Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Mifugo na Uvuvi

Hon. Prof. Patrick Alois Ndakidemi

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Moshi Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

2

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Mifugo na Uvuvi

MHE. PROF. PATRICK A. NDAKIDEMI: Mheshimiwa Spika, kwanza nimpongeze sana Waziri wa Mifugo na Uvuvi na wataalamu wa Wizara na wadau wa sekta hizi kwa kazi nzuri wanayofanya.

Mheshimiwa Spika, sekta ya mifugo na uvuvi inatoa mchango kidogo sana katika uchumi wa Tanzania pamoja na ukweli usiofichika kwamba tuna idadi kubwa sana ya mifugo na tunalo eneo la Bahari Kuu ya Hindi, Maziwa Makuu Matatu na Mito mingi iliyosambaa nchi nzima ambayo ina utajiri mkubwa wa samaki.

Mheshimiwa Spika, Mkoa wa Kilimanjaro una uhaba mkubwa wa ardhi. Pamoja na hilo, Kilimanjaro kuna fursa nyingi za kufuga aina fulani ya wanyama na samaki kwa kutumia rasilimali zilizopo.

Mheshimiwa Spika, kutokana na uhaba wa malisho, maeneo ya mlimani (Kilimanjaro) yanaweza kutumika vizuri sana kwa ufugaji wa ndani (zero grazing) wa mfugo ya kimkakati kama vile ng’ombe na mbuzi wa maziwa, nguruwe, sungura, kuku na bata. Hali ya hewa ya mkoa inaruhusu ufugaji wa ng’ombe wa maziwa wenye tija kubwa kama ilivyo kwenye nchi za Ulaya. Vilevile eneo la Ukanda wa Chini (Kata za Arusha Chini na Mabogini) lenye wafugaji wa nje, lina uwezekano wa kuzalisha kwa tija ng’ombe, mbuzi na kondoo wa nyama.

Mheshimiwa Spika, pamoja na juhudi za wafugaji wa Jimbo la Moshi Vijijini, aina za kienyeji za wanyama (ng’ombe, mbuzi, nguruwe, kuku) wanaofugwa ni kikwazo kikubwa kwenye maendeleo ya sekta ya mifugo.

Mheshimiwa Spika, kwa upande wa uvuvi, kwa kuwa Mkoani Kilimanjaro kuna maji mengi ya kutosha, kuna uwezekano mkubwa sana wa kuwapatia wananchi kipato kizuri kupitia sekta ya uvuvi kwa kuboresha aina ya samaki waliopo kwenye Bwawa la Nyumba ya Mungu, na kuanzisha ufugaji mpya wa samaki kwa kuchimba mabwawa na kufuga samaki wa aina mbalimbali.

Mheshimiwa Spika, hili litawezekana ikiwa wananchi wa Jimbo la Moshi Vijijini watapatiwa mafunzo ya kitaalamu ya jinsi ya kufuga na kukuza samaki kwa kutumia teknolojia ya maji kidogo yanayozunguka. Ufugaji wa samaki hauna gharama kubwa ikiwa mfugaji atachimba bwawa.

Mheshimiwa Spika, ufugaji endelevu wa samaki unaweza kutatua changamoto za umaskini kwa kuwaongezea kipato na kuchangia kikamilifu kwenye pato la Taifa.

Mheshimiwa Spika, katika Kata ya Arusha Chini kwenye Bwawa la Nyumba ya Mungu, wavuvi wanaweza kusaidiwa na Maafisa Ugani wa uvuvi mbinu bora za ufugaji wa samaki, ikiwepo matumizi ya vizimba.

Mheshimiwa Spika, uwekezaji wa vizimba ulioko Ziwa Victoria na kwenye mabwawa machache Tanzania unaweza kufanyiwa majaribio kwenye Bwawa la Nyumba ya Mungu.

Mheshimiwa Spika, ili kufanikisha ufugaji wa samaki na mifugo ya kimkakati katika Jimbo la Moshi Vijijini, ninaishauri Wizara itusaidie yafuatayo; kwanza, Wizara kwa kushirikiana na wadau wa mifugo na uvuvi wafanye utafiti na kuangalia changamoto na fursa zilizopo katika Jimbo la Moshi Vijijini, ili wajue pa kusaidia.

Pili, Wizara ipeleke wataalamu wa mifugo kutoa mafunzo ya ufugaji bora wa mifugo ya kimkakati yenye tija katika Jimbo la Moshi; tatu, kuwe na programu maalum ya kuzalisha mitamba wa maziwa wenye sifa zinazohitajika, ikiwa ni pamoja na mifugo mingine kama mbuzi wa maziwa, ng’ombe wa nyama, nguruwe na kuku. Wafugaji wengi hawana mbegu bora za ng’ombe wa maziwa, kwa ujumla huwa wanabahatisha.

Mheshimiwa Spika, nne, Wizara ihamasishe kuanzishwa kwa vikundi vya ushirika wa wafugaji mifugo na samaki ambavyo itakuwa rahisi kuwapatia huduma za mitaji na utaalamu.

Mheshimiwa Spika, pia Wizara itupatie wataalamu wa kuchimba mabwawa; Wizara ianzishe vituo vya kanda vya kuzalisha vifaranga wa samaki ili wafugaji wavipate kwa urahisi kwani vipo tu kwenye Mikoa ya Morogoro, Tabora, Ruvuma, Lindi, Tanga na Geita.

Mheshimiwa Spika, Wizara iwezeshe wazalishaji vifaranga binafsi ili wasaidie juhudi za serikali kwenye kukuza hii sekta; Wizara kwa kushirikiana na Halmashauri ya Moshi, wawezeshe kupandikiza vifaranga bora vya samaki katika Bwawa la Nyumba ya Mungu, kwani wavuvi waliniambia kwenye kampeni kuwa samaki wamehama, ikiwa na maana kuwa wamepungua.

Mheshimiwa Spika, Wizara iwe na huduma za uhakika za ugani zikizingatia lishe ya samaki; Serikali iwekeze kwenye kuanzisha mashamba darasa ya ufugaji bora wa mifugo ya kimkakati na samaki jimboni kwangu Moshi Vijijini ili wajifunze kwa vitendo (kama ilivyowasilishwa kwenye hotuba ya bajeti 2021/2022).

Mheshimiwa Spika, baada ya maelezo yangu hapo juu, naunga mkono hoja.