Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Kilimo

Hon. Amb. Dr. Bashiru Ally Kakurwa

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Nominated

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Kilimo

MHE. BALOZI DKT. BASHIRU A. KAKURWA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana kw akunipa nafasi ya kuongea katika Bunge hili tukufu kwa mara ya kwanza. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nakushukuru pia kwa kunipa upendeleo wa muda wa dakika 10. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa kuwa ni mara ya kwanza kuongea, nianze kwa kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa kutuneemesha na kuivusha nchi yetu katika kipindi cha misukosuko baada ya kupata msiba mkubwa ambao haujawahi kutokea katika historia ya nchi yetu. Na, nina uhakika Mwenyezi Mungu hatatutupa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, yamekuwepo majaribio ya kupitisha maneno na kutuchonganisha na wakati mwingine kudhalilisha watu na kutunga maneno ya uwongo ili nchi itikisike lakini nasema wameshindwa na wamelegea. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, niwapongeze viongozi wetu wapya. Mheshimiwa Rais Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Amiri Jeshi Mkuu na Dkt. Isdory Mpango Mheshimiwa Makamu wa Rais kwa kushika barabara usukani na hatamu za uongozi wa Taifa letu na kutuwekea mazingira ya matumaini huko tunakoelekea. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa kuwa ni Mbunge wa kuteuliwa na Mheshimiwa Rais, na ni upendeleo mkubwa kwa sababu ziko nafasi 10 tu za Kikatiba na hadi sasa tuko nane. Nimshukuru sana kwa kuniamini na nimuahidi kwamba sitamuangusha. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nikupongeze wewe kwa kuongoza Bunge letu kwa weledi na kwa umakini na hasa kwa siku hizi mbili tangu jana na leo wakati Bunge hili linajadili bajeti ya Sekta Muhimu kwa uhai wa Taifa letu, Sekta ya Kilimo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, niwapongeze pia Wanasimba, Timu ya Taifa kwa kutufuta machozi angalau ya kurejesha mabao matatu kati ya manne. Niwape moyo haikuwa riziki. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sasa nianze kuchangia, tangu jana kusema ukweli nimeandika mengi katika notebook yangu na mimi ni Mjumbe wa Kamati ya Kilimo inayoongozwa na mama shupavu Mheshimiwa Dkt. Christina Ishengoma. Naweza nikasema kwamba sina jipya la kuongea, mengi yamezungumzwa. Baadhi yapo kwenye hotuba ya Waziri, mengine yapo kwenye hotuba ya Kamati. Kwa hiyo, nitakachokifanya ni kufanya muhtasari wa yale ambayo nimeyaona yanajitokeza moja kwa moja yanayohitaji kufanyiwa kazi na kamati yetu lakini pia na Bunge lako. Wabunge wamezungumza kwa uhakika, kwa uchungu lakini wametoa mawazo mazuri sana ambayo yanaweza yakatusaidia. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa bahati nzuri au mbaya ninaweza nikasema kilimo chetu kimepata sifa tatu katika mjadala wa tangu jana. Sifa zote tatu ni mbaya, ya nne ndiyo nzuri tu. Sifa ya kwanza ni kwamba kilimo chetu kwa kweli tija yake ni duni. Uduni wa tija hiyo unaathiri uzalishaji wa mazao yote ya kilimo. Hiyo sio sifa nzuri na maoni ya Waheshimiwa Wabunge ni kwamba tubadilishe sifa hii mbaya kwa kuongeza tija na wote tunakubaliana kuhusu sifa hiyo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sifa ya pili ambayo imesemwa nzuri sana na ni mbaya pia ni kwamba mazao mengi ya kilimo yanayozalishwa yanauzwa bila kuongezewa thamani. Sifa ya tatu mbaya, ni kwamba kilimo chetu hakijapata masoko ya uhakika na yenye manufaa kwa wakulima. Sifa moja nzuri iliyojitokeza ni kwamba Tanzania imejaaliwa kuwa na wakulima wenye huruma, wenye hisani na uungwana, wanazalisha kwa shida na kunyonywa lakini wameweza kuzalisha chakula cha kutosheleza nchi yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo kilimo chetu kinatuweka katika hali ya kuwa na usalama wa chakula. Hii sio sifa ndogo, tunapo mahali pa kuanzia. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sasa kama sifa hizi tatu ndizo tunazotaka kuzibadilisha yamesemwa mengi mapendekezo ya kufanya. Wengine wameelekeza mawazo yao katika uongezaji wa bajeti ya kilimo, nakubaliana nao. Wengine wanataka tubadilishe mbinu zetu katika maeneo ya umwagiliaji, masoko n.k.

Mheshimiwa Spika, bila shaka ni ya kwanza hiyo maana mimi ni form one humu. (Kicheko)

SPIKA: Bado dakika mbili.

MHE. BALOZI DKT. BASHIRU A. KAKURWA: Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, ninachotaka kupendekeza ni kwamba Bunge lako la Kumi na Moja, limechangia sana kuleta mabadiliko makubwa katika Sekta ya Madini. Changamoto tuliyonayo kwa Bunge hili la Kumi na Mbili, ambalo nimepata bahati ya kuwa Mbunge, tujipe ajenda Bunge liweze kuwa na mchango wa uhakika wa kubadilisha Sekta ya Kilimo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Bunge la Kumi na Moja, katika historia litatambulika kwa kuleta mabadiliko makubwa sana ya kisera na kisheria kwenye Sekta ya Madini na tumeona matokeo yake. Hili la Kumi na Mbili, chini ya uongozi wako na ndani ya Serikali chini ya mama Samia tujipe jukumu la kubadili Sekta ya Kilimo ili sifa hizi mbaya za tija duni, za ukosefu wa masoko na kutoyaongezea thamani mazao yetu ya kilomo zibadilike ili tufanane na Sekta zingine zinazobadilika haraka kama vile miundombinu, mawasiliano n.k. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, nakuomba ama unaweza ukaelekeza Kamati yetu au kwa busara yako kufikiria namna ya kufanya kujibu maswali matatu yafuatayo. La kwanza, tunajifunza nini kutokana na mafanikio tuliyoyapata katika Sekta ya Kilimo lakini na makosa tuliyofanya katika Sekta ya Kilimo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, yako mabadiliko huku nyuma yamefanywa. Tume ya Ardhi ilifanya kazi kubwa ikatusaidia kuweka msingi wa kusimamia ardhi yetu. Tume ya Umwagiliaji Awamu ya Tatu, hata Tume ya Ushirika Awamu ya Nne na Sera zingine. Tusikimbie kufanya mabadiliko bila kujiridhisha kwa kufanya tathmini, wapi tumefanikiwa na wapi tumefanya makosa? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, suala la pili la kuzingatia, Bunge hili la Kumi na Mbili linaweza kutoa mchango gani mpya katika kuchochea mapinduzi ya kilimo. Suala la tatu, tuweze kujibu hoja kwa nini mabadiliko makubwa yaliyotokea nchini katika sekta za miundombinu, fedha, sayansi na teknolojia, ongezeko la watu, elimu, mawasiliano, havichochei ukuaji wa kilimo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, baada ya kusema hayo, naomba kuunga mkono hoja. Ahsanteni sana. (Makofi)