Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Mifugo na Uvuvi

Hon. Joseph Michael Mkundi

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Ukerewe

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

2

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Mifugo na Uvuvi

MHE. JOSEPH M. MKUNDI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa nafasi ya kuchangia nitakuwa na mambo machache sana kwenye wizara hii na kimsingi kwa leo mchango wangu utajikita kwenye eneo la uvuvi, na nina sababu ya msingi. Natoka visiwa vya ukerewe na katika square kilomita 6400 ni asilimia 10 tu ya nchi ya kavu zaidi nimezungukwa na maji kwa hiyo watu wangu wengi ni wavuvi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza niwapongeze viongozi wa wizara Mheshimiwa Waziri, naibu na watendaji wote wa wizara hii, wamejitahidi sana kuitendea haki wizara hii na niombe mwenyezi mungu aendelee kuwasimamia kama mjadala ulivyoendelea kwa siku chache zilizopita uchumi wa Taifa hili unategemea sana sekta ya kilimo ikihusisha uvuvi na mifugo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mujibu wa hotuba ya Mheshimiwa Waziri, zaidi ya asilimia 90 ya wavuvi wetu ni wavuvi wadogo. Kwa hiyo, katika mambo ya msingi ambayo tunapaswa kuyafanya ni kujenga msingi, hasa kuwezesha sekta hii ya uvuvi kupitia wavuvi hawa wadogo ili kuweza kuifanya sekta hii ya uvuvi iweze kuwa na impact kwenye uchumi wa Taifa hili. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, miaka michache iliyopita wavuvi wetu walikuwa na shida sana na watumishi wa Wizara ya Uvuvi. Walikuwa kama wanawindana hivi, kama watu mahasimu. Sasa ili tuweze kujenga msingi imara kwenye sekta hii ya uvuvi, lazima kwanza tuanze kujenga mazingira mapya kwenye sekta ya uvuvi. Tu-harmonize hali tofauti na mazingira yaliyokuwepo kipindi cha mwaka mmoja au miwili iliyopita.

Mheshimiwa Mwenyekiti, huko nyuma ilitokea operesheni, kama ambavyo nimekuwa ninasema, watu wengi sana walipoteza mali zao. Sasa ni wakati ambao tunahitaji tujenge mazingira ambayo watumishi, wataalam, wavuvi, wataaminiana ili kama nilivyosema, sekta ya uvuvi iweze kuwa na impact. Kwa sababu tukiweza kuimarisha sekta hii; na kama nilivyosema, zaidi ya asilimia 90 ya wavuvi wetu ni wavuvi wadogo; na kwa maana hiyo sekta hii itatusaidia kutengeneza ajira, itaongeza kitoweo na vitu vingine kama hivyo ili kuweza kusaidia watu wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa jambo la kwanza ambalo nafikiri nichangie kwenye eneo hili, kwanza naomba Wizara yetu itambue kwamba wavuvi wetu wanahitaji sana elimu. Kuna matatizo kadhaa yamekuwa yanajitokeza, lakini hasa ni kwa sababu wavuvi wetu wanakosa elimu kutoka kwa wataalam. Watu wanapotoka Wizarani kwenda kutoa tu adhabu kwa watu wale kwa sababu wamefanya makosa, haijengi dhana iliyo nzuri kuwawezesha watu wetu kuwa imara na kuimarisha mitaji yao. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tutolee mfano wakati ule Wizara inatuma watu kwenda kuchoma makokoro na mitumbwi, hebu imagine mwananchi wa kawaida amejikokota kapata mtaji wake, kaanzisha biashara yake ya shilingi milioni 10 au shilingi milioni 15, siku moja tu ule mtaji unaporomoka. Lazima atakuwa frustrated. Kwa hiyo, kwanza tujikite kwenye kutoa elimu. Tuwe na kitengo maalum kwa ajili ya kuzunguka kwenye maeneo yetu kutoa elimu kwa wavuvi wetu ili yale wanayoyafanya, basi yaendane na miongozo, taratibu na mambo mengine kama hayo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nawapongeza sana Wizara, kupitia hotuba yao, nimeona wako kwenye hatua nzuri ya kutafsiri sheria, miongozo na kanuni zetu kwa Lugha ya Kiswahili. Ni jambo jema kwa sababu wavuvi wetu wengi hawaelewi lugha hii tunayotumia kwenye sheria zetu. Kwa hiyo, kama itatafsiriwa kuwa Lugha ya Kiswahili itatoa fursa kwa wavuvi wetu kuweza kusoma na kuelewa miongozo, kanuni na sheria zinazohusu kazi wanazozifanya. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba tu, kazi hii itakapokamilika, basi sheria hizi kwa Lugha ya Kiswahili iweze kusambazwa kwenye wilaya zetu ili wavuvi wetu waweze kuzipata na kuzisoma, waweze kuzielewa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo la pili ni juu ya tozo. Mwaka juzi, 2019 tulifanya marekebisho ya sheria hapa Bungeni; na katika sheria hizo tulipunguza baadhi ya tozo zilizokuwa zinakabili wavuvi wetu. Kwenye eneo hili, ni kweli baadhi ya tozo zile zimeondolewa, lakini bado kuna tozo ambazo ni kero kwa wananchi wetu. Naomba Serikali iendelee kuziangalia kupitia Wizara, iangalie tozo nyingine ambazo siyo za msingi sana tuweze kuzitoa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vile vile naiomba Wizara, wavuvi wetu hawa wa kawaida wanasumbuliwa sana pale ambapo mamlaka zinapoenda kukusanya tozo. Kwa mfano, kuna tozo za TASAC, ushuru wa mitumbwi, leseni na kadhalika. Mbaya zaidi ni kwamba tozo hizi zinatozwa kwa nyakati tofauti tofauti, jambo linaloleta usumbufu kwa wavuvi wetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba Wizara ione uwezekano wa kuunganisha tozo hizi ili zote ikiwezekana ziwe zinatolewa kwenye center moja halafu sasa Serikali inaweza kuchambua tozo zile kama ni ya TASAC au sehemu nyingine, kuliko kila wakati taasisi inakwenda kuwatoza wavuvi wetu, inakuwa ni usumbufu kwa watu hawa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo lingine ambalo nafikiri nilichangie ni kwenye uvuvi wa vizimba. Tumekuwa tunahamasisha sana wavuvi wetu kufanya uvuvi wa vizimba; ni jambo jema. Kupitia hotuba ya Mheshimiwa Waziri, inaonekana kwenye Ziwa Victoria kwa mwaka mmoja; mwaka 2019/2020 vizimba vilikuwa 431. Mwaka huu kwa mujibu wa utafiti wao, vizimba ni 473; ni jambo jema. Bado kwa mtazamo wangu tunahitaji kufanya zaidi. Tunahitaji tuwekeze zaidi kwenye uvuvi wa vizimba.

Mheshimiwa Mwenyekiti, namna pekee ambayo tunaweza tukawasaidia watu wetu, kwa sababu moja kati ya changamoto zilizopo kwenye uvuvi wa vizimba ni gharama za kuanzisha shughuli hizi za ufugaji wa samaki. Kwa mwananchi wa kawaida kwa gharama zilizopo hivi sasa, ili mtu aanzishe kizimba anahitaji zaidi ya shilingi milioni 10. Ni wananchi wachache sana wa kawaida wenye uwezo huo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, bahati mbaya sana kumekuwa na shida sana kupata vifaranga vya samaki. Hata chakula cha samaki hawa kimekuwa na shida kubwa. Kwa hiyo, naomba Serikali kupitia Wizara, ione uwezekano ili chakula cha vifaranga hawa kiweze kupatikana kwa bei nafuu. Vilevile vifaranga wazalishwe kwa wingi wapatikane. Pia zile gharama nyingine kwa mfano za kufanya Environmental Impact Assessment, angalau zake zipungue ili mwananchi wa kawaida awe na uwezo wa kuanzisha kizimba akafuga samaki, jambo litakalotusaidia kuondokana hata na ile migogoro ya uvuvi usio halali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya hayo machache, nashukuru sana kwa nafasi, Mwenyezi Mungu akubariki sana. (Makofi)