Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi

Hon. Michael Mwita Kembaki

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Tarime Mjini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi

MHE. MICHAEL M. KEMBAKI: Mheshimiwa Naibu Spika, nikushukuru kwa kunipa nafasi hii ili niweze kuchangia katika Wizara hii muhimu katika ustawi wa uchumi wa nchi yetu. Nianze kwa kumpongeza Waziri na Naibu Waziri na watumishi wote wa Wizara hii kwa kazi nzuri ambayo wanaifanya kuhakikisha kwamba, wanapunguza malalamiko na kero ambazo zinakabili Watanzania katika idara hii ya ardhi.

Mheshimiwa Naibu Spika, nianze kwa kusoma majukumu ya Wizara hii ambapo miongoni mwa majukumu hayo ni pamoja na kutatua migogoro ya ardhi na nyumba. Mengine ni kupima ardhi na kutayarisha ramani; kusimamia Shirika la Nyumba la Taifa, pamoja na mambo mengine. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nimeanza kwa kusema haya kwa sababu katika Jimbo letu la Tarime Mjini ipo migogoro ya ardhi ambayo imechukua muda mrefu. Miongoni mwa migogoro hii ya ardhi ni pamoja na ile ya Nyagesese, lakini pia ile ya Mlima Nkongore. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kama unavyojua, mtu akitaka akuondoe utu au akufanye uwe ombaomba ushindwe kutekeleza majukumu yako ipasavyo ni pale anapokunyima uhuru wa kumiliki ardhi. Unapokuwa huna ardhi maana yake utakuwa mhamiaji, utakuwa kibarua na vilevile utakuwa ombaomba. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, katika Jimbo letu la Tarime wapo wakazi zaidi ya kaya 10 ambao sasa hivi wanaishi maisha ya hofu, hawana shughuli za kufanya, wamekuwa vibarua katika mashamba ya wengine kwa sababu ardhi yao imechukuliwa. Ningependa nitaje hizi kaya 10 ambazo ardhi yao imechukuliwa na sasa hawafanyi shughuli zozote na wamebaki ombaomba katika ardhi ambayo wamezaliwa. Wamezaliwa pale, baba zao wamezaliwa pale na wameoa pale na sasa hivi wana wajukuu, lakini sasa hivi ardhi ile hawawezi kuimiliki kwa sababu imechukuliwa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kaya hizi ni pamoja na Kaya ya Girimu Aryuva Kisiri, Kaya ya Maro Muniko Kisiri, Mkami Marwa Mkami, Lewis Cosmas Mwita, Marwa Girima Ngendo, Marwa Kirumwa Mkirya, Nyamuhanga M. Nyasebe, Matiko Mturu, Rugumba G. Ngendo na Chacha Mukami George. Kaya hizi sasa hivi hazina sehemu ya kulima kwa sababu eneo lao limechukuliwa kwa kisingizio kwamba wanalinda Hifadhi ya Mlima Nkongole.

Mheshimiwa Naibu Spika, najiuliza, mwaka 2018 Kamati ya Ulinzi na Usalama ya Wilaya ilienda katika Mlima Nkongole na waling’oa bangi pale, baada ya kung’oa bangi wakaja kwamba wanalitaifisha lile eneo ili wasiendelee kulima bangi. Toka wakati huo, mwaka 2018 wananchi hawa ambao wanaishi katika Mlima Nkongole hawana sehemu ya kulima na walikuwa wanategemea kulima katika eneo lile.

Mheshimiwa Naibu Spika, vile vile miji yao wengine wamejenga nyumba pale nyumba za kudumu, miji yao beacon imewekwa kwamba sasa wanatakiwa wahame katika eneo lile.

Mheshimiwa Naibu Spika, ukweli ni kwamba vitu vingine vinaumiza moyo kwa sababu watu walikuwa wanaendelea na shughuli zao za kila siku, ghafla wanasimamishwa. Ninapozungumza sasa hivi kuna watu wawili wako ndani wamekamatwa kwa sababu wameonekana wakipita pale; na huyu ni Lugumba G. Ngendo. Kwa sababu jukumu la Wizara hii ni kutatua migogoro ya ardhi, ninamwomba Waziri, mimi ninakuaminia sana Mheshimiwa kwa uchapa kazi wako mzuri, naomba utatue tatizo hili la mlima Nkongole ili watu wale wapate haki waendelee kufanya shughuli zao za kila siku kama walivyokuwa wanaendelea hapo mwanzo.

Mheshimiwa Naibu Spika, niliuliza swali hili siku chache zilizopita na majibu niliyopewa hayakuridhisha kwa sababu niliambiwa kwamba Serikali ichukue eneo lile ili kulinda mazingira, lakini kigezo cha kulinda mazingira wananchi wale walikuwa wanalima, lakini waliopewa kulinda eneo lile, vile vile wanalima. Sasa najiuliza, kama walionyang’anywa eneo walikuwa wanalima na hawa waliopewa wanaendelea kulima: Je, ni nani sasa anatunza mazingira hapa?

Mheshimiwa Naibu Spika, ukiangalia katika maeneo mengi, kwa mfano ukienda Milima ya Uluguru utakuta watu wanaishi pale na ile milima kwanza ni chanzo cha maji lakini watu wanaendelea kuishi na wanaendelea kufanya shughuli zao kama kawaida; lakini ukija katika Mlima Nkongole, hata panya ukimtafuta humpati kwa sababu hakuna chochote ambacho unachoweza kuhifadhi pale.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba sana sana Mheshimiwa Waziri anaposimama kumalizia, tafadhali aje na majibu ya namna gani wananchi wa Nkongole watapata haki yako ya kuendelea kufanya shughuli zao za kila siku ili maisha yaendelee, wasiwe watumwa na wasiwe wahamiaji katika ardhi ya baba zao ambao wamezaliwa pale siku zote. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, vile vile napenda kuzungumzia nyumba za National Housing ambazo zipo katika Jimbo letu la Tarime Mjini. Kwa sababu majukumu ya Wizara ni kusimamia Shirika la Nyumba, ukienda katika nyumba zile za National Housing ni aibu sana, watu wanaziba mpaka na makaratasi ya nylon juu ili wasinyeshewe, wengine wanaweka mawe ili vile vigae visidondoke. Naomba Waziri tafadhali sana macho yako yafike pale katika nyumba zile za National Housing ili watu wale wapate kuishi mazingira rafiki kama ilivyo, lakini pia mapato ya Serikali yasipotee hivi hivi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema haya nakushukuru kwa kunipa nafasi, Mungu akubariki sana. (Makofi)