bilioni 7.35 mpaka shilingi bilioni 11.63 ongezeko la asilimia 63. Ndiyo maana nasema watumishi wetu wana roho nzuri, tumekaa hapo mimi na Naibu Waziri nawaambia tutafuteni hela tumeongeza hela hizo za utafiti. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, vilevile tumegundua kwenye sheria tunaruhusiwa kuanzisha Mfuko wa Utafiti, haujaanzishwa kulikuwa hamna kanuni. Kanuni tunazikamilisha inawezekana fedha hizi tulizozipata tukaziongeza kutokana na Mfuko wa Utafiti. Tutaongea na wadau wa maendeleo tuongeze hela ili vituo vyetu vyote vya utafiti vifanye vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mfano sasa hivi kwenye korosho, kila mahali tunataka kuzalisha korosho safi lakini ukiangalia tija yetu ya korosho bado iko chini. Tunaweza tukazalisha twice as much pale Mtwara peke yake, kwa hiyo, tunaenda extensive lakini intensive we are not doing anything. Nasikia Ivory Coast they are doing the best kuliko sisi hapa kwa sababu ya utafiti. Ukiviangalia vituo vyetu vya utafiti vimechoka, kwa kweli ni sawa na yule yule dada daktari alivyosema it is not sexy kwa sababu utafiti ni pata potea, unaweka hela unajaribu unakosa, unaweka hela unajaribu unapata. Nadhani Prof. Ndakidemi yeye alishagundua mbegu moja, kwa hiyo inachukua muda lakini lazima tufanye. Hicho ni kipaumbele cha kwanza. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, katika utafiti la kwanza utafiti kuhusu mbegu, tumeona wataalam wetu wamegundua mbegu nyingi na nzuri; za mtama, mihogo na michikichi inayooteshwa chini ya uongozi wa Waziri Mkuu.

Wananiambia ile mbegu ikiota sasa hivi kwa hekta moja tunaweza tukapata mafuta takriban tani tano, kwa hii michikichi mipya ambayo tunaotesha hapa. Kwa hiyo, tutakomaa na utafiti tu inawezekana tukaondoka Wizarani hatujamaliza lakini tunaanza nalo, tunakomaa nalo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, la pili kwenye utafiti ni kilimo bora. Kwenye pamba tunaambiwa hata spacing tu inaweza ikaongeza tija zaidi ya asilimia 50 na hiyo ni matokeo ya utafiti. Kwa hiyo, kipaumbele cha kwanza kinabaki utafiti haina maana kwamba masoko siyo kipaumbele kwa sababu haina maana kwamba tutafanya utafiti tukimaliza ndiyo twende kwenye masoko, vyote hivyo tunavibeba. Pia kuna vipaumbele vingine hivi tumeviita vipaumbele vikuu vya mkakati, yako mambo ya kujenga vihenge, sumu kuvu na kila kitu. Hivi ni vipaumbele vikuu vya kimkakati ukiona kimekuwa cha kwanza na kile cha masoko tutakwenda navyo hivyo hivyo.

Mheshimiwa Spika, kipaumbele kikuu cha mkakati cha pili uzalishaji wa mbegu. Bajeti ya Wizara imebaki vilevile, panga pangua tumeongeza fedha kwa ASA kutoka shilingi bilioni 5.42 kwenda shilingi bilioni 10.58. Kama alivyosema Mheshimiwa Naibu Waziri hela za umwagiliaji tutakazozipata kwenye Mfuko wa Umwagiliaji, cha kwanza mashamba yote 13 ya ASA mengi yapo tu ni mapori yanatuletea ugomvi na wananchi tunaenda kuyafufua na tutayafanyia umwagiliaji ili tuweze kuzalisha mbegu throughout the year. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tumeanza kwenye ngano, tumehamasisha kilimo cha ngano, tumeingia makubaliano na importers; ngano kilo moja sasa hivi itakuwa Sh.850, the best price, wanasema wenyewe wanatudai mbegu ziko wapi? Nimetoa kibali tumeagiza mbegu kutoka Zambia, just across the border, hatuna!

Mheshimiwa Spika, Waheshimiwa Wabunge wamezungumzia alizeti hapa, record ime-improve sana sasa hivi haitoshi. Kwa hiyo, hata kwenye mkakati wa mafuta ya kula ambao nitauzungumzia hapa tuta-import mbegu na tutatumia revolving fund kuwapa wakulima kuhakikisha tunazidi kuzalisha.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, tunahitaji mbegu ya kila kitu. Nimesikia Waheshimiwa Wabunge hapa wanazungumza mbegu za mahindi zinakuja kinyemela kutoka Zambia, za viazi zinakuja kinyemela kutoka Kenya na matokeo yake tukiwa tegemezi kwenye mbegu uhakika wa chakula (food security) utakuwa mashakani sana. Kwa hiyo, tumeongeza hilo, mashamba yote ya ASA tutayafufua tutayafanyia umwagiliaji. Tutatumia na sekta binafsi na tutapambana na mazingira mazuri ya kibiashara waongeze uzalishaji.

Mheshimiwa Spika, sasa baada ya utafiti umepata mbegu nzuri, unapata kilimo bora kinamfikiaje mkulima, huduma ya ugani. Bajeti ya Wizara haijabadilika. Bajeti tunayomaliza nayo shughuli za ugani tulitenga shilingi milioni 603 tu. Kwa hiyo, wakati unazungumza idadi ya Maafisa Ugani wachache lakini hata fedha zenyewe ndiyo hizo.

Mheshimiwa Spika, sasa panga pangua, bajeti ceiling ni ileile tumetoka kutoka kwenye shilingi milioni 603 za ugani kwenda mpaka shilingi bilioni 11.5. Wakati tunafanya haya unaambiwa sasa Waziri, Naibu Waziri Maafisa Ugani wako TAMISEMI, kwa nini tukate huku tupeleke TAMISEMI, tunapeleka hela hiyo Maafisa Ugani wawe TAMISEMI wawe popote wanatumikia Serikali moja kwani hatutasogea bila kuboresha ugani. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, wako wakulima wakubwa, viko vyama vya ushirika kama Kahama wameajiri Maafisa Ugani na unaanza kuona matokeo lakini sehemu nyingi mtu hajui afanye nini. Hapa Dodoma tukisema tulime alizeti watu wengine wanavuna mbegu ile ile wanaenda kuotesha, productivity inakuwa ndogo sana, unaotesha lini na kwa utaratibu gani?

Mheshimiwa Spika, tutakachofanya kwenye ugani hicho hasa ndiyo tunasema tunataka tusishindwe na tutajitahidi tusishindwe, tutafanya nchi nzima mambo mengi na tunashirikiana na vyama vya ushirika na makampuni binafsi kama ile NOSC – Njombe Out Growers Services Organization na Kahama Cooperative Society na nchi nzima tutapeleka huduma nyingi. Hata hivyo, pamoja na yote tutakayofanya katika nchi nzima tumechagua mikoa mitatu ambayo tunataka kufanya huduma za ugani kwa namna ambayo pengine hatujaifanya kwa muda mrefu au tangu tupate uhuru. Tumechagua Dodoma, Singida na Simiyu, tumeongozwa na umuhimu wa kuzalisha mazao ya mafuta, alizeti at the heart of it. Tunajua tukifanikiwa tutarudi kwa Waziri wa Fedha ule mwaka unaokuja, unaona matokeo haya, unaona shughuli za ugani zinavyolipa hebu twende tukafanye kote. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, katika hii mikoa mitatu pamoja na baadhi ya Maafisa Ugani wengine tunawapa mobility (pikipiki). Nilishasema hapa tunawasaidia kwa fedha za Serikali wawe na mashamba yao, walime, tuweze kukagua unalimaje wewe, mashamba darasa yote yanafufuliwa na ya mwanakijiji ambaye anaonekana anaweza akawasaidia. Pia tutawapatia mafunzo rejea, wengine wameshafunzwa miaka 20, 25 wanafanya kazi hawajafundishwa upya new technics na new discoveries ambazo tunazo.

Mheshimiwa Spika, tutahakikisha tunawapa spark smartphone ambazo zitasaidia vitu vingi. Moja watakuwa wana-monitor masoko lakini pili sisi tutawa-monitor wanafanya nini. Kila siku kuanzia Jumatatu mpaka Ijumaa lazima ajaze kwamba amefanya nini kwenye mobile kilimo. Umeenda kumtembelea Mheshimiwa Gambo lazima ujaze ulienda saa ngapi, tatizo lake lilikuwa nini, umemshauri nini na simu yake. Kwa hiyo, tunaweza tukakaa ofisini tukapiga tukamuuliza Mheshimiwa Gambo eti alikuja bwana shamba hapa? Kwa hiyo, tunafanya hayo katika mikoa hii mitatu.

Mheshimiwa Spika, vilevile tutawapa soil tool analysis kits kwenye kila halmashauri na kadhalika. Katika suala la alizeti ambalo nitalizungumzia mbegu hazitoshi kwa hiyo tutatoa huduma ya ugani na hii huduma ya ugani kwenye alizeti na pamba kwa Simiyu na alizeti itaongeza masuala kama mtama na mazao mengine yote pamoja na Mheshimiwa Mavunde alivyosema suala la kilimo cha zabibu. Kwa hiyo, mazao yote mabwana shamba watafundishwa upya namna ya kulima. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, baada ya mwaka mmoja tutapima matokeo ya hiki tunachojaribu kwenye mikoa mitatu. Tutafanya kazi na Wakuu wa Mikoa na Wakuu wa Wilaya na tutafuatilia kwa karibu na Waheshimiwa Wabunge tunawa-invite muangalie.

Mheshimiwa Spika, sasa labda nilisemee hapa hapa kwamba katika hiyo mikoa mitatu nguvu kubwa sana itaenda kwenye alizeti na mazao mengine, mbegu tutapata wapi? Sasa hivi tumeshazungumza na taasisi moja ya kimataifa nadhani tumeshapata hela ya kuanzia. Juzi nimefanya mkutano kwa Zoom inaweza ikaongezeka, hela hiyo ikija tunaita mkutano wa wakamua mafuta, tutazungumza nao na ma-bankers kuhakikisha kwamba wakulima kwenye vyama vyao vya ushirika wanapata contract farming tunawapa mbegu ya chotara (hybrid) ambapo kwa sababu hatuna record ya kutosha tutawaletea wakati wa mawazo tuta-recovery halafu tutakuwa revolving fund. Kwa wakulima wakubwa bila kujali Mikoa ya Dodoma, Singida na Simiyu iwe ni Kiteto, Simanjiro, Manyara au Morogoro tutawa- encourage na sisi wapate mbegu waingie kwenye contract farming ili sasa viwanda vya kukamua mafuta ambavyo sasa hivi vinafanya kazi miezi miwili, mitatu, minne vinafungwa kwa uhaba wa mbegu za mafuta viweze kuingia kwenye mikataba na wakulima katika mikoa hii.

Mheshimiwa Spika, kipaumbele kingine sitavitaja vyote tulizungumza ni umwagiliaji. Kwenye umwagiliaji bajeti tumeongeza kutoka shilingi bilioni 17.7 kwenda shilingi bilioni
51.5. Pili tumeanzisha Mfuko wa Umwagiliaji ambao tunaamini tutautumia kwa ajili ya kuimarisha shughuli za umwagiliaji na tutajaribu kuongea na wadau mbalimbali tuhakikishe kwamba tunapata fedha nyingi na kuchukua hatua ambazo Naibu Waziri amezieleza.

Mheshimiwa Spika, nizungumzie kidogo kuhusu masoko. Kwanza nianze na tumbaku na Mheshimiwa Naibu Waziri nakushukuru sana kwa maelezo, tunazungumza na ile kampuni ambayo iliondoka hapa, prospect ni kubwa watakuja kurudi kwenye biashara. Wamewasiliana na Mheshimiwa Bashe na tumekubaliana. Walitaka kutuma consultant tumesema hapana tunamtaka yeye mwenyewe aje tuzungumze kwa sababu tunakosa ushindani. Tumbaku ni zao pekee ambalo nilikuta watu wamekamatwa huko Katavi wanaambiwa eti umelima tumbaku bila kibali wakanyang’anywa hela zao, nimetoa amri warudishiwe hela zao. Halafu unapewa pembejeo na makampuni hayo unalima tumbaku ukitaka kuuza unambiwa wewe hukupewa contract ya kulima tumbaku yako ni makinikia wananunua kwa bei ya kutupa, hilo tutalishughulikia.

Mheshimiwa Spika, kuhusu chai, tunaanzisha mnada wa chai kama ambavyo tumeshaeleza.

Mheshimiwa Spika, sasa twende kwenye mahindi. Tumebarikiwa sasa hivi tuna ziada kubwa ya mahindi. Kwanza niwahakikishie hata kabla ya changamoto ya mpaka na Kenya tuliita mkutano mkubwa wa wafanyabiashara wa nafaka hapa Dodoma kuhimizana twendeni tukatafute masoko kwa sababu haya masoko kazi ya private sector kazi yetu ni ku-facilitate. Tulizungumza tukaunganisha na Mabalozi wote wa nchi jirani za DRC, Zambia, Malawi, Burundi, Rwanda, Kenya, tukazungumza na kuweka mikakati ambayo mingine tumeanza kuifanyia kazi.

Mheshimiwa Spika, kwa upande wa Kenya niseme mahindi yetu yanayoenda Kenya tunapima sisi ni salama. Nadhani hata wakati yamezuiwa bado kwa namna fulani yalikuwa yanaenda. Sasa Mheshimiwa Rais ameenda Kenya tumesikia wote tangazo mahindi yanakwenda. Natoa wito kwa wafanyabiashara sombeni mahindi pelekeni Kenya maana yanapendwa sana kule. Natoa wito tena kwa vyombo vyetu vya usalama barabarani mmetusaidia sana, tukiona mtu anasafirisha mahindi na ufuta siyo bangi watu wetu wamekuwa harassed sana kule mpakani acha yaende yauzwe kwa vyovyote na yauzwe popote, nendeni Serikali itasimama na nyie. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sasa hivi ninavyozungumza rate ya kupeleka mahindi Kenya ni wastani wa tani 2,000 kwa wiki. Kwa hiyo, mahindi yanakwenda na tunafuatilia mpakani. Namshukuru sana Mheshimiwa Rais kwa safari yake ya kwenda Nairobi na mimi nilikuwa kwenye msafara wake na nilipata fursa ya kuongea na Waziri wa Kilimo wa Kenya alikuja mwenyewe mpakani Namanga na alinipigia simu. Kwa hiyo, biashara ipo na ni soko kubwa tulichangamkie. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mahitaji ya Kenya ni tani 600,000 ya mahindi bado tunacho-supply kule ni tone tu. Twendeni tukauze. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Bodi ya Nafaka na Mazao Mchanganyiko imetoka Sudan ya Kusini, wamefanya mazungumzo mazuri sana na wafanyabiashara wa Sudan ya Kusini watakuja hapa kwa ajili ya kukamilisha maelewano ya namna ya kuuza mahindi na mchele na mazao mengine Sudan ya Kusini. Mimi binafsi nimepanga tunaenda na msafara wa wafanyabiashara baadaye Sudan ya Kusini na tutaenda DRC, mchele Zimbabwe na kadhalika. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Zimbabwe wana mahindi ya kutosha wanahitaji mchele. Humu ndani kuna Mbunge mwenzetu ni mfanyabiashara, namsifu sana ametusaidia kufungua soko la Eswatini Swaziland, consignment ya kwanza imeenda. Kwa hiyo, tunataka kufungua masoko South Afrika na maeneo kama hayo. Tumekubaliana Wizarani mtu anapoomba kibali cha kusafirisha mazao akishasema nia yake hata asiporudi tunamtafuta na tumekubaliana utamfuata popote umsaidie kujaza online apate kibali bidhaa zetu ziende. Kwa hiyo, tunaendelea kuchakarika kupeleka mazao sehemu nyingine mbalimbali. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo niwahakikishie mahindi sasa hivi Bodi ya Nafaka na Mazao Mchanganyiko imepata shilingi bilioni 10 tumewaambia waingie sokoni bei ya mahindi ni ndogo wale wanafanya biashara nunueni mchangamshe soko nendeni mkauze. Kwa hiyo, tumekubaliana wataanza kufanya biashara hiyo. Tuna mazungumzo vilevile na World Food Program, tuna mkataba pamoja na hivyo kuna mahitaji mengine ya mahindi ambayo yanaendelea. Pamoja na changamoto hii tunaamini kwamba sasa soko litatulia na hasa wafanyabiashara wakiona fursa ipo na mambo yanakwenda.

Mheshimiwa Spika, kwenye mchele sasa hivi tunauza sana Uganda. Tunataka kwenda Saudi Arabia na nchi nyingine kwa ajili ya kufanya kitu kama hicho. Niishie hapo ili nisiache mambo mengine muhimu.

Mheshimiwa Spika, ni kweli tuna changamoto ya ushirika, ni kweli kumetokea wizi mkubwa na ubadhirifu Mheshimiwa Waziri Mkuu amelisimamia sana. Mali za ushirika ziliibiwa mchana kweupe lakini chini ya uongozi wa Waziri Mkuu na Ikulu wakati huo na sasa hivi mali nyingi imerudi. Kweli tumekuwa na majizi humo lakini siyo wote ni majizi kwenye ushirika.

Mheshimiwa Spika, tulimualika Mwenyekiti wa Chama cha Ushirika cha Kahama, nitamualika hapa siku moja ananunua pamba kwa bei nzuri kuliko mtu mwingine yeyote. Kahama sasa hivi pamba inatoka sehemu nyingine inakimbilia kule, analipa hela na baadaye analipa na nyongeza na wameajiri na Maafisa Ugani. Tusimame na ushirika na Waheshimiwa Wabunge naomba tusaidiane tujenge ushirika ndiyo nguvu ya mnyonge Tanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, matatizo hayo ni pamoja na aliyosema Mheshimiwa Saashisha. Mheshimiwa timu ilishaenda kufanya uchunguzi, ripoti ilikuwa haijafika kwangu ilikuwa kwenye Tume nimeipata na nimepitia tusipuuze anachosema Mheshimiwa Saashisha. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Bashe nimemuomba ajipange aende Kilimanjaro kwenye ziara mojawapo atakwenda kulishughulikia hili. Mambo ambayo nimeyaona siyasemi sasa hivi lakini hatutapuuza alichosema Mheshimiwa Saashisha watu wasije wakadhani kwamba unaropoka, umetusaidia sana kutueleza hilo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kuhusu stakabadhi ghalani, narudia tena Mheshimiwa Bashe amelieleza vizuri sana na nawashukuru sana Waheshimiwa Wabunge wote walioeleza changamoto na faida. Kwa hiyo, tutamuomba Mheshimiwa Waziri Mkuu kwenye hili mamlaka ibaki Wizara ya Kilimo. Pamoja na kwamba kuna maduhuli kwenye mazao tusianzishe stakabadhi ghalani kwa lengo la kukusanya maduhuli ya Serikali hata kama tunahitaji maduhuli hayo. Hii ni kwa sababu tunamuadhibu yule anayepeleka kwenye ghala halafu tunaacha hao wengine. Vilevile kuna geographical factors na wingi wa mazao yanayozalishwa.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, sisi ndiyo tutakaotoa kibali kwamba zao hili liingie stakabadhi ghalani. Napenda kuwahakikishia tutafanya hivyo consultatively, tutakaa chini wote na Waheshimiwa Wabunge na wawakilishi wananchi mtashirikishwa pale ambapo tunaona inaweza ikafanya kazi tutapenda tuje tusishirikiane tufanye kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nimalizie mambo mawili harakaharaka; moja nashukuru Waheshimiwa Wabunge na napenda kuwashukuru Waheshimiwa Wabunge wetu wote wa Siha, Mheshimiwa Naibu Waziri wa Longido, Monduli, Simanjiro na Mwanga wakati tunapambana na nzige tulijifunza mambo mengi tukagundua kwamba kilimo anga ni kama vile hatukukiendeleza. Mheshimiwa Waziri Mkuu ulitoa maelekezo na sasa tumetoa, tulikuwa na shilingi milioni 150 za kilimo anga sasa hivi kwa bajeti ileile narudia bila kuongeza ceiling panga pangua tumeweka bilioni tatu na humo ndani mojawapo tutanunua ndege, hizi ndege za mashirika mengine ni zetu pamoja.

Mheshimiwa Spika, Shiriki la Ndege la Jangwani sisi ni wanachama na naamini ni nchi mbili tu Tanzania na nchi nyingine ndiyo zimelipia ada. Kwa hiyo, mlivyosikia tunapiga kelele ndege irudi ni ndege yetu kama ilivyo ya Kenya, Ethiopia, Sudan na kadhalika lakini tunahitaji moja ya akiba hapa kwa ajili ya kuhakikisha kwamba tunapambana na kwereakwerea na kadhalika.

Mheshimiwa Spika, napenda kuwashukuru Waheshimiwa Wabunge ambao tulishirikiana, Wakuu wa Mikoa na Wakuu wa Wilaya.

Mheshimiwa Spika, mwisho suala la mitaji limezungumzwa sana humu, Benki ya Maendeleo ya Kilimo imesemwa na kadhalika. Tutaomba tuwe na siku ifanyike semina, tutakuomba kwa sababu modules ya ile benki sizo ambazo kila mtu anavyoiamini. Halafu kama kuna mawazo tutaongea lakini ukweli ndiyo hivyo kuna namna inavyofanya kazi na kuna maeneo mengi sana imefanya kazi kubwa sana; nimeenda Minjingu nimekuta wamewekeza vizuri sana kwenye upanuzi wa viwanda. Tumeenda maeneo mengine wamekopesha wakulima wadogowadogo, kwa hiyo tutawale hapa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tumeunda kamati, high level panel na nimemchagua Mheshimiwa Bashe awe chairman nawashukuru sana wakuu wa mabenki wote pamoja na Mkuu wa PAS yupo pale kwenye Speakers Gallery pale, wamekubali watakaa kwenye hiyo kamati watafanya kazi kwa takribani miezi minne. Watapata fursa ya kuongea na kila mtu ili tuweze kupana namna ya ku-fund kilimo kwa namna ambayo sio ya gharama kama hii.

Mheshimiwa Spika, labda la mwisho ambalo nimelisahau nimalize kwenye ushirika tunapitia sheria upya na kabla hatujaja na sheria hapa tutahitaji kuwa-consult Wabunge wote. Tunataka twende kwa makini sana kwa sababu tunataka ushirika ukue, AMCOS zifanye vizuri, hatutaki zife lakini tunataka tujue ni nini vikwazo ambavyo tunavipata sasa hivi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana kwa muda huu, Waheshimiwa Wabunge nawashukuru sana…

SPIKA: Kabla hujamalizia kuna Wabunge walikulaumu kidogo kwamba kwenye hotuba yako hukugusa masuala ya horticulture kabisa na kwenye majibu hapa pia umesahau horticulture ama una neno moja mawili ya kusema. (Makofi)

WAZIRI WA KILIMO: Mheshimiwa Spika, nimeongea strategic intervention bila kutaja zao lolote. Tuliposema utafiti hatukusema kwenye zao gani ni mazao yote. Kwenye hotuba ya bajeti nadhani tunaweza tukaonesha hapa alivyosema Mheshimiwa Dkt. Kimei tulimpelekea kitabu na kumuonesha reference na sio kwa bahati mbaya tulimualika Dkt. Mkindi hapa kama mgeni wetu kwa sababu horticulture ni kati ya mazao ya mkakati na Mheshimiwa Waziri Mkuu ametu-guide. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, labda nitoe na mfano, Arusha tutakuwa na kikao cha investment forum into agriculture European watakuja Arusha. Suala kubwa ambalo tunataka kuongea nao ni kurudisha ile logistical arrangement ambayo inasaidia sana kwenye ku-export horticulture. Kulikuwa na call chain system walikuja hapa kwa namna fulani wakashindwa wameenda Ethiopia wanafanya vizuri sana. Niliongea na Balozi nadhani wa Uholanzi alivyonieleza nikasema nataka tuwaite tena tukae nao tuone kama wanaweza wakarudi ili mkulima wa parachichi Njombe pale aweze kuli-export haraka sana na bila uharibifu. Kwa hiyo, kwa kweli hatuwezi kupuuza horticulture.

Mheshimiwa Spika, naomba kutoa hoja.

WAZIRI WA MAWASILIANO NA TEKNOLOJIA YA HABARI: Mheshimiwa Spika, naafiki.