Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi

Hon. Nape Moses Nnauye

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mtama

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi

MHE. NAPE M. NNAUYE: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi nami nichangie kidogo kwenye hotuba hii ya bajeti ya Wizara ya Ardhi na nianze kwa kumpongeza Waziri na Naibu Waziri na timu yake nzima kwa kazi nzuri wanayoifanya kwenye Wizara hii. Kama wenzangu waliotangulia wavyolisema, Wizara hii mwanzoni ilikuwa na kelele nyingi sana, lakini Mheshimiwa Lukuvi kwa uzoefu wake nadhani ameweza kuituliza, kelele zimepungua, hata kama bado yapo mambo machache lakini kwa kweli mnyonge mnyongeni lakini haki yake mpeni, amefanya kazi nzuri sana. Hongera sana Mheshimiwa Waziri. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pia Bunge la Kumi na Moja mimi kwa niaba ya wananchi wa Jimbo la Mtama tulileta mapendekezo Serikalini ya kufuta shamba Na. 37ambalo lipo Maumbika Jimboni Mtama ambalo lilikuwa na hati Na. 5,438; shamba hili tuliliomba kwa muda mwanzoni, hati yake ikafutwa, baada ya muda ikabatilishwa ufuataji wake, sasa kwa niaba ya wananchi wa Mtama nimesimama kumshukuru.

Mheshimiwa Waziri Lukuvi kwa sababu baada ya mjadala naye Serikali imechukua uamuzi wa kulichukua hili shamba na kuwakabidhi Halmashauri ya Mtama.

Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Waziri na Serikali nawashukuru sana na usikivu wenu na wananchi wa Mtama wanashukuru kwa uamuzi huu wa kulirudisha shamba hili sasa lisimamiwe na Halmashauri mpya ya Mtama. Nikuhakikishe kwamba tumeanza utaratibu wa kupanga matumizi bora ya eneo hili na hivi karibuni tutakamilisha utaratibu wa mapendekezo yetu na tutayaleta Wizarani kwa ajili ya kuidhinishwa. Ni matumaini yangu kwamba kelele za watu wachache hazitawarudisha nyuma tena. Mmeshatukabidhi, msirudi nyuma. Mwanzoni mlirudi nyuma, ikatusumbua sana.

Mheshimiwa Niabu Spika, safari hii msirudi nyuma tena, tupo katika mchakato wa kupanga matumizi na tupo katika hatua ya mwisho kabisa. Kwa hiyo, Mheshimiwa Waziri nakuomba ulinde uamuzi wako ili tupate kupaendeleza mahali hapa kwa matumizi ya wananchi.

Mheshimiwa Naibu Spika, naipongeza pia Wizara hii kwa kuhamisha huduma zilizokuwa zinatolewa kwenye kanda kuzipeleka mkoani. Jambo hili limetupunguzia sana gharama wananchi, lakini naomba nitoe mapendekezo, kama mmeweza kutoka kwenye kanda kwenda mkoani, mnaweza pia kutoka mkoani kwenda wilayani.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, umefika wakati baada ya kufanya kazi kwenye kanda na mkaona usumbufu ambao ulikuwepo na bila shaka mtaona tija iliyopatikana baada ya kuzitoa huduma za kwenye kanda kuzipeleka kwenye mkoa. Sasa Mheshimiwa Waziri nadhani twende zaidi, tuzitoe hata kama kwa kuanzia baadhi ya huduma na hasa huduma kama za upatikanaji wa hati hizi. Upatikanaji wa baadhi ya vitu tuutoe kwenye mkoa tuupeleke kwenye wilaya. Tutakuwa tumewasogelea sana watu na tutapunguza sana gharama.

Mheshimiwa Naibu Spika, Mkoa kama wa Lindi bado ni mbali sana mtu kutoka Liwale kuja Lindi Mjini kuchukua huduma. Kwa hiyo, ni mapendekezo yangu kwamba kwa kuwa tumefanikiwa kupeleka kwenye Mkoa na umeona inafanya vizuri; na katika dunia hii ambayo Sayansi na Teknolojia imekua sana, tunaweza bado tuka-control kutoka mkoani lakini bado huduma fulani wasilazimike kusafiri kuzifuata mkoani, bali waende wakazichukue Wilayani. Hayo ni mapendekezo yangu, nami naamini kwa uzoefu wenu na uwezo wenu mnaweza mkalifanya hilo na tukasogeza huduma karibu na wananchi wetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, suala la mwisho nililotaka kulizungumzia ni suala la upimaji na upangaji wa miji yetu. Nimeona kwenye Kamati na nichukue nafasi hii kuipongeza iliyokuwa Kamati yangu ya zamani ya Ardhi wameliona hili jambo la utengaji wa fedha na kuzikopesha Halmashauri zetu zipime zenyewe. Jambo zuri lililofanyika hapa, mnawapa kwa zero interest, nadhani hili jambo ni zuri sana na bila shaka Serikali wameona, kwamba hii fedha wakipeleka, hata kwa hizi chache walizoanza nazo, wakifanikiwa kupima na kumilikisha, tayari ni mradi mzuri wa kuiingizia Serikali mapato.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa mapendekezo yangu; la kwanza, naiomba Serikali iongeze fedha, hizi Wilaya ni kidogo sana, ikiwezekana tu- roll hata nchi nzima kwa sababu itaongeza mapato kwa kiwango kikubwa sana. Kwa hiyo, eneo la kwanza fedha iongezwe. Eneo la pili Mheshimiwa Waziri nilikuwa napendekeza, kwa kuwa kasi ya ukuaji wa miji ni mkubwa, badala ya kwenda kwenye urasimishaji na bila shaka Waziri wa Fedha yupo na amenisikia, hili ni eneo zuri litatupatia fedha ya bure sana. Wape fedha ya kutosha waongeze Wilaya. Sasa pendekezo la pili miji inakua kwa kasi kuna mradi wa kurasimisha urasimishaji una matatizo yake kwa sababu unakuta watu wameshajipanga mnaanza kurasimisha inachukua muda na ni gharama.

Mheshimiwa Naibu Spika, mapendekezo yangu ilikuwa kipaumbele cha hizi fedha pelekeni kwenye Halmashauri mpya ambazo miji yake ndiyo inaanza kukua na hapa naomba upendeleo mkubwa kwa Halmashauri yangu ya Mtama. Naomba tuletewe fedha, Halmashauri bado ni mpya, hatujatawanyika sana. Tukiletewa fedha, tutapima na kupanga vizuri bila gharama na tutajikuta tuna miji mizuri ya kisasa.

Mheshimiwa Naibu Spika, hapa namwomba Mheshimiwa Waziri jambo mahsusi, Mji wa Mtama wakati Mheshimiwa Hayati Dkt. Rais Magufuli anaamua kutupa Halmashauri, ule mji umepanuka. Bahati mbaya wakati wa kupanuka kuna mahali wakapanuka mji ukaenda ukachukua eneo la Tandahimba, nasi tukadhani ni eneo la Mtama. Wakati wa kupima sasa vipimo kuleta kutangaza GN ya Mji wa Mtama, tukakuta lile eneo ambalo wananchi wanapata huduma Mtama, tunajua ni wananchi wa Mtama miaka yote, tukajikuta wanawekwa nje. Karibia theluthi moja ya Mji wa Mtama ipo nje ya Mtama na ipo nje ya Mkoa wa Lindi.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa nilikuwa naomba Mheshimiwa Waziri ikiwezekana basi tuma watu wako waje waliangalie tatizo hili na kwa sababu limevuka suala la Jimbo, limevuka Wilaya, limeenda Mkoa, kwa hiyo, likotokea Wizarani itakuwa rahisi kulitatua. Watume watu wako waje waangalie, ikiwezekana tuone namna ya ku-accommodate. Kwa sababu wenzatu wa Tandahimba wala hawana shida, kwa sababu hili eneo wala hawakujua kama ni lao, isipokuwa GN ya miaka mingi inaonesha hili eneo lipo Tandahimba. Kwa hiyo, ombi langu Mheshimiwa Waziri tuma watu wako waje watusaidie.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, nashukuru kwa kazi nzuri iliyofanywa, lakini nawapongeza kwa kusogeza huduma mkoani, sasa zipelekeni wilayani. Napongeza kwa kutenga fedha za upimaji na kuwakopesha Halmashauri na ninawaomba wale wanaokopeshwa wasimamie fedha zirudi ili na wengine tukope. Hata hivyo Mheshimiwa Waziri nakuomba ukisimama, basi iingize Mtama nipate fedha kwa ajili ya kupima mji wangu mzuri.

Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi. Naunga Mkono hoja. (Makofi)