Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Mifugo na Uvuvi

Hon. Dr. Oscar Ishengoma Kikoyo

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Muleba kusini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

2

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Mifugo na Uvuvi

MHE. DKT. OSCAR I. KIKOYO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana kwa kunipatia nafasi nami nichangie hoja ambayo iko mbele yetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naanza na jambo moja dogo. Asubuhi wakati Mbunge mmoja anachangia, aliongelea Wizara kutaifisha mifugo wa watu wetu. Katika wilaya yangu ninakotoka, natumaini Mheshimiwa Waziri ananisikia, kuna mwananchi tangu mwaka 2017 ng’ombe wake 111 na kondoo tisa walitaifishwa kwa kisingizio kwamba wameingizwa kwenye Hifadhi ya Burigi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kesi ilikwenda Mahakamani, akafunguliwa Kesi Na. 155 ya 2017 akashinda. Huyo mwananchi siku hiyo hiyo akakamatwa tena akafunguliwa Kesi Na. 56 ya mwaka 2017, akashindwa. Akakata rufaa Na. 35 ya 2019 Bukoba, Mahakama ikaamuru arudishiwe mifugo wake. Mpaka leo tunavyoongea, tangu mwaka 2017 hadi leo anafuatilia ng’ombe wake 111 na kondoo tisa, hajapewa mifugo yake.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wakati Waziri anatoa majumuisho, nitaomba kauli ya Serikali, hiyo mifugo iko wapi? Kwa nini Wizara haitaki kumrudishia mwananchi ng’ombe wake?

MHE. JERRY W. SILAA: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa.

MWENYEKITI: Mheshimiwa Dkt. Oscar, subiri. Taarifa Mheshimiwa Silaa.

T A A R I F A

MHE. JERRY W. SILAA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka kumpa taarifa mzungumzaji kwamba kama mwaka 2017 walikuwa ng’ombe 111 watakuwa wamezaa. Kwa hiyo, madeni ya huyo mwananchi wake aweze kuyaongeza na wale ndama watakaokuwa wamezaliwa kwa muda huo.

MWENYEKITI: Mheshimiwa Dkt. Oscar, unapokea taarifa hiyo?

MHE. DKT. OSCAR I. KIKOYO: Mheshimiwa Mwenyekiti, naipokea na huko ndiko nilikotaka kuelekea. Mheshimiwa Waziri huyu mwananchi anaitwa Dunstan kutoka Kata ya Kyebitembe. Naomba wakati unatoa majumuisho utupe kauli ya Serikali. Whether Serikali iko juu ya sheria au utatuambia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wakati wa mjadala wa asubuhi ilikuwepo hoja ya NARCO. Wakati Mheshimiwa Spika anasitisha shughuli za Bunge asubuhi, naye ametoa maoni yake kuhusu NARCO.

MHE. ESTHER N. MATIKO: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa.

MWENYEKITI: Mheshimiwa Dkt. Oscar, subiri. Taarifa; Mheshimiwa Esther.

T A A R I F A

MHE. ESTHER N. MATIKO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka nimpe taarifa mzungumzaji kwamba hoja anayoiongea ni valid sana; na siyo mwananchi wake tu. Tukitaka kusimama hapa kila mmoja, kuna wananchi wengi sana ambao wanapitia hiyo adha. Kwa hiyo, Serikali tu labda ije na mkakati madhubuti kuhakikisha kwamba wale walioshinda kesi warudishiwe mali zao, ikiwezekana na fidia juu. Siyo kwa Muleba tu, ni karibia nchi nzima kuna matatizo kama haya. (Makofi)

MWENYEKITI: Mheshimiwa Dkt. Oscar.

MHE. DKT. OSCAR I. KIKOYO: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuwa ni suala la kisera na Kitaifa, naipokea taarifa yake.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wakati Mheshimiwa Spika anasitisha shughuli za Bunge asubuhi, naye alitoa maoni yake kuhusu NARCO na Mheshimiwa Rweikiza amesema asubuhi. Katika Wilaya ya Muleba tunao mgogoro mkubwa na shirika letu la NARCO. Katika Wilaya ya Muleba pekee, katika Kata ya Rutoro, tuna mgogoro na NARCO wa hekta 50,000. Katika kata zipatazo sita katika Jimbo la Muleba Kusini; Kata za Kyebitembe, Karambi, Mbunda, Kasharunga, Kakoma na Ngenge, tuna mgogoro na NARCO, mgogoro wa Mwisa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Waziri anafahamu, tumeliongelea hili kwa muda mrefu, lakini kutokana na remarks alizotoa Mheshimiwa Spika leo asubuhi, namwomba Mheshimiwa Waziri, hii ardhi hekta 50,000 ukiongeza hekta 70,000 ambazo tuna mgogoro nazo, atuachie Wilaya ya Muleba tukapange matumizi bora ya ardhi. Wao kama NARCO wabaki kama regulator watupe regulatory oversight tukapange matumizi bora ya ardhi yetu, tukalete wafugaji ambao tunao katika Wilaya ya Muleba, wanatosheleza. Hatutaki wafugaji kutoka nje, tunao wa kutosha na tutafuga…

MHE. FESTO R. SANGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa.

MWENYEKITI: Mheshimiwa Dkt. Oscar, pokea taarifa.

T A A R I F A

MHE. FESTO R. SANGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini kikao pia cha Waziri Mkuu cha tarehe 26 Februari, 2016 pale Kagera alitoa maelekezo kwamba NARCO wabainishe mpango bora wa matumizi ya ardhi na kama NARCO imeshindwa kuendesha waweze kuipendekeza Serikali wananchi waweze kugawiwa, hasa hilo nilikuwa naomba kumpa taarifa mzungumzaji.

MWENYEKITI: Mheshimiwa Dkt. Oscar.

MHE. DKT. OSCAR I. KIKOYO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nitaomba ulinde dakika zangu ninaona nina taarifa nyingi leo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunaomba wizara na kwa maana hiyo tunaiyomba Serikali suala la Mwisa II kwa Mkoa wa Kagera watuachie, uwezo tunao, watu tunao, na ng’ombe tunao. Wakatupatie utalaam na uangalizi kidogo na ushauri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Wilaya ya Muleba inazungukwa na Ziwa Victoria, nashukuru mzungumzaji wa mwisho amesema Kagera, Ziwa Victoria tumepewa pesa kwa ajili ya mikopo kwa wavuvi wetu, niishukuru Serikali kwa hilo. Lakini Waziri wa Fedha yupo hapa Tanzania tumebarikiwa kuwa na fursa nyingi kwa upande wa bahari, maziwa, lakini ukiingalia tunavyotumia hizo fursa ni aibu ni aibu sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa upande wa bahari tuna fukwe yenye urefu wa zaidi ya kilometa 1424 zenye kufaa kwa uvuvi ni kilometa 854 ambayo ni sawasawa na asilimia 60 zinafaa kwa ufugaji wa Samaki. Kwa upande wa Ziwa Victoria ninakotokea, tuna ufukwe wa kilometa 3450 ambapo kilometa 2587 sawasawa na asilimia 75 zinafaa kwa ufugaji wa Samaki. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukiangalia shughuli za uvuvi zinazoendelea na mazao tunayoyapata ni aibu, mahitaji ya Samaki kwa upande wa Tanzania kwa mwaka tunahitaji kati ya tani 700,000 mpaka 800,000 kwa mwaka. Lakini pamoja na fursa tulizonazo, pamoja na bahari tuliyonayo, pamoja na maziwa tuliyonayo tunazalisha tani 389,455 hata hatutoshelezi soko la ndani. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, walichukua dakika zangu, naomba niongezee mbili.

MWENYEKITI: Dakika moja na nusu nakupa.

MHE. DKT. OSCAR I. KIKOYO: Mheshimiwa Mwenyekiti, tunaagiza Samaki kutoka nje mpaka sasa na tunalo tatizo la vijana kukosa ajira, sasa tunaomba wizara ituambie ina mkakati gani kuhakikisha kwamba hilo gap la Samaki tunaoagiza kutoka nje kwa pesa ya kigeni tunalipunguzaje na kuhakikisha kwamba tuna-involve vijana wengi zaidi ili tuweze kwanza ku-create ajira, wakati huo huo kupunguza uagizaji wa Samaki nje wakati tuna maziwa, tuna bahari ambavyo vipo, tumepewa tu na Mwenyezi Mungu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, wameongezea suala la kanuni na tozo, niliongelea hapa wakati nachangia Mpango wa Tatu, nimuombe wizara wapitie tozo zote ambazo tunatoza kwenye mazao ya uvuvi wa Samaki. Lakini tunapoongelea tozo tuangalie tunalinganisha na nchi jirani za Kenya na Uganda ambao wote tuna-share kwa mfano Ziwa Victoria kwa upande wa bahari tuna-share na Kenya na wenzetu Msumbiji. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tusiishi kama tunaishi kwenye kisiwa, tunapotengeneza kanuni tuangalie na wenzetu, mchangiaji aliyemaliza kusema, amesema kina cha Ziwa Victoria na kina cha Ziwa Tanganyika vinatofautiana, kwa hiyo tunapotengeneza kanuni, tusitengeneze kanuni kwa nchi nzima tuangalie na mazingira ya maziwa yetu, tuangalie mazingira ya bahari, havifanani. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo naunga mkono hoja, lakini naomba Waziri atakaposimama atuambie hatma ya ng’ombe wa wampiga kura wangu 111 na Kondoo 9 wapo wapi? na wameshazaa wangapi? na faida yake ni nini? na anamrudishia huyo mpiga kura lini hao ng’ombe wake. Nashukuru sana. (Makofi)