Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Kilimo

Hon. Zuena Athumani Bushiri

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Kilimo

MHE. ZUENA A. BUSHIRI: Mheshimiwa Spika, kwanza nianze kwa kukushukuru kunipa nafasi hii kuchangia katika Wizara ya Kilimo. Nianze kwa kuwapongeza Waziri wa Wizara ya Kilimo, Naibu Waziri na Watendaji wake wote kwa kazi nzuri sana wanazozifanya. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nitajielekeza katika kilimo cha umwagiliaji, umwagiliaji wa mpunga pamoja na tangawizi. Kilimo cha mpunga ni kilimo cha chakula na biashara, kilimo cha mpunga kinaingizia kipato sana wafanyabiashara, kilimo cha mpunga ni kilimo ambacho kinahitaji maji ya kutosha, lakini kwa tabia ya nchi mvua zimekuwa chache sana hivyo mazao ya kilimo cha mpunga yamekuwa machache sana.

Mheshimiwa Spika, natambua kwamba Serikali imejipanga mipango mizuri sana ya kuweza kuwezesha kuweka miundombinu endelevu katika sekta ya umwagiliaji. Nitoe mfano katika kilimo cha umwagiliaji wa mpunga katika Lower Irrigation Moshi, Lower Irrigation Moshi ilianza na hekta 2300 lakini hadi sasa hivi zinalimwa hekta 1100 hii inatokana na miundombinu chakavu ambayo imejengwa tangu mwaka 1987. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kama kweli Serikali nia yetu ni kuboresha miundombinu hii katika skimu zetu ni vizuri tukaelekeza nguvu ili tuweze kufanyakazi ya kusaidia wakulima wale ambao wametengeneza mabwawa yao ili Serikali iongeze nguvu ya kutengeneza mabwawa ya kutosha ili kilimo cha umwagiliaji kiwe kilimo endelevu.

Mheshimiwa Spika, nije katika suala zima la kilimo cha tangawizi, wote tunatambua kwamba kwa kipindi hiki cha Corona tangawizi imekuwa ni kilimo ambacho kimeleta tija sana nje na ndani ya Tanzania, hakuna familia ambayo inaweza ikalala bila kukosa kipande cha tangawizi. Kule Same Mashariki katika Mkoa wa Kilimanjaro wilaya ambayo inalima sana zao hili la Tangawizi, wakulima wamekuwa wakilima kilimo hiki kwa shida sana kwa sababu ya maji. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kilimo cha tangawizi kinahitaji maji ya kutosha, wamejaribu kujisukuma wao wenyewe na kutengeneza miundombinu ya maji kwa maana ya kutengeneza mabwawa Wapare wanaita ndiva. Ndiva ni mabwawa madogo.

Mheshimiwa Spika, niiombe Serikali ili kusaidia kilimo hiki kiweze kukua iweze kusaidia wakulima wale kuwatengenezea mabwawa ambayo yatavuna maji kipindi cha mvua ili kilimo hiki cha tangawizi kiwe kilimo endelevu na kiweze kuwaingizia mapato wakulima wetu pamoja na Serikali kwa ujumla.

Mheshimiwa Spika, nije katika zao la vitunguu, zao la vitunguu linalimwa mkoani Kilimanjaro ni biashara kubwa sana kwa akina mama kule Kilimanjaro ukienda utakuta akina mama wamebeba makarai wanauza vitunguu, vitunguu vinalimwa Himo, vitunguu vinalimwa Hai, vitunguu vinalimwa Ruvu, vitunguu vinalimwa katika Kijiji cha Gonja, Mahore, Mpirani, Kalung’oyo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, wakulima wanatumia nguvu nyingi sana katika kilimo hiki, lakini nguvu zao zote zinaishia pale ambapo maji yanakuwa hayapatikani ya kutosha. Bado niendelee kuiomba Serikali ili kilimo hiki kiweze kushamiri na kuwapatia mapato wananchi. Naomba iendelee, hoja yangu iendelee ile ile ya kuomba Serikali itengeneze mabwawa, na kilimo hiki kimeleta manufaa sana kule Kilimanjaro kwa sababu vitunguu vingi vinauzwa Kenya, soko la Himo ndipo wafanyabiashara wanaotoka Kenya wanapovuka pale na kununua vitunguu hivi, kwa hiyo, ni zao ambalo linawaingizia mapato. (Makofi)

SPIKA: Ahsante sana, Mheshimiwa Zuena Bushiri.

MHE. ZUENA A. BUSHIRI: Mheshimiwa Spika, naunga mkono hoja. (Makofi)