Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Mifugo na Uvuvi

Hon. Nicodemas Henry Maganga

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mbogwe

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Mifugo na Uvuvi

MHE. NICODEMAS H. MAGANGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi na fursa hii niweze kuchangia Sekta hii ya Uvuvi na Mifugo. Awali ya yote napenda nimshukuru Mwenyezi Mungu kwa kunipa nafasi niweze kuweka mawazo yangu kwenye hii Sekta ya Mifugo na Uvuvi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakumbuka mwaka 2020 tulikuwa kwenye uchaguzi. Miongoni mwa vitu tulivyokuwa tukitembea navyo majukwaani, ukisoma ukurasa wa 52 ilani yetu ambayo ilikuwa andiko letu kuu kuweza kuwaomba ridhaa wananchi ili tuweze kuwaongoza katika Chama cha Mapinduzi, tuliahidi kwamba tutawasaidia wafugaji pamoja na wavuvi. Hata hivyo, kila kinachoendelea sasa hivi kwenye hili Taifa, leo ni mwezi wa Saba sasa, unaona kabisa kwamba bado hatujatekeleza huu ukurasa wa 52. Kwa hiyo, namwomba kaka yangu Mheshimiwa Mashimba pamoja na Mheshimiwa Ulega, kwa kuwa wao ndio wasimamizi wakuu wa Wizara hii, kwanza sheria zilizotungwa za hiyo sekta ni chonganishi, naweza nikasema hivyo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ikumbukwe kwamba hata Mheshimiwa Rais wa Awamu ya Tano tulimchukia sana Kanda ya Ziwa wakati akiwa sekta hiyo, lakini ukweli ni kwamba baada ya kukua, nami kuingia kwenye michakato hii ya kisiasa na kuona kabisa sheria ziliwekwa vibaya; kwa maana hiyo mimi nikushauri Mheshimiwa Mashimba, ongea na Mheshimiwa Rais, kuna vipengele muhimu vya kuweza kufanyiwa marekebisho ili uweze kurudi hata Bungeni mwaka 2025, lazima sheria zibadilishwe, maana wafugaji kwenye hili Taifa wamekuwa kama wakimbizi. Wewe ni Msukuma mwenzangu tunaongea lugha moja na tumetoka sehemu moja, lakini kiukweli yaani ukisimamia hizo sheria lazima watu watakuchukia hata kama ni mtoto mdogo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukiangalia wafugaji wanavyoteseka kwenye mapori hasa kwenye Jimbo langu la Mbogwe, kuna utitiri wa mapori, nilishaongea na Mheshimiwa Waziri tukiwa wawili na alisema atanisaidia, sasa leo nitashika shilingi ili anihakikishie kwamba Mbogwe katika bajeti yake atanisaidia mabwawa mangapi na majosho mangapi ili niweze kuachilia kushika shilingi? Waheshimiwa Wabunge naomba mniunge mkono kwenye hili kama tutashindwana na kaka yangu ili kusudi tupinge, tusiwe tunapitisha tu kila bajeti bila hata kujua kinachoendelea. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitumie nafasi hii kuzungumzia wafugaji wa Tanzania. Lazima tukubaliane kwamba; unajua katika maisha huwa kuna Kiswahili kinasema tunaishi kwa kutegemeana. Tukirudi kwenye historia ya nyuma, miaka ya nyuma huko, wakati wa utawala wa Mwinyi, ikumbukwe kwamba Wasukuma professional yetu sisi ni wafugaji. Ukiangalia Wamasai miaka ile tulikuwa tunagombana nao maporini, kazi yao ilikuwa kuja kutuibia ng’ombe ili nao waende wakafuge. Sasa hivi ukiangalia Wasukuma wengi wameacha biashara ya kufuga ng’ombe. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tukiangalia Taifa tuna-force kuingia kwenye utajiri; na hotuba ya Mheshimiwa Rais wa Awamu ya Tano alizungumzia kwamba hata Wabunge tutafute ubilionea. Kwa maana hiyo mimi kama Msukuma sasa, sheria za ufugaji zikirekebishwa vizuri, mimi nitarudi kwenye professional yangu. Hakuna haja ya kuhangaika na network, wala haya mamitandao sijui mara M-Pesa rusha huku, fanya hivi; maana sisi Wasukuma professional yetu ni wafugaji. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukisoma hata maandiko ya Neno la Mungu kulikuwa na Mfalme Daudi, alikuwa ni mchunga ng’ombe; hakuwa hata na Malaria maana alikuwa anakunywa maziwa ya ng’ombe. Hata mimi wakati bado sijaja mjini nilikuwa siugui typhoid, maana maziwa ya ng’ombe yale wale waliosoma sayansi wanaweza wakakuelezea ni nini maana ya kuwa na faida ya ng’ombe. Leo yanapokuja hata maziwa haya ya kiwandani, nakuwa sipati picha maana kila mara magonjwa yanazidi kuwa mengi na mpaka tunataka kuingia kwenye chanjo ambazo hazina sababu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hii ni kutokana na kuwadharau wafugaji na sisi Wasukuma tunaonekana washamba kwenye Taifa hili. Ni kweli sisi Wasukuma tuna sifa moja, yaani mkiingia pori moja ni kufyeka kwa kwenda mbele ili kusudi kujaribu kujitandanua kimaisha. Kwa kuwa sasa Chama cha Mapinduzi kiliahidi kwamba kwanza kwenye hizi hifadhi zetu tutapewa maeneo, tupewe sasa maeneo. Huu mwaka ni wa kwanza, bado miaka minne tuingie kwenye uchaguzi mwingine, tusiongee story. Binadamu sisi huwa tunasahau, yawezekana kabisa shida tuliyoipata kwenye kampeni watu wanaweza kuwa wameshasahau, lakini nataka niwahakikishie, tusipotimiza mambo haya, tutapata taabu sana mwaka 2025. (Kicheko/Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niongelee upande wa uvuvi. Wananchi wangu wengi wako Ziwa Victoria. Nilishawahi kuongea na Mheshimiwa Mashimba na leo niongee naye nikiwa kwenye vyombo. Wavuvi wanapata taabu sana. Kuna mageti; ukitokea pale tulipokuwa na wewe Mheshimiwa Waziri na Rais wa Zanzibar, tulienda kwenye mwalo mmoja wa Mganza, ulisikia shida za wafanyabiashara wale na walikueleza changamoto wanazokabiliana nazo. Yamewekwa mageti mle njiani ya kipigaji. Wanahangaika wafanyabiashara wa dagaa, wafanyabiashara wa samaki wanafanyabiashara kwa shida, wanasumbuliwa na watu hawa wa misitu. Serikali ni moja lakini inakuwa kana kwamba Serikali ziko mbili. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimwombe Mheshimiwa Mashimba, kaka yangu, Wizara hiyo kwa kuwa naye ameipenda na Rais wa Awamu ya Sita amemwamini, itendee haki hiyo nafasi. Kumbuka kwamba kuna mwenzio ambaye hata kwenye Ubunge wake amepita kwa wakati mgumu sana, nikimsikia sasa hivi speech zake kidogo saa hivi anatoa hotuba ambazo zina urafiki na wananchi kule anakotokea. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukiangalia wavuvi wengi wanakufa wakiwa wanakimbizana na operation za mle ziwani. Mwaka 2016 kuna marafiki zangu watatu walikufa wakiwa wanafukuzwa na watu wa maliasili kwenye Kisiwa cha Rubondo walikuwa wanakaa Chakazimbwe. Kuna Visiwa vya Chakazimbwe, Mrumo, Iramba na Mjuno; Mheshimiwa Mashimba ukifanya ziara huko ukaongea na wale watu, utapata ukweli wangu, tarehe ya leo 27 nakushauri pamoja na Naibu wako mfanye ziara kwenye Visiwa vya Yozu, Nyamango humo, mkaongee nao. Wale wa professional yenu wawaambie na ili mje sasa siku moja mlete hata Muswada wa kufanya marekebisho ili kusudi nao waishi vizuri na waweze kuendelea vizuri na uvuvi wao. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kwenye Kamati ya Matumizi nishike shilingi ili kaka yangu anihakikishie bajeti yake atanisaidiaje kwenye Jimbo langu, tusiongee tu maneno maneno hapa halafu mwisho wa siku tusiweze kufanikiwa chochote. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda jambo lingine tena niliweke sawa hapa. Namshukuru Mungu jana mchango wangu mwenyewe nilichangia na niliongea maneno mengi; namshukuru Mheshimiwa Lukuvi ameniahidi vitu vingi atanisaidia. Tukiangalia hii Sekta ya Uvuvi, tukaangalia na hii sekta ambayo tuliichangia jana, ni vitu viwili vinakaribiana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa maana hiyo, jana kwa kuwa Mheshimiwa Lukuvi alisema atakuja Mbogwe, ni vyema sasa tuje tupitie maeneo na mazingira ya Mbogwe yale ili kusudi tuangalie hata tunapokuja kubadilisha sheria mkaona na usumbufu ule wananchi wa Mbogwe wanaoupata kwenye yale mapori utakuwa umenisaidia sana kaka yangu. Sijui unanisikia Mheshimiwa Mashimba. Nakuona kama unanisikia, lakini naomba andika hiyo halafu uje uitolee maelezo kwenye kuhitimisha hotuba yako. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine nikushukuru wewe, leo ni mara yangu ya tisa sasa kuchangia hapa. Mwanzoni niliongea vitu vingi na nikaiomba Serikali ya Awamu ya Tano iweze kutusaidia na isitubague sisi watu wenye elimu kidogo, lakini karama zetu zinakubali na kuweza kufanya vitu vikubwa kwenye hili Taifa, naomba nawe maneno yangu uyasikilize. (Makofi/Kicheko)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunapoongelea neno viwanda, ni vyema na sisi tujitegemee na tujitambue. Tusitegemee tu kila kitu; nimemsikiliza mchangiaji wa kwanza anajaribu kutolea mifano Botswana, wapi na wapi; ni vyema tujiamini, kwa sasa tulipo hapa, tuko sawa sawa kabisa. Tukiwa tunachukua mifano Ulaya tu, kila kitu Ulaya, hatutaenda popote pale. Sisi tuliumbwa na Mungu, tuliwekwa kwenye ardhi ya Tanzania, Mungu alituamini, tena akatupa Taifa lenye makabila mengi na Taifa letu halijapata vita hata ya kikabila. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni vyema kila mmoja sasa akithaminiwa; msomi amthamini ambaye hajasoma. Huyu ambaye hakusoma, amthamini msomi. Tunaishi kwa kutegemeana, maana hata sisi ambao hatujasoma hatuwezi kuingia kufanya operation kwenye hospitali yoyote, lakini tumekuwa na shida sasa hivi humu Bungeni, kumekuwa na mvutano fulani na kuchukiana sisi kwa sisi; ma-professor na wale wasio ma-professor. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nawaomba Wabunge, sote humu tuna akili timamu na tumevuka mishale mingi kufika kuingia kwenye jengo hili, tuheshimiane kuanzia leo. Naomba kwa kauli mniunge mkono, hiyo vita isiendelee.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana. Ahsante katika jina la Yesu.

MWENYEKITI: Ahsante sana Mheshimiwa Maganga. Naamini Mheshimiwa Waziri amekusikia vizuri na ninaamini ataweza kukusaidia vizuri.

MHE. NICODEMAS H. MAGANGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nitaunga mkono akinifafanulia, maana nashika shilingi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante.