Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Kilimo

Hon. Kunti Yusuph Majala

Sex

Female

Party

CHADEMA

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Kilimo

MHE. KUNTI Y. MAJALA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipatia nafasi ili niweze kuchangia Wizara hii muhimu ambayo inatusababisha tuendelee kuishi.

Mheshimiwa Spika, Mkutano wa Pili wa Bunge hili, niliuliza swali kwa Mheshimiwa Waziri Mkuu kuhusiana na suala nzima la kilimo cha kutegemea mvua ya Mwenyezi Mungu. Waziri Mkuu majibu aliyoyatoa alisema kama Serikali inatoka sasa kwenye kilimo cha kutegemea mvua ya Mungu na kwenda kujikita kwenye kilimo cha tija, kilimo cha umwagiliaji. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, siku za nyuma sekta ya umwagiliaji ilikuwa Wizara ya Maji lakini kwa kuona ufanisi wake ni mdogo tukashauri sekta ya umwagiliaji itoke kwenye Maji iende Kilimo ili watu wa Kilimo waweze kuisimamia sekta hii na iweze kuleta tija ndani ya Taifa letu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini cha kushangaza na cha kustaajabisha baada ya sekta hii kutoka Wizara ya Maji kuletwa Wizara ya Kilimo mwaka 2020/2021bajeti iliyoisha mwaka jana, Wizara ya Kilimo, Sekta ya Umwagiliaji Fungu Na.5 ilipitishiwa au iliidhinishiwa shilingi bilioni 17, fedha za maendeleo za ndani zilikuwa shilingi bilioni 3 na fedha za nje zilikuwa ni shilingi bilioni 9. Sasa katika hizi fedha za ndani shilingi bilioni 3 Serikali haijatoa fedha hata shilingi moja kwa ajili ya kwenda kwenye umwagiliaji na badala yake fedha za nje wenzetu wakatoa shilingi bilioni 5. Tunasema Serikali tunakwenda kujikita kwenye kilimo chenye tija cha umwagiliaji mnatenga wenyewe bila ya kulazimishwa mnasema hii ndiyo tutakayoiweza hata kuitoa nako ni shughuli, imeshindikana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, najiuliza kama Bunge tuna sababu gani ya kukaa humu ndani na jadili na kupitisha fedha halafu haziendi kwenye kazi ambayo tumekwenda kuipitisha? Leo Fungu Na.5 linaomba fedha za maendeleo shilingi bilioni 5, shilingi bilioni 3 haikupewa shilingi bilioni 5 itapewa? Hivi vitu vinakwaza, vinakatisha tamaa, vinaturudisha nyuma na wakati mwingine tunaona hatuna sababu ya kuendelea kuchangia Wizara hii. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Serikali inakiri kwamba sekta hii ndiyo ambayo imeajiri zaidi ya asilimia 65 ya Watanzania. Hivi inasema imeajiri kwa wakulima mmoja mmoja kuhangaika huko kwa majembe ya mikono, kwa mikopo ya gharama kubwa, ilhali tuna Benki yetu ya Kilimo ambapo lengo na madhumuni ilikuwa ni kwenda kuwasaidia wakulima wetu kuweza kupata fedha na mitaji kwa ajili ya kuhakikisha wanakwenda kulima kilimo chenye tija. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, niombe kwa Serikali kwa kuwa Benki ya Kilimo iko chini ya Benki Kuu ambayo masharti yake yanakwenda kubaki vilevile kama benki nyingine, tuone namna gani tunakwenda kuitoa Benki hii ya Kilimo ili tuweze kuipunguzia masharti wananchi wetu waweze kupata mikopo ya yenye tija na hatimaye waweze kilimo chenye tija.

T A A R I F A

MHE. CONSTANTINE J. KANYASU: Mheshimiwa Spika, taarifa.

SPIKA: Taarifa naipokea.

MHE. CONSTANTINE J. KANYASU: Mheshimiwa Spika, naomba kumpa taarifa mchangiaji kwamba Wizara ya Kilimo wana Mfuko unaitwa Agriculture Trust Input Fund ambapo ni mfuko huu, pamoja kwamba ni mfuko chini ya Wizara uko one hundred percent commercial. Wanamkopesha mkulima anayetegemea mvua, wanamkopesha mkulima ambaye hapati masoko lakini katika kipindi cha miaka minne ambayo wamempangia kurejesha akisharejesha anakuta kuna interest ambayo inazidi asilimia 50 ya hela halizokopa. Kwa hiyo, matokeo yake watu wengi wanaona hakuna tofauti ya hela inayosimamiwa na Wizara ambayo ilipangwa kwa ajili ya kuwasadia wakulima na ile inayotoka kwenye benki za biashara.

Mheshimiwa Spika, nakushuru sana.

SPIKA: Mheshimiwa Kunti unapokea taarifa hiyo?

MHE. KUNTI Y. MAJALA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru na nimshukuru kaka yangu Mheshimiwa Kanyasu, haya yote ndio tunayazungumza suala zima la kumsaidia mkulima, Serikali dhamira na nia yenu ni kuwasaidia wakulima kuweza kuhakikisha wanakwenda kupata fedha ama mikopo yenye riba nafuu na itakayokwenda kutolewa kwa muda mrefu hili waweze kuhakikisha kwamba wanalima mazao yao na wanapata fursa ya kuweza kuyauza kwa tija na hatimaye waweze kurejesha hiyo mikopo.

Mheshimiwa Spika, lakini stakabadhi ghalani Waheshimiwa Wabunge wenzangu hapa wamesema suala zima la stakabadhi ghalani na Mkoa wangu wa Dodoma tuliathirika sana na wakati wizara inatulekea stakabadhi ghalani Mkoa wa Dodoma, Mheshimiwa Bashe alituita pale ukumbi wa Msekwa tulimkatalia tukamwambia stakabadhi ghalani kwa kuwa Serikali hamjajipanga kuleta stakabadhi ghalani kwa kuwa wananchi wetu hawana taarifa hawaelewe ni chochote. Lakini pili hamjaweza kuwasaidia wakulima wa Mkoa wa Dodoma na mpaka mfikie hatua ya kwenda kutuletea stakabadhi ghalani.

Mheshimiwa Spika, kwa kuwa wao wana mabavu, wana vyombo vya dola wana kila kitu wakaamua kutuletea stakabadhi ghalani watu wetu walipigwa walinyanganywa mazao yao lakini pili mbaya zaidi Wilaya ya Chemba, Kata ya Mpendo tunapakana na Bahi shughuli zote na kata ile ndiyo inayolima ufuta kwa wingi Kata ya Mpendo wanapata huduma Wilaya ya Bahi, wakulima wa Mpendo walikuwa mazao yao wakivuna wanapeleka Bahi wanauza.

Mheshimiwa Spika, baada ya stakabadhi ghalani kwa kuwa zoezi hili lilikabidhiwa kwa Wakuu wa Wilaya wananchi na wakulima wa Kata ya Mpendo walikuwa wanalazimishwa awe ana kilo mbili awe ana debe moja awe na gunia atoke Mpendo kilometa 97 mpaka Makao Makuu ya Wilaya ya Chemba pale kwenye ghala aende akaweke bodaboda ukikodi ni shilingi 35,000, kilo ya ufuta ni shilingi 2,000 ana debe moja ni Shilingi 40,000huyu mkulima mnamuinua kwa namna gani? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nikushukuru sana stakabadhi ghalani wabaki nayo wao Bashe aipeleke kule pamoja na Mheshimiwa Mkenda pelekeni kwenye majimbo lakini kwetu kwenye Mkoa wa Dodoma tunawashukuru kwa huduma hiyo lakini hatuhitaji hata kuisikia na nitakuwa wa kwanza kwa ajili ya stakabadhi ghalani sitaki kusikia stakabadhi ghalani sitaki kusikia stakabadhi ghalani ndani ya Mkoa wangu wa Dodoma. (Makofi/Kicheko)