Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi

Hon. Eng. Stella Martin Manyanya

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Nyasa

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi

MHE. ENG. STELLA M. MANYANYA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kunipa hii nafasi ambayo kwa kweli nilikuwa nimeshakata tamaa kwa ajili ya muda, lakini nashukuru sana kwa nafasi hii.

Mheshimiwa Naibu Spika, nami pamoja na wenzangu kama walivyotangulia, nianzie kwa kumshukuru Mungu na pia niwapongeze sana Mheshimiwa Waziri Lukuvi pamoja na Naibu wake Mheshimiwa Dkt. Mabula na Katibu Mkuu, Mheshimiwa Mary Matondo ambaye tulikuwa naye kwenye Bunge la Katiba, alisaidia sana katika rasimu ile ya Katiba; vilevile Naibu Katibu Mkuu, ndugu yetu Nicolaus Mkapa pamoja na timu yao yote ambayo inawasaidia katika ngazi mbalimbali za kiutendaji.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba niongelee zaidi kuhusu gharama za kuhaulisha ardhi. Suala hili nililizungumza pia kupitia swali langu ambalo niliuliza hapa Bungeni na likapata majibu tarehe 9 Aprili, 2021 na lilikuwa swali Na. 329. Nashukuru sana kwa majibu ambayo nilipewa wakati huo, kwa hiyo, niko katika mwendelezo wa kuendelea kutetea juu ya jambo hilo.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuna changamoto kubwa sana. Pamoja na kazi kubwa inayofanywa vizuri na Wizara hii, lakini changamoto ya kodi zinazotozwa katika kuhaulisha ardhi, zinafanya kuwe na kikwazo cha watu kuhaulisha ardhi zao au mali wanazokuwa wamezipa, matokea yake wanabaki kuwa na mitaji ambayo ni mfu. Kwa sababu unapokuwa na ardhi uliyonunua, lakini iko kwenye jina la mtu na unashindwa kuihaulisha aidha kwa sababu umekosa fedha za kufanyia hivyo, basi inakufanya uwe na kitu ambacho siku yoyote yule ambaye alikuuzia akigundua pengine hujabadilisha, anaweza akaja kukudai kwamba hii bado ni mali yangu.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwenye majibu nilifahamishwa kwamba kuna ada ya upekuzi 40,000, pia kuna asilimia 0.02 ambayo ni ada ya uthamini wa hiyo mali inayokuwa imepatikana. Ada ya taarifa shilingi 40,000; ada ya kibali shilingi 80,000/=; na ada ya usajili 1% ya thamani ya hiyo mali. Baada ya kulipa hizo, kuna kodi sasa ambayo inalipwa TRA, asilimia 10 ya thamani ya mali uliyoipata.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa haraka tunaweza tukaona ni jambo la kawaida. Ukisema kwamba unaponunua, basi tenga na fedha ya kulipa hayo yote, lakini siyo rahisi kiasi hicho. Tukumbuke kwamba wakati mwingine mtu anauza kitu chake siyo kwa sababu alitaka kuuza, bali ni kutokana na shida aliyonayo au changamoto fulani inayomkabili. Kwa hiyo, anaweza kuuza hata kwa bei ambayo ni ya chini isiyotarajiwa, sawa na minada inavyofanyika. Hata hivyo unakuta kwa yule aliyenunua, akitaka kuhaulisha, huyu mthamini au mpekuzi anapoenda atatoa thamani inayodaiwa inalingana na hali ya sasa.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuna mzee mmoja nilimkuta akilalamika anasema kwamba ameambiwa thamani ya eneo kwa mfano la hapa maeneo ya St. Gasper ni takribani shilingi 80,000/= kwa square mita. Sasa unakuta katika kile kiwanja chake kidogo kilikuwa kinafikia karibu shilingi milioni 80. Mpaka akasema basi, nipeni mimi hiyo shilingi milioni 80 ili niwaachie hicho kiwanja. Kwenda kulipa asilimia 10 ya huo mtaji ambao anasema kwamba ameupata, inakuwa ni gharama ambayo mtu hawezi.

Mheshimiwa Naibu Spika, vilevile siku za nyuma elimu haikutolea kiasi cha kutosha. Unakuta mtu labda pengine mstaafu alinunua kiwanja chake kutoka kwa mtu ambaye wakati huo tuseme alikinunua kwa shilingi milioni moja na baada ya kukinunua, akakaa akapata kiinua mgongo chake akajenga, anasema nikabalishe, anaambiwa ahaa, sasa pamoja na hiyo nyumba uliyojenga, pamoja na hicho kiwanja, sasa gharama imeshakuwa shilingi milioni 150, ulipe asilimia 10 ya huo mtaji uliokaa hapo.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, unakuta ni mambo ambayo ni kweli kwa mujibu wa Sheria ya Kodi yako sawa, lakini nadhani ni vema tukayaangilia upya hasa kwa hawa wananchi wanyonge ili na wenyewe waweze kumiliki mitaji yao kihalali. Hata kwenye jibu la Mheshimiwa Waziri wakati ananijibu, alisema katika sehemu kubwa inayopewa malalamiko ni hiyo ya capital gain, yaani mtaji uliopatikana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, hatusemi kwamba hatujui athari yake kimapato, tunajua, lakini sasa hayo mapato hayakusanywi vizuri, kwa sababu hawa watu wanashindwa kuweza kulipa hizo gharama na matokea yake sasa hata kama anataka kukopa, anakopa vipi ili aweze kuwekeza wakati huo mtaji uko kwa jina la mtu mwingine?

Mheshimiwa Naibu Spika, hili suala ni muhimu na kwa sababu nilijibiwa siku ile kwamba watazungumza na Wizara ya Fedha ili kuweza kupata namna bora zaidi ya kulishughulikia ikiwezekana, sasa nimeangalia kwenye taarifa yao sijaona mahali palipozungumziwa suala hili. Ndiyo maana nikaona kwamba nilikumbushe tena kwamba kuna changamoto kubwa, watu wengi wana viwanja, wana mashamba, wana majengo yako kwenye hayo mashamba, lakini yanasomeka kwa jina lingine.

Mheshimiwa Naibu Spika, bahati mbaya hiyo sasa inatokana na nini? Hata ukitaka kufuatilia, unaweza kukuta hata anuani iliyopo pale ni ya mtu mwingine matokeo yake sasa hata kufuatilia masuala ya mapato kwa ujumla wake inakuwa ni shida. Naomba kama tulivyofanya hayo katika masuala mengine, mfano magari wakati ule yalivyokuwa na kero za kodi zile tukafanikiwa, basi na hili tuliangalie hasa kwa hawa wananchi wanyonge wale ambao wanahitaji kuwekeza, wanaohitaji nao wapate mtaji ambao ni halali kupitia hizi mali za rasilimali ya ardhi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo lingine nilikuwa naungana na wenzangu katika suala la Mabaraza ya Ardhi. Katika baadhi ya maeneo hilo suala bado ni tatizo, kwa sababu wale wazee wanaendelea kushughulikia mabaraza hayo unakuta wengine ni ndugu zao, wengine ndio anakuwa mtu ambaye sio ndugu yake. Kuna wakati unakuta wao wenyewe wanakuwa ni sehemu ya mgogoro.

Mheshimiwa Naibu Spika, mimi binafsi kwenye Kijiji cha Kata ya Kihagana, pale Tumbi na Kihagana, nina migogoro iliyodumu zaidi ya miaka nane, mtu anatoka hapo kwenye Baraza la Kata anaambiwa wewe ndio umeshinda, wakienda Wilayani huyu ndio kashinda; wanaenda Mkoani wanarudi. Mwingine anaanza tena upya kutaka rufaa.

Mheshimiwa Naibu Spika, nitaomba pia Mheshimiwa Waziri katika ziara zake za Mkoa wa Ruvuma atusaidie kumaliza pia hii changamoto ya kesi hizi; ya kwanza ni ya Bwana Mateso na Binti mmoja Nombo, pia kuna ya akina Ndiu na ya tatu niliisahau ya Mama Lambo, zimedumu muda mrefu, ni kero. Yaani ukifika pale, Mbunge kazi yako ndiyo hiyo. Ukiongea na huyu, anakwambia wewe unataka kumsaidia fulani. Naomba kwa kweli Mabaraza ya Ardhi sasa hivi wasomi ni wengi, kwa nini tusiyaweke sasa yakawa katika sura bora zaidi kuliko iliyopo sasa hivi? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nilikuwa naomba pia nizungumzie suala la mgogoro wa Lipalamba, naomba pia kwenye Hifadhi ya Lipalamba ule mgogoro bado unafukuta.

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya maneno hayo, nakushukuru sana. Ahsante sana, naunga mkono hoja. (Makofi)