Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi

Hon. Nicodemas Henry Maganga

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mbogwe

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi

MHE. NICODEMAS H. MAGANGA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Awali ya yote napenda nimshukuru Mwenyezi Mungu kwa siku ya leo tena kuweza kupata fursa hii ya kuweza kuchangia Wizara hii ya Ardhi. Mimi ni Mbunge wa Mbogwe. Jimbo la Mbogwe ni Wilaya mpya. Nitumie nafasi hii kumshauri mtani wangu, Mheshimiwa Waziri Lukuvi pamoja na Naibu Waziri, dada yangu Mheshimiwa Angeline Mabula.

Mheshimiwa Naibu Spika, michango mingi wenzangu wameigusia, mimi naomba kutumia muda vizuri ku-focus kwenye nafasi ambazo ni za muhimu zinazowakabili wananchi wa Tanzania hasa wa Mbogwe. Lipo jambo moja Mheshimiwa Waziri kwenye upande wa hizi taasisi, kwa maana ya Makanisa pamoja na Misikiti, pale ninapotokea Mbogwe, kuna migogoro mingi sana maeneo yale ya taasisi. Nianze kwa kukueleza Mheshimiwa Waziri, kwa kuwa Jimbo la Mbogwe ni Wilaya mpya kwanza sina Baraza la Wilaya. Naomba unisaidie sana jambo hilo na uiweke kwenye kumbukumbu zako ili usisahau mtani wangu, itakuwa hakuna nilichokifanya katika mchango wangu.

Mheshimiwa Naibu Spika, nilikusikiliza wakati unatoa hotuba Mheshimiwa Waziri, kiukweli bila unafiki, nimeridhishwa na maelezo yako. Japokuwa sasa nami nimepata hii nafasi ya kukushauri leo mbele ya Bunge hili Tukufu, uniruhusu tu nigusie kidogo ili kusudi pale panapowezekana nawe uweze kujipanga ili kusudi Taifa letu tuweze kusafiri vizuri na tuweze kufika salama safari yetu ya kuelekea 2025.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nasikitika kwa kuanza kumpa Mheshimiwa Waziri shutuma ya sekta yake. Toka niapishwe kuwa Mbunge, kwenye ofisi zangu migogoro mingi ni ya ardhi. Nilipomaliza kuapishwa tu pale, niliporudi nyumbani, nilikutana na watu hawa wa Msikiti wa Masumbwe Mjini, walikuwa na kesi, tayari ilikuwa Mahakamani na baadaye hiyo kesi ikahukumiwa kwamba walipe shilingi milioni 70. Wazee wangu hawa wamekuwa wakilalamika sana, maana Serikali ni moja tunayoiongoza na mpaka sasa hivi hawana uwezo wa kulipa hiyo hela.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, nitumie nafasi hii kuiomba tu Serikali iangalie upya hilo suala, pamoja na kwamba kesi zilishafika Mahakamani, lakini hawa watu hawana uwezo wa kulipa hayo madeni ya nyuma. Kwa hiyo, nakuomba wewe pamoja na Mheshimiwa Rais wa Awamu ya Sita, mwone namna gani mnaweza kuwasaidia watu wenye misikiti na makanisa ili kusudi waendelee kumwabudu Mungu katika roho na kweli pasipo na pressure za madeni. Maana kila Kanisa ukiingia sasa hivi, michango mingi utaambiwa Serikali inatudai na ukiangalia kiuhalisia, hawana uwezo wa kuyalipa hayo madeni.

Mheshimiwa Naibu Spika, namwomba Mheshimiwa Waziri, likiisha hili Bunge, afike Mbogwe; maana kwa kuwa Mbogwe kwanza haina Baraza, halafu ni Wilaya mpya ambayo GN yake ilitoka mwaka 2019; kwanza kuna uhaba wa watumishi kwenye sekta yake. Nafahamu Serikali ya Awamu ya Tano tulikuwa tukipigania kuhusu maendeleo na kiukweli huwezi ukapata maendeleo bila kuwa na hati (document) ya kuweza kukufanya ukakopa hata benki.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kuwa Mbogwe sasa inakuwa kwa kasi na ni Wilaya inayojitambua ina Mbunge kijana halafu makini, anazijua biashara vizuri, namwomba Waziri pamoja na Naibu Waziri wa Ardhi dada yangu, wafike Mbogwe waangalie Mji wa Mbogwe jinsi ulivyo, ni mzuri. Mbogwe sisi tuna madini lakini pia sisi ni wafugaji, kumekuwa na migogoro kati ya wafugaji na wakulima; wewe Waziri mtani wangu ndio mwenye kutoa maamuzi hayo ukifika. Kwanza ukifika tu wakakuona, wataona kama vile ameshuka Yesu hapa, watakuwa na imani hata wale watumishi wa shetani walioko kwenye Wizara yako ambao wanatumia utapeli kuwatapeli wananchi na kuwapora ardhi yao watakuogopa na wananchi wale watapata haki zao za msingi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, upo mgogoro mwingine ambao nimekuwa nikiuzungumza kwenye mikutano yangu karibia kote. Kuna mashamba haya ya dhahabu, Wilaya yangu ina migodi karibia 22, lakini ukiangalia kila palipo na dhahabu kuna migogoro ya ardhi na kiuhalisia migogoro ya ardhi ya mashamba ya dhahabu haiwezi kutatuliwa na sekta ya madini, maana kila sekta inajitosheleza.

Mheshimiwa Naibu Spika, japokuwa yale maeneo hayajapimwa, kwa busara ya Mheshimiwa Waziri na heshima ambayo umenipa kwanza toka unipokee hapa Bungeni, ukifika utaona jinsi gani unaweza kuitatua hiyo migogoro ili watu waweze kupata zile asilimia na haki zao wenye mashamba yale yaliyojaliwa na Mwenyezi Mungu kupata dhahabu.

Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Waziri wa Ardhi pamoja na Naibu, jambo lingine kuna Kata moja inaitwa Bukandwe Kijiji cha Kanegele Kambarage, pale na penyewe kuna mgogoro wa mbuga nzuri ambayo ina rutuba na inatoa mpunga mzuri sana. Ukifika na penyewe utaona jinsi gani uweze kunisaidia, kuna heka karibia 145 ambazo wamekuwa wananchi wakizigombania pamoja na kampuni moja ambayo jina nimelisahau, nitakwambia nikitoka hapa Bungeni ili kusudi uweze kunisaidia Mheshimiwa Waziri.

Mheshimiwa Naibu Spika, ipo changamoto nyingine. Kuna Sekondari ya Kata yangu ya Burugala, Sekondari ilijengwa, lakini wananchi wanavyodai ni kwamba hawajapewa chochote na Serikali. Hivyo sasa, kwa kuwa sekta hii ni yako Mheshimiwa na mtani wangu, tukifika huko mambo hayo nina imani utayamaliza tu.

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo lingine, Mji wa Mbogwe una kata karibia saba ambazo zimeendelea sana; ukinipa wataalamu wazuri waaminifu, maana mimi katika maisha yangu huwa napigania sana kupata watu waaminifu wa kufanya nao kazi; na ninakumbuka mchango wangu wa kwanza wakati naingia hapa Bungeni, niliishauri Serikali ya Awamu ya Tano kwamba sasa kwa kuwa Serikali imeanza upya; na sisi darasa la saba tupo na tupo wengi tunapiga sana kura, tena kwa uaminifu, huwa tunashinda kwenye misitari, msitubague. Mteue Wakurugenzi hata Darasa la Saba, maana kazi ya Ukurugenzi siyo kazi sana na hakuna kazi rahisi kama kuwa Mkurugenzi. Maana watendaji wapo tu wale Wakuu wa Idara, Wakuu unawaamrisha tu kwamba fanya hiki na hiki. (Kicheko/Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa maana hiyo sasa, leo hii Awamu ya Sita nitumie nafasi hii tena kurudia maneno yale niliyoyazungumza mwanzoni. Kwa kuwa najua uteuzi naendelea, tupewe nafasi watu wa Darasa la Saba ambao hatuna CV nyingi sana, ila tuna sifa ya uaminifu, ili twende tukazisimamie Halmashauri. (Kicheko/Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nchi yetu iko kwenye vita ya uchumi, hatuwezi tukaweka michango kwa kukupongeza tu, lazima mzee ukae attention. Kwanza unatakiwa ubadilike, sura yako ni nzuri mno Mheshimiwa Waziri, wakati mwingine na watendaji wako wanakudharau. Wewe una nia nzuri, huwa nakuangalia sana mambo yako, una nia nzuri sana ya kuweza kuliletea mabadiliko hili Taifa, lakini waliomo ndani ya sekta yako hawana mapenzi mema na nchi hii na wala na wewe.

Mheshimiwa Naibu Spika, mimi niko Dodoma hapa leo mwezi wa Saba. Jana niliongea na wewe Waziri, wakati naingia hapa Dodoma, mimi niliingia kwa kutafuta maeneo yale hot cake, kuna maeneo mengi tu yenye uwazi ambayo yalikuwa yanaonekana, kama unavyofahamu Mheshimiwa Waziri sisi Wasukuma kwa kuwa tuna roho nzuri sana, ni wepesi wa kuwaamini watu. Baada ya kujaribu kuchukua yale maeneo, tumeingia migogoro ambayo yaani haiwezi ikaisha leo wala kesho. Ufafanuzi ulionipa, nami kwa kuwa ni mwelewa halafu ni senior, nimeshaelewa ni nini cha kufanya ili kusudi hela yangu isipotee. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Waziri nikuombe sana, kwa kuwa tuko kwenye vita ya uchumi, badilika uwe mkali kidogo pamoja na Naibu Waziri ili kusudi wakuogope wale watendaji wako, watu waweze kupata haki zao kwa wakati muafaka. Leo Mheshimiwa Waziri utaona watu wengi wanakupongeza, kila mtu anasimama anakupongeza, lakini siku ukikosa haya madaraka, utakuja kuniambia, siku moja Maganga uliongea Bungeni. Hao hao ambao walikuwa wanakupongeza, watakugeuka na kukuona yaani hufai na hukutumia vizuri mamlaka yako wakati ukiwa Waziri. (Makofi)

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MHE. NICODEMAS H. MAGANGA: Mheshimiwa Naibu Spika, kwa maana hiyo, Mheshimiwa Waziri nakuomba sana utembelee kwenye Jimbo langu la Mbogwe maana wewe ardhi zote ni za kwako; na kuna mapori mengi ambayo yalishamaliza kwanza kuwa na sifa ya kuwa maporiā€¦

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa kengele ya pili imegonga, nikawa nasubiri umalizie sentensi, naona mambo mazito unaendelea kumwaga hapo. Ahsante sana.

MHE. NICODEMAS H. MAGANGA: Mheshimiwa Naibu Spika, haya nakushukuru. Basi mchango wangu mwingine nitamwandikia Waziri ili auone, maana nimeshauandaa hapa ninao.

Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana, nashukuru. (Makofi)