Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Kilimo

Hon. Issaay Zacharia Paulo

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mbulu Mjini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Kilimo

MHE. ZACHARIA P. ISSAAY: Mheshimiwa Spika, namshukuru sana Mwenyezi Mungu kwa kutujalia baraka zake mbalimbali sisi pamoja na Taifa letu.

Mheshimiwa Spika, nachukua nafasi hii kuipongeza sana Serikali ya Awamu ya Tano na Sita kwa jitihada kubwa iliyofanya katika sekta hii muhimu sana ambayo ndiyo uti wa mgongo kwa Watanzania walio wengi.

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya wananchi wa Jimbo la Mbulu naungana na Watanzania wote kumwombea kwa Mwenyezi Mungu Mheshimiwa Hayati Dkt. John Pombe Magufuli, Rais wa Awamu ya Tano, Ee Mungu umpokee mtumishi wako mwaminifu, mtiifu, mzalendo, mwana mapinduzi mahiri wa Afrika katika ufalme wako wa milele mbinguni, Amina.

Mheshimiwa Spika, nampongeza sana Mheshimiwa Samia Suluhu Hasan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kuapishwa kupokea uongozi wa Taifa letu tuendelee kumwombea kwa Mwenyezi Mungu aweze kumlinda na kumjalia baraka zake katika kutuongoza.

Aidha, nawapongeza sana Mheshimiwa Waziri, Naibu Waziri pamoja na watendaji wetu wote wa Wizara hii kwa ngazi mbalimbali katika jitihada zao kutekeleza, kusimamia na kushauri kwa weledi mkubwa katika nyakati mbalimbali.

Mheshimiwa Spika, sasa naomba kutoa mchango wangu kupitia hotuba ya mapendekezo ya bajeti ya Wizara hii kupitia kwa Mheshimiwa Waziri na Mwenyekiti wa Kamati hii.

Mheshimiwa Spika, Serikali isimamie suala la ubora wa pembejeo, uwepo wa Maafisa Ugani na mashamba darasa kwa kila kijiji hususan mashamba ya taasisi na shule za sekondari za kata katika maeneo yanayofikika kwa urahisi ili kuwasaidia wakulima wengi ambao kwa sasa wanapata mavuno ya gunia tano mpaka kumi kwa ekari moja wakati wangeweza kupata hadi gunia 40 kwa pembejeo bora.

Mheshimiwa Spika, kimsingi hadi sasa wakulima wetu wengi bado hawajafikia kile kiwango cha kilimo cha kisasa chenye tija. Hivyo basi ni muhimu sana Serikali ione utaratibu wa uhamasishaji wa kilimo chenye tija, pamoja na kuangalia uwezekano wa Maonesho ya Nane Nane kwa ngazi ya Wilaya kwa kufanya mapitio ya gharama za kuwezesha ili kuondoa gharama zisizo na tija.

Mheshimiwa Spika, Serikali iajiri Maafisa Ugani walau kwa ngazi ya kata na kuwapatia walau pikipiki na mafuta kupitia Halmashauri ili waweze kupanga ratiba ambayo itakuwa wazi kwa wananchi kwenye vijiji vya kata husika kama ilivyo kwa kada zingine za watumishi.

Mheshimiwa Spika, Serikali iache utaratibu wa kuzuia mauzo ya mazao ya wakulima kwenye masoko ya nje kwa kuwa wakulima nao hulima kwa gharama kubwa. Hivyo basi kama sababu kubwa ya kufanya hivyo ni upungufu wa mazao hayo Serikali inunue kupitia wakala wake na baadaye iuze kwa bei mbili tofauti ya soko la ndani na nje kwa kuwa tunawakatisha tamaa wakulima wetu.

Mheshimiwa Spika, Serikali itazame upya majukumu ya msingi ya kada za kilimo na ushirika kwa ngazi za Halmashauri za Wilaya, Kata na Vijiji kwani kwa sasa kata hizi katika maeneo mengi nchini zinakosa tija katika kutoa huduma kwa wananchi utakuta Afisa Ugani yuko kwenye ngazi fulani lakini hana mpango kazi.

Mheshimiwa Spika, naunga hoja asilimia 100 na naomba kuwasilisha.