Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi

Hon. Francis Leonard Mtega

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mbarali

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi

MHE. FRANCIS L. MTEGA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi nami niweze kuchangia katika Wizara hii ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi. Nianze kwa kumshukuru na kumpongeza sana Mheshimiwa Waziri kwa kazi nzuri anayofanya, lakini nimpongeze sana Naibu Waziri, Katibu Mkuu na Watendaji wote wa Wizara kwa ujumla.

Mheshimiwa Naibu Spika, leo ningependa nichangie kuhusu migogoro ya ardhi na mipaka, hususan mipaka. Migogoro ya ardhi imekuwa mingi kwa nchi yetu kwa ujumla, lakini Mheshimiwa Lukuvi amekuwa hodari sana na mahiri kwa kuitatua, nampongeza sana. Hata Mbarali tulikuwa na mgogoro baina ya mwekezaji wa Kapunga na wananchi, lakini mwaka ule 2015 alikuja haraka sana na kuumaliza mgogoro ule. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kuna mgogoro mkubwa sana wa mipaka kati ya TANAPA na vijiji 55 katika Jimbo la Mbarali. Huu mgogoro kwa kweli ni mkubwa sana na una athari nyingi. Namwomba Mheshimiwa Waziri aupe kipaumbele kuutatua mgogoro huu, vinginevyo Wana-Mbarali hawatakuwa na amani na utulivu kabisa. Mpaka huu wa GN Namba 28 bahati mbaya sana umepita vijijini, mawe mengine yako katikati ya vijiji. Sasa wananchi wale wanaishi kwa matamko; atakuja kiongozi huyu anasema msiwe na wasiwasi, endeleeni na shughuli zenu kama kawaida, Serikali inafanyia kazi. Anakuja kiongozi mwingine anasema mko ndani ya hifadhi hamruhusiwi kufanya kitu chochote. Sasa hii inawapa shida wananchi wale, hawajui wafanye nini, kwa sababu, shughuli nyingi wanazifanya ndani ya maeneo yao wanayoishi.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa mfano, kuna mashamba mazuri kule Mnazi na mashamba yale yanatoa mpunga kwa wingi na tuna viwanda vikubwa pale Ubaruku vinachakata mpunga tena wa hali ya juu. Sasa kuwaambia wasifanye shughuli yoyote, maana yake ni kuwarudisha nyuma kiuchumi na kukosesha pato la Taifa. Kwenye Ilani imeainishwa kabisa kwamba tunaenda kuboresha kilimo na kuhakikisha wananchi hawa wanakuwa na kipato cha kutosha na vilevile Taifa linakuwa na akiba ya chakula. Sasa wanapozuiwa wasifanye shughuli zao za kila siku, kwa kweli hatuwatendei haki wananchi wale wa Mbarali.

Mheshimiwa Naibu Spika, pia kuna shughuli mbalimbali, kwa mfano kule Luhanga kuna ujenzi wa Shule ya Msingi na ujenzi wa Zahanati. Sasa kiongozi huyu anakuja anasema endeleeni na ujenzi msiwe na wasiwasi, kesho kiongozi mwingine anakuja kuzuia kwamba msifanye jambo lolote la kuendeleza kwa sababu mpo ndani ya hifadhi, subirini Serikali itoe maamuzi yake kwamba wapi kutakuwa ni mpaka ndipo mtakapoendeleza ujenzi. Sasa hii inawavunja moyo wananchi wale, wamepoteza nguvu zao na sasa hawaendelei na ujenzi.

Mheshimiwa Naibu Spika, tunamwomba Mheshimiwa Waziri, maamuzi ya Serikali yaharakishwe ili kubainisha mpaka sahihi ni upi? Yawezekana kuna vijiji vitaambiwa viondoke, yawezekana kuna vitongoji vitarekebishwa, sasa hii ingefanyika haraka ili wananchi wawe huru kufanya kazi zao za kila siku wajipatie kipato na vilevile waweze kuliongezea pato Taifa letu.

Mheshimiwa Naibu Spika, nije upande wa GPS. Zamani mipaka ilikuwa inawekwa mawe tu, kiasi kwamba wazee wanakuwepo ni mashuhuda kwamba mpaka ulikuwa hapa na viongozi wa eneo lile wanashuhudia, lakini sasa ni GPS. GPS hii ni wataalamu peke yao wanaoweza kutafsiri. Sasa naomba Waziri atakapojumuisha, atuambie ni nani ata-cross check kuona kwamba hawa wataalam wetu wanaotafsiri coordinates zile kuweka mawe, je, hawawezi wakawa wanaingia ndani zaidi au pengine kutoka nje zaidi? Kwa sababu, wananchi pale hawana utaalamu wowote, wao wakishaona jiwe limewekwa ni kulalamika tu kwamba, sisi mpaka tunajua ulikuwa kule, sisi mpaka haukuwa hapa.

Mheshimiwa Naibu Spika, hivyo tuna migogoro mingi sana kuhusu GPS katika tafsiri yake na mawe yanavyowekwa, wananchi hawawi na uhakika, wanakuwa na wasiwasi mkubwa sana. Kwa kweli, Mbarali tuna uhaba mkubwa sana wa ardhi, Mbarali tuna mifugo mingi, Mbarali tuna mashamba ya mpunga, Mbarali tuna hifadhi ya TANAPA; ile hifadhi ni kubwa mno kiasi kwamba eneo linalotumika kwa wanyama liko upande wake, lakini eneo la wananchi ambapo linaonekana ni oevu, kwa kweli ni kubwa mno na kwa sasa hivi ule u-oevu haupo. Nimezunguka sehemu nyingi ni vumbi tupu na mashamba, lakini Ihefu kwa kweli bado ni sehemu oevu na inahifadhiwa na wananchi hawaruhusiwi kwenda kule. Sehemu nyingine zote ni kavu, zina mashamba, hakuna uoevu, hakuna maji; maji yanapita tu mtoni, yanatoka Makete, pale ni mapito ya maji, wala hakuna madhara yoyote. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, namwomba Mheshimiwa Waziri, kwa kweli aende mwenyewe kule ashuhudie, aone haya mawe yaliyopandwa vijijini yanavyoathiri wananchi na kwamba, sehemu zile kwa kweli hazihusiani kabisa na uoevu unaoongelewa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi, naunga mkono hoja. Ahsante sana. (Makofi)