Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Mifugo na Uvuvi

Hon. Ally Mohamed Kassinge

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kilwa Kusini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

2

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Mifugo na Uvuvi

MHE. ALLY M. KASSINGE: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Nami nianze kuchangia Hotuba ya Bajeti ya Wizara ya Mifugo na Uvuvi, kwanza kabisa kwa kupongeza uongozi wa Wizara ambao kwa ujumla umeanza kuleta matumaini mazuri kwa Watanzania hususan kwenye Sekta ya Mifugo na Uvuvi. Kwa hiyo, nawashukuru na ninawapongeza sana viongozi kuanzia Mheshimiwa Waziri, Naibu Waziri na Makatibu Wakuu wote. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kubwa zaidi ambalo linatupa matumaini ni kwamba uongozi huu umejikita kwenye ubobezi wa sekta wanazosimamia. Ukiangalia Katibu Mkuu wa Uvuvi, amejikita katika masuala hayo, Katibu Mkuu wa Mifugo kadhalika ni mzoefu wa masuala hayo. Ndugu yangu Mheshimiwa Ulega, Naibu Waziri ni mzoefu wa masuala hayo kitaaluma na pia kimakuzi. Kwa hiyo, Watanzania hatuna shaka katika hili.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la kwanza ambalo nataka kuanza kuchangia katika hotuba hii, kwanza kabisa ijitambue kwamba ni Wizara ya Mifugo na Maendeleo ya Uvuvi na siyo Wizara ya Mifugo na Kukwaza Uvivu Tanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nazungumza hivi kwa sababu mengi ambayo wachangiaji wenzangu wamezungumza, niwarejeshe tu katika kanuni za mwaka 2020, kanuni ya 66(1)(d)(f)(g). Vifungu hivi vinakwaza kabisa maendeleo ya uvuvi katika nchi yetu ya Tanzania. Sihitaji nidadavue vinakwaza vipi? Bahati nzuri wachangiaji wenzangu waliotangulia wameelezea. Naomba katika mabadiliko ya kanuni Mheshimiwa Waziri anayokwenda kuyafanya, azingatie haya ambayo kwenye vifungu nivyovitaja yanakwanza uvuvi Tanzania. Hilo la kwanza. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, la pili, naomba wataalam wa Sekta ya Uvuvi, wanapokwenda kutengeneza kanuni mpya, ziwe ni kanuni shirikishi na pia ziwe ni kanuni zinazoendana na mazingira husika. Kwa mfano, sisi watu wa Pwani, taratibu za uvuvi zinazingatia masuala ya nyakati, nyakati za pepo na miandamo ya miezi. Kwa mfano, unapokataza watu wasivue mchana kwa ujumla wake tu, wakati taratibu za uvuvi wa baharini zinazingatia mwandamo wa mwezi, kuna kipindi cha mwezi mchanga, kuna kipindi cha mwezi mpevu, kuna kipindi cha mwezi mwangavu, hilo lizingatiwe. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine kuna hawa samaki maarufu kama Kambakochi au Kambamiti. Kule Kilwa ni tofauti na Rufiji ambapo Kilwa uvuvi wa Kambakochi unatakiwa uanzie mwezi Januari, lakini leseni ambazo Wizara inatoa inaanzia mwezi Aprili. Maana yake ni kwamba mpira unapigwa huku, golikipa anaangukia huku; tofauti kabisa. Hapa tunaomba izingatiwe pia, ndiyo maana tunasema kwamba sheria hizi na kanuni hizi ziiwe shirikishi, ziulize wazoefu wa maeneo husika. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine ambalo ninaomba ni kukuza Sekta ya Uvuvi na hususan katika Sekta ya Wilaya ya Kilwa, ni kuhakikisha kwamba pale Kilwa Kivinje ambapo nimejiridhisha kabisa samaki wengi ambao wanaliwa Tanzania wanatoka Kilwa; ukiona samaki wanaliwa Dar es Salaam wanatoka Kilwa, ukiona samaki wanaliwa mikoa mingine ya Kusini, wenzetu jirani zetu Mtwara na Ruvuma wanatoka Kilwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ushahidi wa hili wale ambao wanatumia barabara hii maarufu kama ya Kibiti - Lindi, ukifika pale Somanga, ukinunua samaki unakuja Dar es Salaam au unakwenda Mtwara au unakwenda Ruvuma maana yake hao ndiyo samaki wa Kilwa. Kama hivyo ndivyo, kuna haja ya kuanzisha soko la samaki la kisasa pale Kilwa Kivinje ili wavuvi wetu wawe na uhakika wa soko. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitoe taarifa tu kwenye Wizara hii, katika utaratibu usio rasmi jirani zetu wa Kongo wanakuja Kilwa kununua samaki tani za kutosha. Tumeandaa utaratibu gani wa kuingiza mapato ya Taifa kwa kuuza samaki nje ya nchi? Tuko katika utaratibu usiosimamiwa vizuri na Wizara. Nashauri katika eneo hili, Wizara isimamie inavyotakiwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine Mheshimiwa Waziri, matumizi ya nyavu zilizozuiliwa. Kimsingi nyavu hizi, wananchi wetu wavuvi hawa masikini wa Tanzania wanavua kulingana na aina ya samaki wanaovua. Kwa mfano, dagaa wote tunawafahamu, wanahitaji milimita kumi. Wote tunajua dagaa ni visamaki vidogo vidogo sana, vinahitaji milimita sita, ikizidi milimita saba. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa tangu kumetolewa zuio la kukataza zuio la kukataza uvuvi wa nyavu hizi, uvuvi wa mchana, wavuvi wetu wamebaki kuwa masikini, wamechomewa nyavu zao, wamechomewa vyombo vyao, vimeangamizwa, hii ni msiba mkubwa katika Taifa hili na siyo haki kufanya katika nchi ambayo iko huru. Malengo na matarajio ya Watanzania ni kuona kwamba kila sekta inasaidia wahusika. Kama ni Sekta ya Kulima isaidie wakulima, Sekta ya Uvuvi isaidie wavuvi, Sekta ya Ufugaji isaidie wafugaji. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sihitaji nizungumzie kilio cha Wana-Kilwa cha kuchomewa nyavu zao, kuangamiziwa vyombo vyao vya uvuvi, kilichofanywa huko na Waziri ambaye amemaliza muda wake. Nina matarajio mazuri na Mheshimiwa Waziri wewe kaka yangu, hautafanya kama mwenzako aliyekutangulia. Utakuwa ni msikivu, utakuwa ni mwenye huruma kwa Watanzania masikini hususani wavuvi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sambamba na hilo, niseme tu kwamba katika mpango wa Wizara wa kuanzisha bandari za uvuvi, nimeona imetajwa Mbegani hapa, lakini mwanzoni Kilwa ilikuwa kwenye mpango. Tunaomba mpango huu kwa miaka mitano hii, Kilwa isisahaulike. Kilwa Masoko pale kuna kina cha kutosha, kuna bandari ya asili. Kwa hiyo, ule mpango wa miaka mitano ubaki vile vile. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja. (Makofi)