Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Mifugo na Uvuvi

Hon. Edward Olelekaita Kisau

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kiteto

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

2

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Mifugo na Uvuvi

MHE. EDWARD O. KISAU: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana kwa nafasi hii. Kwanza kabisa nampongeze Waziri, Naibu Waziri, Katibu Mkuu na timu yao wote.

Mheshimiwa Spika, nampongeza sana Mheshimiwa Balozi Dkt. Bashiru, juzi alituwekea foundation nzuri sana. Tunapozungumza habari ya kilimo au mifugo na uvuvi, kama asilimia 65 au 70 ya Watanzania wako huko; we have no option, lakini Bunge hili umenisaidia, kwamba baada ya miaka mitano Watanzania wanufaike na sekta hizi za mifugo, uvuvi na kilimo. Najua pengine tutakuwa tumechelewa mwaka huu, lakini tunaanza kutema cheche hapa ili sasa mwaka wa fedha ujao Serikali ijue kabisa, kama tunataka kuweka legacy kwenye kilimo, mifugo na uvuvi, ni lazima tu-commit pesa nyingi sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nilikuwa nasoma takwimu za Serikali hapa, tunaambiwa kuna mifugo karibu milioni 33.6. Ilani ya Chama cha Mapinduzi imeainisha vitu vingi sana ambavyo tumeahidi kufanya kwa miaka mitano ijayo. Hekta za mifugo kutoka 2,788,000 hadi hekta 6,000,000. Kwa hiyo, maana yake tumeahidi kutenga hekta 3,211,000. Ili mifugo iweze kustawi ni lazima wawe na maeneo.

Mheshimiwa Spika, mzungumzaji aliyepita alikuwa anasema ng’ombe anazaliwa Kagera anaishia Lindi, there is absolutely nothing wrong. Ng’ombe kuhama ni coping mechanism ya magonjwa, wanatafuta maji na malisho. Wafanye nini sasa kama hifadhi zinachukuwa maeneo yao? Kuhama kubaya ni ile ya kusababisha migogoro na watumiaji wengine wa ardhi. Hiyo hapana, lakini kuhama ni coping strategy.

Mheshimiwa Spika, vile vile ilani inazungumza na nilikuwa nasoma hotuba ya Wizara hapa; inasema mtajenga majosho 129. Ni kidogo sana na hii inatokana na bajeti yenu kuwa ndogo sana. Kwa mfano, Kiteto peke yake majosho tunayohitaji ni 48, kwa sababu ilani inasema lazima katika kila kijiji chenye mifugo kiwe na josho. Sasa kama mnapewa bajeti ya kutengeneza majosho 129, Kiteto peke yake inahitaji 48, haiwezekani. It is a very big joke.

Mheshimiwa Spika, vile vile ilani imesema tutajenga mabwawa kama 400 hivi kwa miaka mitano. Kwa hiyo, in average ni mabwawa karibu 91 kila mwaka, lakini hapa ninyi mmepewa mabwawa manne tu. Kama siyo manne, Matano. It is a very big joke. Kwa Kiteto peke yake, pungufu ya malambo ni 44, halafu tunaweka kwenye bajeti manne.

Mheshimiwa Spika, kwa kuwa tumedhamiria kwamba Bunge hili liwanyanyue Watanzania katika sekta hizi muhimu sana, nashauri; kwa sababu nilikuwa naangalia hapa, uvuvi na mifugo; na imetokea trend siku hizi ukichanganya mifugo na kilimo kuna sekta moja itapewa pesa nyingi kuliko nyingine. Ukichanganya maji na mifugo kuna sekta moja itapewa hela kutoka nyingine. Sasa maji tunafanya vizuri, kilimo tunaelekeaelekea hivi kidogo, sasa mmechanganya uvuvi na mifugo. Sasa uvuvi inachukua bajeti mmetenga hapa karibu shilingi bilioni 90 na kitu kwa uvuvi halafu mifugo shilingi bilioni 16.

Mheshimiwa Spika, tukitaka kufanya vizuri zaidi labda huko mbele tutenge kabisa, tuwe na Wizara maalum ya Mifugo, tuwe na Wizara maalum ya Uvuvi, tuwe na Wizara ya Kilimo. Tukitenga hivi tutaweza kuweka nguvu kubwa zaidi.

Mheshimiwa Spika, nami napendekeza tena, lazima tuji-commit, kuweka asilimia 10 ya mapato yetu kwenye uvuvi, kwenye mifugo na kilimo. Tukifanya hivyo tutaweka investment, lazima iwe serious. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mzungumzaji aliyepita alikuwa anatoa mifano ya nchi nyingine kama Ethiopia, Rwanda na Uganda; na Botswana by the way, ndiyo inafanya vizuri zaidi kuliko nchi yoyote Afrika kwa ku-export beef, lakini angalia investments zao, ni kubwa zaidi.

Mheshimiwa Spika, nami nakubaliana nawe. Kuna siku nimetembelea NARCO hapo, kwenda kuangalia ng’ombe pale. Ni kweli, yaani hata majani yaliyoko pale hayawezi kumalizwa na ng’ombe walioko NARCO. Ni afadhali mngewapa wafugaji tu. Kwa hiyo, ni lazima tuangalie tija kwa miradi tunayowekeza kwenye sekta hizi.

Mheshimiwa Spika, tulikuwa tunasoma ilani hapa; tani za kunenepesha mifugo nchi hii ni 900,000 peke yake na tuna ng’ombe milioni 33 na tumejiwekea malengo ya kutengeneza hizo tani milioni nane. Kwa hiyo, huo ni mfano tosha tu kwamba hatuja-invest heavily kwenye mifugo. Kwa hiyo, tusishangae sana.

Mheshimiwa Spika, hata hivyo, pato la Taifa asilimia 7.9 siyo kidogo. Wakati mwingine huwa nafikiri kwamba hatutengenezi mipango sahihi ya ku-capture contribution ya mifugo. Kama kuna wanywa bia hapa, hakuna mnywa bia hata mmoja asiyekula nyama. Nami sitaki kuvuruga Bunge lako, lakini ningesema leo wanyooshe mikono wanaokula nyama hapa, watasimama mpaka wale waandishi wa habari ambao wanapiga kamera hapa. Hiyo ni contribution ya mifugo. Kwa hiyo, I think hamjaweza ku-capture kabisa contribution ya mifugo.

Mheshimiwa Spika, kwa Jimbo la Kiteto peke yake tuna mifugo 500,000, mbuzi 500,000, siyo kidogo hiyo, ni contribution kubwa sana. Ripoti zeni zinasema kuna watu milioni nne wanategemea direct income kutoka kwenye mifugo katika nchi hii. Kwa hiyo, lazima tuwe serious katika ku-invest, tuweke pesa nyingi ili mifugo yetu iweze kuleta tija kwa Taifa.

Mheshimiwa Spika, nilikuwa naangalia ripoti zangu za Kiteto hapa wataalam wanaohitajika, ukiangalia wataalam wanaohitajika kwenye sekta hii ni 106 halafu waliopo ni 35, pungufu 40. Kwa hiyo lazima kweli tu-invest kwenye mifugo na uvuvi kama tunataka kwenda mbele huko. Miaka miwili iliyopita sisi tumepata mvua kubwa sana na Kiteto sasa tuna wafugaji wanakula Samaki sasa.

T A A R I F A

MHE. ESTHER MATIKO: Mheshimiwa Spika, taarifa.

SPIKA: Taarifa Mheshimiwa Esther Matiko nimekuona.

MHE. ESTHER MATIKO: Mheshimiwa Spika, ahsante nataka tu nimpe taarifa ndogo mchangiaji wakati anachangia amesema tukiamua kuazimia nakuchukua walau asilimia kumi ya mapato, tungeweza kufika mbali upande wa mifugo, uvuvi hata kilimo. Nimkumbushe tu kwamba ni Azimio la Malabo ambalo tumelisaini ambalo linatutaka walau tutenge asilimia kumi ya bajeti ya Serikali kwenye eneo la kilimo, mifugo na uvuvi. Kwa hiyo, siyo kwamba tuhiari tu kama mapato ila ni Azimio ambalo tumelisaini. Ahsante. (Makofi)

SPIKA: Taarifa hiyo unaipokea Mheshimiwa Edward.

MHE. EDWARD O. KISAU: Mheshimiwa Spika, nakubali na napokea, lakini ninataka tu nimuambie kwamba hatuhitaji Malabo actually ili tuamue ku-invest ten percent. Malabo declaration ni kwamba tu wametusaidia, lakini kweli kama tungekuwa tunasubiri Malabo declaration na Malawi na hata hivyo pamoja na declaration hiyo investment inayoenda kwenye kilimo ni less than one percent, less than one percent. Kwa hiyo, kwa kweli lazima, lazima tutoke huku tu-invest every kwenye uvuvi, tu-invest every kwenye mifugo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nasema hivi, siku hizi Kiteto tumepata kama mabwawa mawili ya samaki na tumeanza kujifunza kula samaki na wilaya yangu kwa mara ya kwanza kwa mwaka fedha wamesema tutapata kodi kama milioni nane hivi inatokana na Samaki na wafugaji wameanza kutengeneza leseni kutoka kwenye halmashauri.

Mheshimiwa Spika, halafu anakuja mtu wa maliasili eti anawaambia wale wafugaji wale brand new, watu ambao wanataka kula samaki for the first time, halafu unawaambia tena eti hairuhusiwi, sijui nini, yaani tunawaongezeeni watu wa kula samaki ili tuongeze tija zaidi halafu mtu anatwambia mambo ya leseni yametoka wapi ni confusion na ndio ile Mheshimiwa Rais wetu alikuwa anasema concept of one government. Kwa hiyo, kwa kweli lazima tuwatetee, lakini baada ya kusema haya lazima sasa na ninyi mifugo muwe serious nilikuwa nasoma ripoti zenu hapa.

Mheshimiwa Spika, wanasema eti ng’ombe milioni sita zimekamatwa kwenye mapori tengefu, ng’ombe milioni sita ipo kwenye ripoti hapa, na kwanza nashangaa kwa sababu hawajaandika jimbo langu na kila siku wanakamatwa hapo na pori hili Tengeru linaitwa Mkongoroyo, lazima muwatete wafugaji hawa, ipo kwenye ripoti zenu. Naona Waziri anamuuliza mwenzake hapo. (Makofi/Kicheko)

Mheshimiwa Spika, ukisoma ukurasa wa 205 nendeni mkasome data za mifugo kukamatwa kwenye mapori haya, ni lazima kama nchi tusimame huu ni uchumi hatutaki ng’ombe hizi zikamatwekamatwe hovyo ni uchumi wa wananchi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, baada ya kusema hayo, nakushukuru sana na naunga mkono hoja. (Makofi)