Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Mifugo na Uvuvi

Hon. Hamida Mohamedi Abdallah

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Lindi Mjini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Mifugo na Uvuvi

MHE. HAMIDA M. ABDALLAH: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi nami niweze kuchangia hoja iliyopo mezani ya Wizara ya Uvuvi na Mifugo. Kwanza nianze kumpongeza Waziri pamoja na Naibu wake na timu nzima ya Wizara yake kwa kuwasilisha bajeti yao ya kipindi hiki cha mwaka 2021/2022 katika utekelezaji wake.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia nampongeza Mheshimiwa Waziri kwa kutuunganisha Wabunge wote wa mikoa hii ambayo tunatoka maeneo ya ukanda wa bahari na kuweza kufanya kikao cha pamoja na kuchambua changamoto mbalimbali zinazowakumba wavuvi wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitumie nafasi hii kumpongeza sana Mheshimiwa Dkt. Bashiru, aliyekuwa Katibu wa Chama cha Mapinduzi Taifa kwa kusimamia vizuri uandishi wa Ilani yetu ya Chama cha Mapinduzi. Ilani yetu imeeleza vizuri katika eneo hili la sekta ya mifugo na uvuvi kwa lengo la kutaka kuleta mapinduzi makubwa na kuzifanya sekta hizi ziweze kukuza uchumi, kukuza ajira, kuendelea kuwekeza kwenye viwanda vidogo vidogo na kuendelea kuleta ustawi wa wananchi wetu ambao wamejiajiri katika sekta hizo na hatimaye kuongeza kipato na kuleta mapato makubwa kwa Taifa letu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nampongeza sana Waziri na timu yake kwa sababu mengi wameyazingatia, lakini nina mashaka makubwa sana katika utekelezaji wake. Kwa sababu fedha ya maendeleo inayoletwa katika sekta hizi ni ndogo sana. Pamoja na kwamba kuna mipango mizuri ya utekelezaji wa kipindi hiki cha 2021/2022, kama fedha hazikuja kama ambavyo tunatarajia, maana yake yale yote mazuri ambayo tunayategemea katika kuleta mapinduzi makubwa katika sekta hizi itakuwa ni kazi bure. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, naiomba sana Wizara ya Fedha, kumekuwa na changamoto kubwa sana ya utolewaji wa fedha katika sekta mbalimbali. Namwomba sana Waziri wa Fedha Mheshimiwa Mwigulu Mchemba aangalie namna gani atahakikisha anasimamia Sheria ya Fedha kupeleka fedha kwa wakati ili Wizara hizi ziweze kusimamia utekelezaji wa mambo ambayo tunayapanga na kuhakikisha kwamba tunaleta maendeleo kwa wananchi wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, najua kwamba Mpango wa Tatu wa Taifa umeelekeza nguvu kubwa sana katika uwekezaji wa uvuvi wa bahari. Naipongeza Serikali kwa sababu wameanza kwa kasi nzuri ya kuwekeza Bandari ya Mbegani na kwa kununua meli ya kuanza kufanya kazi katika sekta hii ya uvuvi. Hata hivyo, tukumbuke tuna wavuvi wadogo wadogo katika maeneo yetu; na sekta hii watu wengi wamejiajiri kwa sababu, sisi wazaliwa wa maeneo ya Pwani tangu wazee wetu, kazi kubwa ilikuwa ni shughuli ya uvuvi. Kwa hiyo, vijana wetu, watoto wetu, baba zetu, wamerithi kutoka kwa mababu zetu kufanya shughuli hii kuweza kujipatia kipato na kuweza kuendelea kumudu maisha yao. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika kipindi cha miaka mitatu mfululizo iliyopita, kumekuwa na changamoto kubwa sana ya kupata manyanyaso makubwa kwa wavuvi wetu. Hatutegemei kutokea yaliyotokea. Ndugu yangu Naibu Waziri, Mheshimiwa Ullega alikuwepo anayajua na ndugu zake wa Mkuranga, Lindi, Pwani na maeneo mengine Dar es Salaam anajua changamoto ambazo zimewakumba wavuvi wetu. Tunaiomba sana Serikali kuzingatia kwa sababu, wavuvi wetu wengi wamepoteza Maisha, wavuvi wengi wame-paralyze kwa kupata pressure, wavuvi wengi ndoa zao zimeharibika kwa sababu ya maisha yao kutoenda. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mvuvi mdogo ni mtu masikini sana, anapoingia baharini anapata samaki wa kumwezesha yeye kupata kipato na kuweza kumudu kuendesha maisha yake. Kwa hiyo, naiomba sana Serikali kuhakikisha kwamba tunasimamia kwenye eneo hili ili wavuvi wetu wasibughudhiwe. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunapotunga sheria na kanuni tuzingatie katika maeneo husika. Unapomtaka mvuvi mdogo akavue mita 50 kwenda chini ya bahari na boti yake aliyokuwa nayo ni dhaifu, hana vifaa vya kisasa, hivi unategemea huyu unamtakia maisha mema kweli! Naiomba Serikali kutazama namna bora ya kuhakikisha kwamba tunawasaidia wavuvi wetu wadogo wadogo ili kutengeneza ajira na waweze kumudu maisha yao. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naiomba Serikali kuhakikisha kwamba tunawaweka sawa wavuvi wetu wadogo kwa kuwapa elimu, lakini kuwawezesha kupata mikopo waweze kununua vifaa vya kisasa na waweze kuingia baharini kuweza kufanya shughuli zao. Huwezi kuanza jambo kubwa kama hujaboresha katika jambo dogo. Kwa hiyo, naiomba Serikali kusimamia katika eneo hilo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kila mara nilikuwa namfuata Waziri karibia miezi mitano sasa, kila tukikutana ajenda inakuwa moja ya ujenzi wa Chuo Kikuu cha Masuala ya Uvuvi na Usafirishaji Majini. Sisi pale Lindi Manispaa tumetoa tayari ekari 150. Kwa hiyo, naiomba Serikali, Waziri atakapokuja ku-wind-up atuambie ni lini wataanza kujenga chuo hiki ili tuwekeze katika rasilimaliwatu kuhakikisha kwamba baadaye tutapata wataalam watakaokuja kusimamia sekta hii ya uvuvi na usafirishaji? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika Mkoa wa Lindi tumebahatika kupokea wafugaji. Wafugaji hawa mmetuletea lakini hamjawatengenezea mazingira ya wao kuweza kuishi vizuri. Imekuwa mwenye nyumba anaombwa na mtu mmoja kwamba nina familia ya watu 20, naomba niwalete kwako. Unapowaleta unawaacha, huwahudumii, huwatengenezei mazingira yoyote. Wafugaji hao wanahangaika, hawana maeneo ya kulisha mifugo yao na badala yake wanavamia mashamba ya watu na kusababisha migogoro mbalimbali. (Makofi)

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa mzungumzaji)

MHE. HAMIDA M. ABDALLAH: Mheshimiwa Mwenyekiti, naiomba Serikali kuhakikisha kwamba wafugaji waliokuja katika Mkoa wetu wa Lindi, watengenezewe mazingira mazuri ya kuishi ili waweze kufanya shughuli zao za ufugaji. Pale Lindi hatuna shughuli za ufugaji, sisi tumezoea kuishi kwa kuvua, tunakula samaki, lakini bado tunahitaji kula nyama ili tuendelee kuboresha afya zetu. Kwa hiyo, Serikali ifanye kila namna ya kuona namna gani wanaweza kuboresha wafugaji waliowaleta kwetu Lindi. Wana familia zao, wanahitaji kuishi vizuri, watoto wao wanahitaji kusoma, kwa sababu maisha yao hayaeleweki, hawana uhakika wa kuishi; mara leo wako hapa, kesho pale, kesho kutwa kule. Kwa hiyo, hali siyo shwari. Naomba Serikali isimamie suala hili. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti…

MWENYEKITI: Ahsante sana Mheshimiwa. Nimekuachia kidogo umalizie, muda wako ulikuwa umeisha. (Makofi)

MHE. HAMIDA M. ABDALLAH: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana, naomba kuunga mkono hoja. (Makofi)