Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Kilimo

Hon. John Michael Sallu

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Handeni Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Kilimo

MHE. JOHN M. SALLU: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi hii nami nichangie kwenye Wizara hii ya Kilimo. Kwanza niwape hongera sana Waziri, Naibu Waziri, Makatibu na watendaji wote wa Wizara kwa kazi kubwa wanayoifanya kusukuma gurudumu letu la kilimo. Nikija upande wa mbegu, mbegu ni kitu muhimu sana katika kilimo, kwa bahati nzuri uzalishaji wa mbegu wa ndani sasa unaanza kupanda kulinganisha na miaka ya nyuma ambako zaidi ya asilimia 70 ya mbegu ilikuwa inaagizwa kutoka nje, hapo niwape hongera sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, katika hotuba ya Waziri ameainisha kwamba ataipa nguvu kubwa ASA ili iweze kuzalisha mbegu kwa wingi. Lakini hapo hapo naishauri Serikali isiwasahau wazalishaji binafsi kwa kuwawekea mazingira rafiki ili waweze kuzalisha kwa wingi kwani mpaka sasa hivi wazalishaji binafsi wanazalisha asilimia 90 ya mbegu. Kwa hiyo, hatutakiwi tuwaache nyuma. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, watafiti wetu wa mbegu wanafanya juhudi kubwa kutengeneza mbegu zenye tija lakini mara nyingi zinaishia kwenye makabati, hazipati kutangazwa vya kutosha ili wananchi wakazifahamu. Ushauri wangu hapa, turudishe lile zoezi la kugawa mbegu kwa ruzuku. Wananchi wakipewa mbegu kwa ruzuku wakulima wadogo wadogo wataanza kutambua zile mbegu mpya zilizokuja na hivyo ikifikia kununua watakuwa wanazitafuta kwa majina zile mbegu mpya watalaam wetu walizozitengeneza. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ukija kwa upande wa umwagiliaji. Sisi wa Handeni vijijini tuna mto mkubwa unapita pale mto wa Pangani ambao haukauki mwaka mzima. Tuna mabonde mazuri ya umwagiliaji ambayo nilikuwa naomba Serikali iyatolee macho. Bonde la Masatu lililoko Kata ya Segera na Bonde la Jambe lililoko Kwamgwe. Kwa kutumia umwagiliaji, tunaweza kutengeneza mazao ya mbogamboga ambayo yanaweza kusaidia sana kiuchumi pamoja na ku-export nje ya nchi tukapata hela za kigeni. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, vile vile kwenye mazao ya matunda, kwenye matunda, sisi wa Handeni Vijijini tunazalisha sana matunda ya maembe pamoja na michungwa. Lakini kwa bahati mbaya tumevamiwa sana na wadudu waharibifu wa matunda hayo. Nzi weupe, kwa hiyo, naomba Wizara itoe macho itusaidie janga hili ambalo linadhuru sana machungwa na miembe iliyoko kwenye kata takriban 10. Nikizitaja kata ambazo zimeathirika sana ni Kata ya Kwedizinga, Segera, Mgambo, Kabuku, Kabukundani na Kwamgwe. Kwa hiyo, tunaomba sana Serikali itoe macho ili iweze kutusaidia janga hili la wadudu waharibifu.

Mheshimiwa Spika, nashukuru sana kwa muda niliopata. Naunga mkono hoja. Ahsante. (Makofi)