Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi

Hon. Maimuna Salum Mtanda

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Newala Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

2

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi

MHE. MAIMUNA S. MTANDA: Mheshimiwa Naibu Spika, nawapongeza sana kwa kupunguza kiasi kikubwa cha migogoro iliyokuwa na Maafisa Ardhi wasio waaminifu ambao walikuwa wanagawa ardhi moja kwa zaidi ya watu wawili, changamoto hii ilikuwa kubwa sana katika baadhi ya maeneo ikiwemo Halmashauri ya Wilaya ya Kilwa. Hongereni sana.

Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na mafanikio hayo bado kuna baadhi ya changamoto za ardhi ikiwemo moja, mgogoro wa mpaka kati ya Halmashauri ya Wilaya ya Newala na Halmashauri ya Wilaya ya Masasi kati ya eneo la Mpanyani karibu na Nangoo. Kutokana na mgogoro uliopo ambao haujapata suluhisho, msimu wa korosho unapowadia Halmshauri hizi mbili hugombania wapi kwa kwenda kuuza korosho zao, kila Wilaya huvutia kwake ili wapate mapato. Mgogoro huu umechukua muda mrefu tunaomba utatuliwe.

Pili, katika Kijiji cha Chilangala eneo la Mbwinji, watu wa Mamlaka ya Maji (MANAWASA) wamechukua ardhi ambayo wanakijiji walikuwa wamelima mazao yao ya chakula na biashara bila kulipa fidia kwa wananchi husika wa Chilangala kwa ajili ya mradi wa maji. Changamoto hiyo imezua mgogoro mkubwa kwa wananchi wa Chilangala ambao hawajajua hatma ya ardhi yao iliyochukuliwa. Tunaiomba Wizara ya Ardhi iingilie kati ili wananchi wa Chilangala walipwe fidia ya ardhi yao.

Mheshimiwa Naibu Spika, tatu, Serikali imeanza kufanya sensa ya utambuzi wa nyumba vijijini zenye hadhi angalau ya kudumu kwa miaka 15, nyumba zilizojengwa kwa udongo, saruji na kuezekwa kwa bati ili ziweze kulipa pango la nyumba. Pamoja na lengo zuri la Serikali la kudhibiti mapato lakini malalamiko yaliyopo kwa wananchi wa kipato kidogo ni namna watakavyopata fedha za kulipia pango kwa kuwa wapo baadhi yao wamejengewa nyumba hizo na watoto wao au ndugu zao. Lakini wapo wanaolalamika kwa kuwa walijenga nyumba hizo kipindi bei ya zao la korosho ikiwa nzuri, lakini kwa hali iliyopo sasa wanapata wakati mgumu ni namna gani watakwenda kulipia pango hilo katika mazingira ya sasa ambapo bei ya mazao haijatulia.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwenye kifungu 2011 - Ofisi ya Ardhi Mtwara ilijiwekea mpango wa kutoa elimu kwa umma kuhusu sheria mbalimbali za ardhi katika Halmashauri tisa za mkoa huo kufikia Juni, 2021. Hadi kufikia Mei 15, 2021 Ofisi ya Ardhi Mkoa imefanikiwa kutoa elimu kwa Halamshauri za Masasi, Nanyamba na Nanyumbu pekee huku muda uliobaki ni mwezi mmoja tu. Je, ni nini kimekwamisha zoezi hilo kusuasua ukizingatia kuwa muda wa mpango umebaki mwezi mmoja tu? Je, upo uwezekano wa Ofisi ya Ardhi Mkoa kumaliza zoezi la utoaji wa elimu katika mwaka huu wa fedha wa 2021/2022?