Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi

Hon. Samweli Xaday Hhayuma

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Hanang'

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi

MHE. SAMWELI X. HHAYUMA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. Awali ya yote nichukue nafasi hii kumpongeza Mheshimiwa Waziri, Naibu Waziri na wataalamu wote wa Wizara ya Ardhi kwa kazi nzuri wanayoifanya. Kwa kweli Mheshimiwa Waziri toka amepewa jukumu la kuiongoza Wizara ya Ardhi, Wizara ya Ardhi imekuwa na utulivu mkubwa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya maelezo haya nitaongelea mambo kama matatu kama muda utaniruhusu. La kwanza ni suala la upimaji wa ardhi ambao wenzangu pia wameongelea kwa kina kwenye eneo hili, hasa kwa maeneo yetu ya vijijini unakuta miji yetu inaanza kuwa vijiji baadaye inaanza kuwa miji na kwenye maeneo hayo unakuta watu wamepimiwa maeneo makubwa kiasi cha ekari moja. Wanapoanza sasa kwenye kuzipima, unaambiwa kwamba ikipimwa ekari moja kuwa eneo la makazi inakuwa ni ngumu, mpaka ugawe maeneo kadhaa ili viwanja viweze kutambulika kwa mujibu wa sheria.

Mheshimiwa Naibu Spika, ninachoomba tu, wananchi hao wapewe elimu ya kutosha wakati wa upimaji huu ili waweze kuelewa na kweli wananchi wetu wa vijijini wana changamoto kubwa ya hofu ya Maafisa wanaotoka wilayani. Washirikishwe vizuri, waelezwe wanapata manufaa gani baada ya kufanya upimaji huo? Unaambiwa kwamba ukipima eneo moja, ni kiasi fulani cha fedha, lakini viwanja vile vinavyoongezeka gharama pia inaongezeka. Sasa wananchi wanapaswa kuelezwa kwamba gharama zile zinapoongezeka, wao wanapata manufaa gani?

Mheshimiwa Naibu Spika, wakati mwingine kwa sababu ya uhaba wa wataalam, Wizara imekuja na ubunifu ambao ni mzuri sana wa kushirikisha kampuni binafsi. Hizi kampuni binafsi zina mtazamo wa kunufaika. Sasa ukiangalia mahitaji ya wananchi wa vijijini; hawana fedha. Tuangalie namna ya kuwezesha ili hawa wananchi waweze kupimiwa ardhi yao bila gharama kubwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, kama nilivyowahi kuchangia kwenye Bunge hili, eneo la ardhi tukipima ardhi yote kwa kasi, tunaweza kupata mapato kwenye eneo la ardhi. Ninaomba sana Wizara iwekeze kwenye eneo la kupeleka wataalamu wa kutosha wa ardhi kwenye wilaya zetu. Wapeleke pia na vifaa vya kutosha. Kuna changamoto kubwa ya kwenye eneo hilo.

Mheshimiwa Naibu Spika, tuna upungufu mkubwa wa wataalam hasa baada ya kuanzishwa kwenye Ofisi hizi za Kanda, Ofisi za Mikoa; za mikoa zimewezeshwa vizuri na kama Mheshimiwa Nape alivyosema, wilaya nazo ziwezeshwe ili ardhi iweze kupimwa. Hii itasaidia kuondoa migogoro ya ardhi inayojitokeza mara kwa mara. Wataalam wapewe vifaa kwa sababu kwa sasa hivi vifaa viko mikoani. Ili tuweze kupata huduma, maana yake tuzunguke kwenye wilaya zote za mkoa, mpaka afanye booking sisi huku kuna migogoro vijiji na vijiji kwenda kuitatua, ni kalenda ndefu. Mtusaidie tupate vifaa vya kutosha vya upimaji wa ardhi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, niongelee pia eneo la Mabaraza ya Ardhi, wenzangu wameongelea sana, nami nikazie hapo. Kwenye Mabaraza ya Ardhi yale ya Kata, tujaribu kuona namna ya kuyaboresha, yana changamoto kubwa ya kiutendaji kwa sababu hayawezeshwi vizuri. Mabaraza haya pia wale wanaofanya maamuzi wanapaswa wapewe elimu nzuri ili angalau waamue kwa mujibu wa taratibu na sheria. Kwenye taratibu hizi za kuamua kesi kwenye Mabaraza ya Kata, linapofika suala la kwenda kutembelea eneo, hapo sasa zinaanza dalili ya kuanza kupata changamoto, kwa sababu unatakiwa kila upande uchangie kiasi ili waweze kufika kwenye site. Maana yake yule ambaye ana nguvu, ndiye atakayeangaliwa na yule ambaye hana uwezo, maana yake hataweza kuchangia hizo gharama za kwenda kwenye site. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa hili eneo tuliangalie vizuri namna ya kuratibu haya mabaraza kwa sababu wakiamua, ndiyo maamuzi yao; kama kuna rufaa, yanaenda kwenye Mabaraza ya Ardhi ya Wilaya. Ukija kwenye Baraza la Ardhi, Mabaraza haya ya Wilaya ambayo yako chini ya Wizara yako Mheshimiwa Waziri, hapa tuna changamoto kubwa, Wabunge wengi wanalalamika kwenye maeneo yao, hakuna Mabaraza ya Ardhi. Mfano tu mimi Jimbo langu la Hanang; Wilaya ya Hanang hatuna Baraza la Ardhi, tunategemea Baraza la Ardhi la Babati, nalo kwa muda mrefu halina Mwenyekiti. Jinsi Wilaya ya Hanang ilivyo, kuna wananchi wanatoka kilometa zaidi ya 100 kufika tu Makao Makuu ya Wilaya.

Mheshimiwa Naibu Spika, kutoka Katesh Mjini ambayo ni Makao Makuu ya Wilaya, kilometa 70 mpaka Babati. Ukienda babati unakuta Mwenyekiti hayupo, wala udhuru huo haujatolewa kabla. Yawezekana ni siku ambapo kesi hiyo inatakiwa itolewe Ushahidi, anakuja na watu wanne au watano ambao ni mashahidi, kilometa zaidi ya 170. Gharama za kuwaleta hao watu, nauli tu ni zaidi ya shilingi 75,000/=. Anafika na watu hao anaambiwa kesi imeahirishwa kwa sababu Mwenyekiti hayupo. Baada ya hapo, itaahirishwa tena na wala hataambiwa kwamba Mwenyekiti atapatikana wakati gani?

Mheshimiwa Naibu Spika, huo ni usumbufu mkubwa kwa wananchi, tuwe na Baraza la Ardhi la Wilaya ya Hanang. Tulishatoa majengo, tupate Mwenyekiti na lile baraza lianzishwe ili kuondoa kero ambayo tunaipata kwa sasa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nigusie kidogo kwenye haya mashamba makubwa ambayo tumewapa wawekezaji. Sisi tuna mashamba tumempa mwekezaji ambayo zamani yalikuwa ya NAFCO, yalilimwa na tulikuwa tunapata ngano yakutosha. Baada ya kuwa yule mwekezaji wa awali amejitoa kwenye kilimo cha ngano, mashamba yale tukampa mwekezaji mpya. Ni zaidi ya miaka 12 sasa hivi hakuna chochote kinachoendelea.

Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Waziri wa Kilimo ameenda ameona na Wizara ya Kilimo imesema kwamba wameshajadiliana naye, wamekubaliana ndani ya mwaka mmoja, kama hatakuwa na chochote anachokifanya basi yale mashamba yaweze kutwaliwa, yarudi Serikalini na tuangalie namna ya kuwapatia watu wengine ambao watazalisha kwa tija.

Mheshimiwa Naibu Spika, namwomba Mheshimiwa Waziri, wakati tutakapokuja atusaidie kwenye eneo hili. Imekuwa kwa mwaka huu amelima ekari 3,000 kati ya ekari ya 47,000. Sasa hii ni kama hujuma tu kwa sababu hatuzalishi, sisi Halmashauri hatupati chochote, wananchi wetu hawapati chochote. Tunaomba ukishaileta hili utusaidie. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema haya ninaamini, Mheshimiwa Waziri atakuwa na majibu ya kina juu ya taabu hii wanayopata wananchi wangu kwenye eneo la Mabaraza la Ardhi. Kama sitapata ufafanuzi wa kina, nafakiri tumeshajaribu kuongea hili suala kwa sababu ni kero kubwa kwa wananchi wangu, nitamshikia shilingi yake. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema hayo, naomba kuwasilisha. (Makofi)