Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Viwanda, Biashara na Uwekezaji kwa mwaka wa Fedha 2016/2017

Hon. Dr. Harrison George Mwakyembe

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kyela

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Viwanda, Biashara na Uwekezaji kwa mwaka wa Fedha 2016/2017

MHE. DKT. HARRISON G. MWAKYEMBE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze kwa kumpongeza Mheshimiwa Waziri na wasaidizi wake kwa hotuba nzuri ya bajeti ya Wizara. Naunga mkono hoja.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na Serikali ya Marekani kuuongezea muda Mpango wa AGOA kwa miaka 10, mpango ambao unazipa fursa nchi za Kiafrika kuuza bidhaa zake kwenye Soko la Marekani bila kutozwa ushuru, Tanzania bado haijatumia fursa hii vizuri. Soko la AGOA katika Jumuiya ya Afrika Mashariki limetawaliwa na nchi ya Kenya ambapo mwaka 2013 nchi hiyo imeuza zaidi ya asilimia 96 ya bidhaa zote toka Afrika Mashariki, ikifuatiwa na Tanzania 3%, Uganda 0.4%, Rwanda 0.2% na Burundi asilimia 0%. Bidhaa zitokazo Kenya kwenda Soko la Marekani kwa asilimia kubwa ni mazao ya kilimo cha maua, chai, kahawa, pamba na mazao yake.
Mheshimiwa Mwenyekiti, mazao makubwa yaliyofanywa na Kenya yamechangiwa na nchi hiyo kuwa na mkakati mahsusi wa Kitaifa wa AGOA unaoainisha maeneo ya vipaumbele. Tanzania ni miongoni mwa nchi ambazo hazina mkakati mahsusi wa Kitaifa wa AGOA, hivyo kushindwa kuitumia fursa hiyo adimu na adhimu kikamilifu. Mwaka 2015 kulikuwa na jitihada za Wizara ya Viwanda, Biashara na Uwekezaji kwa kushirikiana na sekta binafsi kuandaa mkakati ya Kitaifa wa AGOA. Ni muhimu tujue tumefika wapi na hatua hiyo muhimu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, moja ya udhaifu tulionao Tanzania ni ufungashaji mbovu wa bidhaa zetu na usalama kiafya wa mazao tunayotaka kuuza nje, udhaifu ambao umetufanya tuwaachie Wakenya kununua vitunguu, hiliki, tangawizi, viazi, pilipili, mchele mzuri nakadhalika, kutoka mashambani mwetu kwa bei ndogo na wao kumalizia kwa ufungashaji bora na kuzingatia masharti ya afya ya usindikaji, hatua ambazo zinaongeza thamani ya bidhaa na kuwaingizia fedha nyingi za kigeni.
Mheshimiwa Mwenyekiti, mwaka 2015 tarehe 26 Februari, 2015 Tanzania tuliongoza nchi ya Jumuiya ya Afrika Mashariki kwenye kikao muhimu cha kujadili masuala haya ya kibiashara na Serikali ya Marekani jijini Washington DC. Pamoja na mambo mengine, mkutano huo uliwezesha nchi zetu kusaini makubaliano na Serikali ya Marekani ya urahisishaji wa biashara (Cooperation Agreement on Trade Facilitations, Sanitary and Phytosanitary measure and technical Barriers to trade). Makubaliano haya yametufungulia njia Watanzania kurekebisha upungufu wetu, kuomba msaada wa kiufundi pale tutakapokuwa tayari kusonga mbele. Moja ya hatua muhimu za kujiandaa ni kuja na huo mkakati wa Kitaifa wa AGOA niliouelezea awali.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nina imani kubwa na Mheshimiwa Waziri na timu yake ya wachapakazi ambayo imeonyesha utayari wa kuchakarika ili nchi yetu sasa ijenge uchumi wa viwanda. Hivyo nina imani kuwa mkakati huo wa Kitaifa wa AGOA utakuwa tayari na kuanza kufanyiwa kazi. Wilaya ya Kyela inasubiri kwa hamu fursa ya kuuza kwenye Soko la Marekani bidhaa zake kuu mbili; mchele wenye ladha nzuri ya pekee na unaonukia na kokoa “organic” ambayo haitumii mbolea zozote za kemikali na ambayo imepata sifa kubwa Ujerumani na Uholanzi. Tatizo letu kubwa ni afya ya mimea na bidhaa zetu kuendana na viwango vya Kimataifa na ufungashaji wa bidhaa zetu ambao bado una ukakasi. Hatua tuliyofikia na wamarekani ni nzuri, tuitumie bila kuchelewa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mara nyingine tena naunga mkono hoja.