Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Kilimo

Hon. Mwantumu Mzamili Zodo

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Kilimo

MHE. MWANTUMU M. ZODO: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa fursa hii ya kuchangia kwenye Wizara hii nyeti ya Kilimo.

Mheshimiwa Spika, wakati wa bajeti ya Wizara ya Elimu nilitoa mchango kuhusu ajira. Serikali yetu imekuwa na changamoto kubwa ya ajira hata Waziri wa TAMISEMI asubuhi alilithibitisha hilo. Kati ya nafasi za walimu 6,000 zilizotangazwa mpaka sasa watu 89,000 wameomba ajira hizo, kwa hiyo, tunaweza tukapata picha hapo.

Mheshimiwa Spika, mbadala wa hilo ambalo litaenda kutatua changamoto hiyo ya ajira kwa vijana wetu na Watanzania ni kupitia sekta hii ya kilimo. Hata hivyo, mkazo kwenye sekta hii ya kilimo ni mdogo mno na Watanzania wengi tunalima bila tija, tija yetu ni ndogo sana kwenye kilimo.

Mheshimiwa Spika, mfano mzuri tu, mimi natokea Mkoa wa Tanga, miaka miwili, mitatu iliyopita tulihamasishwa sana kulima mihogo na wewe mwenyewe nafikiri utakuwa ni shahidi, tukaambiwa kuna Wachina wanakuja kununua mihogo lakini watajenga viwanda vikubwa. Niko na jirani yangu hapa Mzee Mwijage nafikiri alikuwepo wakati huo Mzee wa Viwanda na yeye atakuwa ni shahidi na watu walihamasika sana walikwenda kuchukua mikopo mikubwa sana kwenye mabenki. Ilikuwa ukifika pale kwa Msisi Wilayani Handeni, kuna mashamba ambayo labda uzunguke kwa bodaboda au upande juu ya mlima ndiyo hilo shamba lote unaweza kuliona.

SPIKA: Mheshimiwa Mwantumu, Kanuni zetu zinaruhusu kumuuliza Mbunge swali. Kwa hiyo, unaweza kumuuliza Mheshimiwa Mwijage vile viwanda ulivyoahidi viko wapi na mimi kwa kweli nitatoa nafasi ajibu. (Makofi/Kicheko)

MHE. MWANTUMU M. ZODO: Mheshimiwa Spika, ahsante sana, nitafanya hivyo.

SPIKA: Endelea Mheshimiwa Mwantumu.

MHE. MWANTUMU M. ZODO: Mheshimiwa Spika, nachotaka kusema baada ya yale maagizo na sisi viongozi kuhamasisha wananchi hakuna kiwanda hata kimoja kimejengwa na hata wanunuzi wenyewe hawapo. Watu wale wamechukua mikopo mikubwa mabenki na mpaka sasa hivi watu wengine wana presha. Kwa hiyo, niiombe Wizara tuwe tuna taarifa za kutosha, tukisema tunapeleka viwanda na kuhamasisha wananchi kweli viwanda vije.

Mheshimiwa Spika, sambamba na hilo sasa hivi tumeibua tena zao lingine la kimkakati, zao la mkonge kwa Mkoa wa Tanga. Namshukuru sana Waziri Mkuu ameshakuja karibu mara tatu na ukisoma mikakati ya Serikali wana mikakati mizuri sana. Kuna Bodi ya Mkonge pale na nafikiri Mkurugenzi wa Bodi ya Mkonge toka jana yuko hapa, anafanya kazi nzuri sana. Waziri Mkuu aliagiza wakati wa ziara yake kwanza yale mashamba matano yagawanywe na wale watu wa Bodi ya Mkonge waanze kugawanya yale mashamba kwa wale wananchi ambao wanaishi kwenye maeneo yale na baadaye ndiyo wajaribu kuangalia watu wengine. Kweli Bodi ya Mkonge inafanya hivyo wameanza kugawa kwa shamba lile la Hale, Mwelia, Magoma, Mgombezi na mashamba mengine. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini sasa watendaji wetu wa Serikali, huku juu mipango ni mizuri sana lakini sisi tuko kule chini tuna deal sana na watu wa kule chini wa ngazi za mashina, matawi, huku chini hakuna taarifa kabisa yaani ukiacha wale wananchi wanaoishi kuzunguka mashamba yale ya mikonge, wale ambao hawaishi kwenye yale mashamba ya mikonge hawana taarifa kabisa. Wanakwambia tunasikia mkonge unalipa, tunasikia sasa hivi mkonge hekta moja ni shilingi 3,600,000, kwa hiyo na wao wenyewe wanasikia. Wakati hapo kuna Afisa Kilimo Mkoa ameajiriwa, kuna Afisa Kilimo Wilaya yuko pale kaajiriwa na anafanya kazi, kuna Maafisa Ugani japokuwa ni wachache lakini wapo, huyu Mkurugenzi peke yake wa Bodi ya Mkonge kama hatasaidiwa na hawa watendaji wengine wa Serikali hataweza kufanya kazi hiyo mwenyewe.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, sasa Wizara iwaelekeze watendaji wao kushuka chini kwenye mikutano ya vijiji, mikutano ya kata na hata kwenye mikutano ya Majimbo; Wabunge wanajitahidi sana mara nyingi kuzungumzia suala hili, lakini watendaji wale wa Serikali hawazunguki kutoa hamasa. Wala huwezi ukajua kama kuna Afisa Ugani pale kwenye ngazi ya kata na hata ukimuuliza mwananchi hamjui kabisa. Wale watu wapo tu hawatoi elimu, kilimo kinaporomoka lakini wameajiriwa wanalipwa mishahara. Kwa hiyo, niiombe Wizara isimamie watu wake ili kuleta tija. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, hapo hapo kwenye kilimo niipongeze Wizara ya Kilimo nimeona kilimo kinaendelea kukua. Kwa mfano, mwaka 2019 kimekuwa kwa 4.4% na 2021 ukuaji wa kilimo ni 4.9%. Pia kwenye ajira kinaendelea kutoa ajira kutoka kwenye 58.1% mwaka 2019 mpaka 65%.

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

SPIKA: Ahsante sana.

MHE. MWANTUMU M. ZODO: Mheshimiwa Spika, ahsante sana, naunga mkono hoja lakini naomba Wizara sasa ihakikishe inafanya kazi kweli kweli kuleta tija kwani kwenye kilimo tija bado ni ndogo sana.

Mheshimiwa Spika, nashukuru. (Makofi)