Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Mifugo na Uvuvi

Hon. Mashimba Mashauri Ndaki

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Maswa Magharibi

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Mifugo na Uvuvi

WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Spika, nimshukuru tena Mwenyezi Mungu kwa kuniwezesha kusimama mbele ya Bunge lako Tukufu na kuhitimisha ama kutoa mchango wangu kwa hoja iliyokuwepo jana na leo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nikushukuru wewe binafsi sana, sana, kwa kutuongezea mjadala wetu jana, pamoja na kwamba ulisaidiwa kidogo jioni, lakini pia umeendelea leo, lakini nikushukuru sana wewe pia kwa kuongoza mjadala vizuri. (Makofi)

Nimshukuru pia Mheshimiwa Naibu Spika, Wenyeviti wa Bunge, kwa uwezo na umahiri wao kuliendesha Bunge letu, lakini pia nichukue nafasi hii kumshukuru na kumpongeza kwa dhati Mheshimiwa Kassim Majaliwa, Majaliwa, pamoja na Waheshimiwa Mawaziri ambao wamekuwa wakikaimu nafasi yake wakati hayupo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Waziri Mkuu amekuwa makini sana katika kusimamia shughuli za Serikali, aidha napenda kuwashukuru sana, sana Waheshimiwa Wabunge wote ambao mlipata nafasi kuchangia hotuba yetu, lakini hata wale ambao hamkupata nafasi mmechangia, kwa sababu katika hili ni Wabunge 48 wamechangia kwa kuzungumza na Wabunge watatu, wamechangia kwa kuandika. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, changamoto za Wizara yangu kwa kweli ni nyingi na dalili yake kwamba changamoto ni nyingi ni uchangiaji wa Waheshimiwa Wabunge wamekuwa wengi na wewe imekulazimu angalau kupunguza dakika za Mbunge kila mmoja kuchangia. Sasa inaonesha ni kwa namna gani sekta hizi mbili ya mifugo na uvuvi ni sekta muhimu na za msingi sana kwenye Taifa letu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, na kusema ukweli sekta hizi zinabeba watu wengi, lakini pia wengi wao kipato chao siyo kile cha juu, ni kipato cha chini na cha kati kidogo. Kwa hiyo, ni sekta ambazo kwa kweli zina umuhimu mkubwa na ndiyo maana zinapojadaliwa kweli zinavuta hisia za watu wengi.

Mheshimiwa Spika, nipende kushukuru sana, ushauri wa Kamati yetu ya Kilimo, Mifugo na Maji, ushauri wao ulikuwa mzuri sana na niahidi tu kwamba tutauzingatia wote. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa sababu michango ni mingi sana na mimi nimechanganywa na makaratasi mengi ya wasaidizi wangu hapa yaani wana majibu karibu yote ya Waheshimiwa Wabunge, sasa niseme tu kwamba Waheshimiwa Wabunge hoja zenu, maoni yenu na mapendekezo yenu tutayazingatia katika utekelezaji wa bajeti yetu ya mwaka 2021/2022 na tutatoa majibu kwa njia ya maandishi kwa kila hoja ambayo imezungumzwa na kila Mheshimiwa Mbunge, wale walioandika, pamoja na wale waliopata nafasi ya kuzungumza. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo mimi hapa niseme mambo machache tu ambayo nadhani si muhimu sana kuliko mengine, lakini nadhani kwa sababu ya muda wetu yale nitakayoweza kusema. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kulikuwa na suala la ushirikishwaji hafifu wa wadau wakati wa kutunga sheria, kanuni na taratibu, inawezekana kwa sababu kama kawaida sekta hizi ni pana hasa kwenye upande wa uvuvi, ukisema uvuvi ukanda wote wa bahari, zaidi kilometa 1,400 ni ukanda mrefu na watu ni wengi. Ukija Ziwa Victoria ni kubwa watu ni wengi, nenda Ziwa Tanganyika, nenda Ziwa Nyasa ni watu wengi.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo ushirikishwaji unaweza usionekane sana ingawa watalaam wetu kwakweli wamekuwa wakijitahidi sana wanapofanya utafiti juu ya jambo linalotaka kufanyiwa mabadiliko au linalotaka kufanyiwa marekebisho, wamekuwa wakijitahidi kupita kwenye maeneo ya wadau ili kupata taarifa zao ili kupata maoni yao.

Mheshimiwa Spika, lakini niseme tu kwamba Wizara itajitahidi, tutajitahidi kuhakikisha ya kwamba kila mdau anayehusika kwenye masuala ya uvuvi, kila mdau anayehusika kwenye masuala ya mifugo kama tunataka kutunga sheria ama kubadilisha ama kupitia upya lazima tutawashirikisha. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kuna wakati tulienda Mafia tukakutana na wavuvi walisema hiyo changamoto na kwa sababu changamoto kule ilikuwa ni kubwa zaidi, tuliamuru watafiti na watalaam wetu warudi tena kule na walirudi wakaenda kushirikisha wadau wetu mbalimbali ili kusudi tu tuweze kupata majibu ya changamoto ambazo zinawakabili wavuvi wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, niende kwenye suala la wavuvi kuhitaji elimu kutoka Wizarani badala ya kuwachomea zana zao za uvuvi. Hili suala ni la msingi sana na tumeliona baada ya kufanya mikutano na wavuvi, tulifanya mkutano mkubwa na wadau wa uvuvi Dar es Salaam, tukafanya mkutano mkubwa na wadau wa uvuvi Mwanza, tumeliona na hawa wadau wengi wanakuwa hawana habari na mambo mengi yanayotokea ndani ya Wizara. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, na hivyo tumeamua ndani ya Wizara kuanzia Katibu Mkuu wangu anayehusika na Uvuvi na watendaji wake, Wakurugenzi pamoja na Wakuu wa Idara, Wakurugenzi wa Taasisi zilizo chini ya Uvuvi wote tumeamua sasa twende kwa hawa wadau, kujaribu kuzungumza nao na kuwaelimisha juu ya sheria tulizozipitisha na kanuni tunazozitunga na kuzipitisha ili wazifahamu. Kwa sababu wadau wengi wanakuwa hawazifahamu, kwa hiyo, tumekubaliana kwamba tutatoa elimu juu ya sheria, kanuni na taratibu zilizoko, lakini pia tutatoa elimu juu ya tozo mbalimbali ambazo zinapitishwa na Bunge lako Tukufu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini pia tutatoa elimu juu ya tafiti mbalimbali tunazozifanya sisi ngazi ya Wizara ili kuhakikisha tu kwamba tuko kwenye ukurasa mmoja na wadau wetu badala ya kwenda tu na kuwachomea nyavu zao, badala ya kwenda tu na kuwalaumu, badala ya kwenda tu na kupora labda mitumbwi yao, hapana; lazima tuwape elimu halafu ndio tuweze kuanza kushughulika nao. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tutashirikiana pia na wadau wengine wanaoshiriki kwenye mazao ya uvuvi kama TASAC ili ya kwamba tuone ni kwa namna gani elimu inaweza ikafika mapema.
Lakini kulikuwa na suala la wavuvi wa Ziwa Tanganyika waruhusiwe kutumia taa za solar zenye watts 200 badala ya watts 50 kwa chombo. Serikali tuliruhusu matumizi ya taa kumi zenye watts tano kwa kila moja kwenye uvuvi wa dagaa katika Ziwa Tanganyika na hii inatokana na utafiti uliofanyika pia hatufanyi vitu hivi bila kuwa na utafiti bila kuwa na taarifa kamili zinazohusiana na utaalam wa jambo fulani. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, utafiti unaonesha kwamba mwanga wa taa hizo kumi kwa watts tano unafika kina cha mita 150. Sasa ukisikiliza maoni ya Waheshimiwa Wabunge hapa, wanasema ni chini ya hapo, lakini utafiti wetu unaonesha hivyo. Ongezeko la mwanga halina tija sana kutokana na sababu kuwa zaidi ya kina cha mita 150 hakuna samaki kwa kuwa hakuna hewa ya oxygen kule chini. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sasa mimi sijaelewa vizuri labda kwa sababu tutahitaji kuzungumza na kukutana na wadau, tutaelewa vizuri wanachokimaanisha labda kina maana gani. Kwa hiyo, tutaendelea kuwatembelea wavuvi wetu walioko Ziwa Tanganyika, tuelimishane nao juu ya habari hii ya taa na ingawa pia wengine wana maoni kwamba taa za solar pia zisitumike, yaani kuna wakati maoni mbalimbali yanakuja na yanafika mahali yanatuletea shida kidogo.

Mheshimiwa Spika, suala la lingine lilikuwa linahusu kuruhusu uvuvi wa kambamiti uanze Disemba hadi Mei; Mheshimiwa Mpembenwe nadhani alizungumza suala hili.

Mheshimiwa Spika, uvuvi wa kambamiti kwa mujibu wa sheria na kanuni zilizopo unaruhusiwa kufanyika kuanzia mwezi Machi hadi Septemba kila mwaka kwa Kanda ya Kaskazini inayohusisha Wilaya za Bagamoyo, Pangani, Chalinze na kuanzia mwezi Aprili hadi Agosti kila mwaka kwa Kanda ya Kusini inayohusisha Wilaya za Mkuranga, Kibiti pamoja na Kilwa. Aidha, kipindi kilichobaki kimeachwa ili kambamiti waweze kuzaliana na kukua.

Mheshimiwa Spika, maamuzi haya yamefanyika baada pia ya taarifa za utafiti wa kisayansi na kuzingatia uendelevu wa rasilimali za kambamiti. Hayo ndiyo tuliyoyazingatia katika kuangalia ni kipindi kipi ukanda ule wa Kaskazini wavue na ni kipindi kipi ukanda huu wa Kusini wavue. Kwa hiyo, hayo ndio tuliyoyazingatia, lakini ni baada ya kufanya utafiti.

Mheshimiwa Spika, tutaendelea kufanya utafiti na kuona kama maoni ya Waheshimiwa Wabunge ndio valid kwa sasa ili tuweze kuamua pia. Sisi hatuko stagnant sana, hatuko rigid sana kiasi kwamba tunashirikiana, tunasikiliza kile kilio cha wavuvi wetu, cha wadau wetu kuhakikisha kwamba tu tunakwenda pamoja. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, niende kwenye mifugo; muda wetu ni mchache, lakini nizungumzie kuhusiana na uhaba wa miundombinu ikiwemo majosho, mabwawa, visima na minara. Niseme tu kwamba kwa kweli uhitaji ni mkubwa na kwa namna ambavyo Waheshimiwa Wabunge mmechangia, mmeona pia namna fungu letu lilivyo. Sasa kwa sababu uhitaji ni mkubwa kwa mwaka huu wa fedha hatutaweza kukamilisha kila jambo walilohitaji Waheshimiwa Wabunge tulifanye kuhusiana na miundombinu ya mifugo. Tutafanya kwa sehemu lakini sehemu zingine tutafanya kwa miaka inayokuja.

Mheshimiwa Spika, kwa mfano, tumeweza kujenga majosho 12 tu, mengine 59 yanaendelea kujengwa, tuna majosho 199 yamekarabatiwa na majosho 111 yanaendelea kukarabatiwa. Kwenye mpango wetu wa mwaka huu tumesema tutajenga majosho 129; kwa hiyo, tutaangalia tutaanza na mahali ambapo majosho hayapo kabisa. Tutawapa kipaumbele mahali ambapo ng’ombe wako wengi, lakini pia majosho hakuna. Kwa hiyo, tutaangalia hilo lakini miaka inayofuata tutaendelea kwenda kwenye maeneo mengine pia. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sasa kuhusiana na mabwawa; mabwawa pia tunayo kidogo kwa mwaka huu wa fedha ambao ninaomba sana Waheshimiwa Wabunge mtupitishie tuna mabwawa matano. Sasa tutayagawaje kwa Wabunge na majimbo 260 na kitu, hiyo pia ni changamoto yetu nyingine. Lakini nawaombeni tu kwamba tukubaliane maeneo ambayo yatapata mabwawa basi ukipata moja, ninaomba tu tushirikiane, siku nyingine tutapata nyongeza kwa kadri ambavyo tutakuwa tumepata fedha.

Ndugu yangu Mheshimiwa Nicodemus Maganga alisema tutachukua shilingi asipopata, lakini nimhakikishie tu kwamba mpango wetu ni kila mmoja aweze kupata kulingana na fedha tulizonazo. Lakini niombe tu kwamba ikiwa hautafanikiwa kupata kwa mwaka huu, kuna mwaka utafanikiwa kupata. Kabla ya 2025 unayoihofia, tutakuwa tumekupa malambo au mabwawa ambayo tutatuliza wapiga kura wako. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nizungumzie kuhusiana na upatikanaji wa malisho, jambo hili pia limechangiwa na Wabunge wengi. Sasa Wizara tunaendelea kuboresha malisho. Mheshimiwa Naibu Waziri wangu amelizungumza kidogo, lakini mpango wetu ni kwamba tunataka mashamba ya Serikali na mashamba ya Taasisi za Serikali, tuyape mbegu kama ambavyo Naibu Waziri amezungumza tuwape mbegu waweze kupanda. Taasisi zetu za utafiti pia tutazipa mbegu waweze kupanda na wakishapanda tutajitahidi kwa kadri iwezekanavyo kuwaleta wafugaji wetu waweze kujifunza kwenye maeneo haya ambayo tumesema tutapanda. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tumesema tutaenda Halmashauri 20 ili ziwe na mashamba darasa ya malisho, sasa Halmashauri hizi 20 bado ni pungufu, haziwezi kuenea kwenye maeneo ambayo wafugaji wetu wametawanyika. Lakini ninaomba sana, sana maeneo ambayo tutafika na malisho na mbegu hizi za malisho, basi wafugaji walioko kwenye maeneo hayo wajifunze namna ya kustawisha malisho ili tuweze kuwa na malisho ya kutosha. Lakini pia tunataka tuhamasishe wadau wetu Serikali za Mitaa na wao maeneo wanayotenga wajaribu pia kupanda mbegu ambazo sisi tutakuwa nazo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, niseme tu kwamba kuna Halmashauri ambazo zimetenga maeneo ya wafugaji vizuri, lakini kuna Halmashauri zimetenga maeneo ya wafugaji na maeneo ya wakulima, lakini kwa upendeleo sana ambao sio mzuri na upendeleo huu umeleta mgongano kwenye baadhi ya Halmashauri. Utakuta eneo la Halmashauri zima, limepewa wafugaji asilimia 70, wakulima asilimia 30 wakati idadi ya wafugaji na wakulima iko sawa, sasa utakuta lazima maeneo kama haya kutakuwa tu na ugomvi.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, ninawasihi sana Halmashauri zetu kwamba tunapopanga maeneo ya malisho tuzingatie pia uwiano wa watu walioko kwenye Wilaya yetu, tuzingatie pia uwiano wa shughuli za kimaendeleo zinazofanyika kwenye Halmashauri zetu hizo, vinginevyo tutaendeleza ule ugomvi. Lakini nafurahi kusema kwamba kuna Wilaya ambazo zimeamua zitaanza kutenga maeneo na kufanya kama ranchi.

Mheshimiwa Spika, nawaunga mkono Halmashauri za namna hiyo na ninawaombeni Halmashauri za namna hii badala ya kuomba fedha za miradi ya kimkakati za kujenga stendi, za kujenga sijui vitu gani basi pelekeni kwenye ranchi hizi mlizotenga. Hizi ranchi zinaweza zikawapa fedha nyingi kuliko mnavyoweza kutarajia. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa kifupi tu niseme sisi ranchi tunakodisha kwa hekari moja shilingi 3,500; sasa ukikodisha wafugaji wengi kwenye ranchi mtakazokuwa mmetenga, wafugaji wengi ukawa na hekari za kutosha ni chanzo kimojawapo cha mapato ya Halmashauri zenu. Badala ya kung’ang’ania na miradi ya stand, miradi ya masoko sijui na miradi ya namna gani, utakuwa umetatua tatizo la kipato cha Halmashauri yako, lakini utakuwa umeondoa mgogoro kati ya wakulima na wafugaji au wafugaji pamoja na wawekezaji wengine wanaotaka kutumia ardhi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, katika suala la kuongeza upatikanaji wa huduma za ugani na vitendea kazi, hili suala pia limezungumzwa sana na Waheshimiwa Wabunge, ni kweli tutaendelea kushirikiana na Ofisi ya Rais TAMISEMI ambao ndio wanahusika hasa kwenye ajira za Maafisa Ugani wetu hasa wale wote wa uvuvi pamoja na wale wa mifugo. Lakini tutaimarisha mifumo yetu ya huduma za ugani kiganjani ikiwemo m-kilimo ambao ni mfumo unaosaidia kufikisha elimu ya ufugaji bora wa samaki, ufugaji bora wa mifugo kwa wadau wetu mbalimbali. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, tutaendelea kufanya hivyo. Lakini tumesema kwenye taarifa yetu tutawezesha safari hii kununua pikipiki 300, ambazo tutazigawa kwenye maeneo ambayo tunaona ni critical kwenye baadhi ya halmashauri. Mahali ambapo wafugaji au shughuli za ufugaji ziko nyingi, tutagawa pikipiki ili kuweza kuwasaidia hawa watu wetu pia waweze kusafiri na kukutana na wadau wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, labda niende sasa nizungumze kidogo kuhusiana na suala la NARCO, wewe umetoa mchango wako juu ya jambo hili.

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

SPIKA: Bahati mbaya muda umeisha, lakini basi nakupa bonus dakika tano umalizie.

WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Spika, basi nakushukuru sana ahsante sana, nikushukuru sana. Mengine sasa tutatoa majibu kama nilivyosema kwa maandishi, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi.

Mheshimiwa Spika, naomba sasa kutoa hoja. (Makofi)

WAZIRI WA MAMBO YA NDANO YA NCHI: Mheshimiwa Spika, naafiki.