Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Kilimo

Hon. Prof. Patrick Alois Ndakidemi

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Moshi Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

2

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Kilimo

MHE. PROF. PATRICK A. NDAKIDEMI: Mheshimiwa Spika, kwanza nimpongeze sana Waziri wa Kilimo na Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Kilimo, Uvuvi na Maji kwa kuwasilisha vizuri hotuba ya bajeti na Ripoti ya Kamati ya Kudumu ya Bunge. Pia niwapongeze sana wataalamu wa Wizara pamoja na wadau wa maendeleo kwa mchango mkubwa sana kwenye sekta ya kilimo.

Mheshimiwa Spika, Mpango wa Tatu wa Maendeleo ya Taifa umeainisha nafasi ya sekta ya kilimo katika uchumi wa Tanzania kwani sekta hiyo inaajiri asilimia 65 ya nguvu kazi ya Watanzania, huchangia asilimia 27.5 kwenye pato la Taifa, asilimia 24.7 fedha za kigeni na asilimia 60 ya malighafi ya viwanda hapa nchini. Kilimo huchangia asilimia 100 ya chakula kinachotumika hapa nchini. Kwa bahati mbaya sana, umuhimu huu wa sekta ya kilimo haujaonekana kabisa kwenye bajeti ya Wizara. Kwa mfano, bajeti ya Wizara ya Kilimo ya mwaka 2021/2022 ni shilingi 294,162,071,000, hii ikiwa ni asilimia 0.08 ya bajeti ya Taifa ambayo ni trilioni 36.260.

Mheshimiwa Spika, Rais wa Awamu ya Sita alipohutubia Bunge alieleza kuwa Serikali yake itatoa kipaumbele kwenye sekta ya kilimo ili kuwakwamua wakulima wetu. Kwenye hili, Serikali haijazingatia ahadi ya Rais wetu. Asilimia 0.08 ya bajeti ya kilimo katika bajeti yote ya Taifa ni kidogo sana na haiendani kabisa na ahadi ya Rais ambaye ni kiongozi wetu mkuu.

Mheshimiwa Spika, kwa kuwa kilimo ndio roho ya uchumi wa nchi yetu, ni vyema Serikali ikaiwezesha kikamilifu Wizara ya Kilimo ili waweze kutatua changamoto za wakulima.

Mheshimiwa Spika, ninaishauri Serikali itekeleze lile Azimio la Malabo lililoazimiwa Equatorial Guinea na wakuu wa nchi za Afrika tarehe 26-27 Juni, 2014 ambapo waliazimia kuwekeza asilimia 10 ya bajeti zao za Taifa kwenye kilimo. Kwa mantiki hiyo, bajeti ya kilimo ingekuwa takribani shilingi trilioni 3.626.

Mheshimiwa Spika, kama Serikali itawekeza kikamilifu kwenye kilimo, naishauri Wizara ya Kilimo iwekeze kwenye mambo makuu muhimu yafuatayo:-

(a) Utafiti wa mazao ya chakula na biashara (uzalishaji wa mbegu bora na mbinu za kuongeza tija); taasisi za utafiti wa kilimo ziwezeshwe.

(b) Utafiti wa udongo kwenye kila eneo linalolimwa ili kujua changamoto za rutuba ya udongo.

(c) Utafiti wa mabadiliko ya tabianchi.

(d) Utafiti wa masoko ya kilimo na kuzingatia intelejensia ya masoko.

(e) Kuboresha ushirika kwa kubadilisha sheria kandamizi za ushirika na kusaidia kwenye eneo la uongozi wa ushirika.

(f) Uboreshaji wa shughuli za ugani.

(g) Uzalishaji wa mbegu bora za mazao ya kimkakati kupitia Wakala wa Mbegu (ASA).

(h) Uwekezaji wa kutosha kwenye kilimo cha umwagiliaji, kwa kuelekeza fedha kwenye maeneo yenye maji ya kutosha.

Mheshimiwa Spika, mchango wangu wa pili ni kuhusu fursa za kilimo cha umwagiliaji katika Jimbo la Moshi Vijijini, Mkoa wa Kilimanjaro.

Mheshimiwa Spika, Mkoa wa Kilimanjaro una fursa kubwa sana za kilimo cha umwagiliaji. Hii ni kutokana na ukweli kwamba Kilimanjaro kuna mito mingi inayoanzia mlimani na kuishia Bahari ya Hindi bila kutumika kikamilifu kwenye kilimo.

Mheshimiwa Spika, ninaishauri Serikali ijenge skimu mpya na kukarabati ile mifereji ya asili ili haya maji yatumike kuzalisha mazao badala ya kuishia baharini.

Katika jimbo langu la Moshi Vijijini, ninaishauri Serikali ifanye yafuatayo:-

Mosi, Serikali iwekeze kikamilifu kwenye kuboresha na kujenga upya mifereji ya asili. Miundombinu hii imechoka, na ni muhimu sana kwenye kilimo cha kahawa, ndizi, mbogamboga na matunda. Mifereji hii ikiboreshwa kikamilifu itasaidia katika block farms za asili za mazao hayo katika jimbo langu la Moshi Vijijini.

Pili, Serikali ijenge skimu mpya za umwagiliaji katika maeneo ya tambarare ambayo hukumbwa na mafuriko makubwa kila mwaka. Maji ya mafuriko yaelekezwe shambani kuzalisha chakula (mpunga na mazao mengine). Mafuriko ya mwaka huu yamesababisha maafa makubwa, na Wizara ya Kilimo ilipeleka misaada ya chakula na ya kibinadamu katika Kijiji cha Mandaka Mnono kilichopo Kata ya Oldmoshi Magharibi.

Mheshimiwa Spika, pia Wizara ijenge skimu mpya Kata ya Oldmoshi Magharibi katika kijiji cha Mandaka mnono ambapo kuna 1250 ha. Pia Wizara ijenge skimu mpya Kata ya Arusha Chini katika Vijiji vya Mikocheni na Chemchem ambako kuna 2000 ha. Wizara pia ijenge skimu mpya Kata ya Mabogini ambapo kuna 1350 ha.

Mheshimiwa Spika, skimu hizi mpya zikijengwa, zitaongeza 4600 ha kwenye kilimo cha umwagiliaji na kuongeza uzalishaji wa chakula na kuchangia kikamilifu katika uchumi wa wananchi na Taifa.

Mheshimiwa Spika, baada ya maelezo yangu hapo juu, naunga mkono hoja.