Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi

Hon. Aleksia Asia Kamguna

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi

MHE. ALEKSIA A. KAMGUNA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuweza kuchangia. Awali ya yote hatuna budi kumshukuru Mwenyezi Mungu ambaye ametuwezesha sote kuwa salama. Nawapongeza Wizara ya Ardhi, ukweli Wizara ya Ardhi ni kati ya Wizara ambazo zilikuwa na matatizo makubwa sana katika nchi hii lakini wamejitahidi. Hapa walipofikia si haba, wamefanya kazi kubwa sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, hata hivyo, panapokuwa na manufaa hapakosekani changamoto. Wizara hii pamoja na kujitahidi lakini kuna changamoto hususan za mipaka. Nazungumzia mipaka iliyopo katika Bonde la Kilombero, Wilaya ya Malinyi, Ulanga, Kilombero yenyewe na Jimbo la Mlimba. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, hizo wilaya zina matatizo. Tumepata bahati ya kupata ardhi nzuri, tunamshukuru Mungu, lakini ardhi tuliyopata inatutesa. Kuna mwananchi ambaye amezaliwa Malinyi tangu miaka hiyo, yawezekana labda Mjerumani au Mwingereza yuko pale kwenye Bonde la Mlimba, kwenye Bonde la Ngombo. Sasa leo hii wanamwambia yule mwananchi ahame. Sasa hatujui akihama anaenda wapi.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa mara ya kwanza wanasema lile eneo lilipimwa mwaka 1952, lilipimwa na GN ya kwanza ikawekwa 2012. Wakaja wakaweka tena GN ya pili 2017. Zote hizi zinam-limit yule mwananchi asiweze kulima, asiweze kuwa na makazi pale. Sasa tunajiuliza kwa miaka yote hiyo, huyu mwananchi ataenda kuishi wapi? Kazaliwa pale, kakulia pale na pengine hata Morogoro Mjini haijui. Leo unamwambia ahame Ngombo, ahame Mlimba, ahame Kilombero na sasa hivi Kilombero ni mji mkubwa sana wa Ifakara, wenyewe wanafahamu, lakini mnatuambia tuhame.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa naiuliza hii Wizara, kama iliweza kupima mwaka 1952 wakati wananchi wale walikuwa wachache tu hawakuweza kuwaelewesha kuwa eneo limepimwa na mwondoke wakaja wakaweka GN 2012 na 2017. Hebu niiulize Wizara, Tanzania ni kubwa na ina ardhi nzuri hususan Morogoro na hizi wilaya ambazo nimezitaja. Sasa naiomba Serikali itoe tamko, je, kwa sasa hivi tufuate GN ya 2012 au wale wananchi wafuate GN ya 2017, kwa maana wale wananchi hawawezi wakafanya kazi zozote za kimaendeleo, wapo wamekaa. Wakienda kulima watu wa TAWA wanawafuata ambao ni askari wa maliasili wanasema hili ni eneo la maliasili. Wakikaa hivi hivi ina maana kwamba watu wanakaribisha umaskini. Je, hawa watu tunawafanyaje? Naomba Wizara inisaidie hilo ili wale watu waweze kujua kama wanaishi pale na kama hawataishi watupe mbadala kwamba waelekee wapi. Tanzania ni kubwa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, la pili, nazungumzia mipaka vile vile kati ya wakulima na wafugaji. Mkoa wa Morogoro ni kati ya mikoa ambayo ina changamoto kubwa sana ya migogoro kati ya wakulima na wafugaji na hii migogoro inatokana na mipaka. Hakuna mipaka ambayo inaainisha kwamba hili ni eneo la wakulima na hili ni eneo la wafugaji. Matokeo yake watu tunasema tuna amani. Ukweli katika ule mkoa sehemu kubwa amani haipo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sisi kipindi cha kampeni tulienda kufanya kampeni tunakuta kabisa mtu anaenda analisha sio ya kuambiwa, kwa macho yangu, anaenda analisha ng’ombe wake anapeleka kwenye mashamba ya watu. Mimi mwenyewe pia lilinipata kwenye shamba langu, nawakuta vijana wanaenda, nawauliza mbona mnalisha kwenye shamba, wananiambia unaniuliza mimi, muulize ng’ombe!

Mheshimiwa Naibu Spika, niambie, hivi unamkuta mtu analisha ng’ombe kabisa kwenye shamba lako, unamuuliza, anasema unaniuliza mimi, muulize ng’ombe unamjibu nini? Unamfanyaje mtu kama huyu? Ni mateso. Yaani tunaishi kama vile sisi ni wahamiaji. Uende kwenye GN unaambiwa uondoke, basi ulime angalau ujikwamue mkulima mdogo, unaambiwa mashamba hayo ndiyo malisho kwao. Sasa huyu mwananchi wa Ifakara, mwananchi wa Kilombero na Kilosa na Mvomero katika Mkoa wa Morogoro, anaishije huyu? Siku zote ukiangalia sana mkulima na mfugaji, mkulima kipato chake ni cha chini na mkulima huyu ndiyo anayegandamizwa. Naomba majibu kwa haya masuala yangu mawili. (MakofI)

Mheshimiwa Naibu Spika, nashauri Wizara kama wanataka kuwe na amani tungechukua ile mipaka tuweke ekari kama moja yaani huku wakulima na huku wafugaji. Anayevuka kuelekea kwa mwenzake ni mgomvi, maana sasa hivi amani hakuna! (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lingine ambalo nataka kuongelea ni hizi institution zetu za Serikali, kwamba tuna shule na hospitali za Serikali, lakini zile hospitali zina viwanja, shule zina viwanja. Ukiangalia sana unakuta kwamba shule nyingi wanafika wakati vile viwanja vinachukuliwa na watu wenye pesa. Sasa ukiuliza kwa nini, kwa mfano kiwanja cha mpira, watu wameweka wamejenga shule ya Serikali, wana kiwanja chao cha mpira cha michezo, lakini baada ya muda mwenye pesa akiona eneo linamfaa anaenda anajenga nyumba. Sababu ni nini? Hakuna, eneo lile halina hatimiliki, lingekuwa na hatimiliki wale watu wasingevamia lile eneo. Kwa hiyo, naiomba Wizara tujitahidi kupima mali za umma. Shule zetu, hospitali zetu ili wale watu wachache wenye pesa wanaorubuni wasiweze kuingilia pale hatimaye wakachukua maeneo ya umma na baadaye tukakosa hizo sehemu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, la nne na la mwisho kabisa, nashindwa kuwaelewa Wizara ya Ardhi kwamba, hivi mtu anajenga bondeni, anajenga sehemu ambayo haitakiwi mtu kujenga. Anajenga wa kwanza, mnamwangalia; anajenga wa pili, mnamwangalia, wanafika 1,000 mnasema wabomolewe waondoke. Sasa mlishindwa nini kumsimamisha yule wa kwanza badala ya kulete hasara kubwa katika Serikali? Hilo nalo naomba mnieleze, kwani kunakuwa na matatizo gani kuwasimamisha mtu ambaye amejenga kwenye sehemu ambayo ni bonde au njia ya kupita maji? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mimi nimetoka kwenye maji. Watu wanakwambia, maji yanakimbia watu, sio kweli hata siku moja. Maji hata ujenge nyumba ya aina gani…

MHE. ZUBERI M. KUCHAUKA: Mheshimiwa Naibu Spika, taarifa.

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Kamguna, kuna Taarifa kutoka kwa Mheshimiwa Kuchauka.

T A A R I F A

MHE. ZUBERI M. KUCHAUKA: Mheshimiwa Naibu Spika, nilikuwa nataka nimpe taarifa mchangiaji. Siyo tu kwamba hao watu wanaojenga wanaonekana, mpaka umeme wanaletewa na pengine hata kama huduma ya maji wanaletewa vilevile. Halafu baadaye wanakuja kuwaambiwa wabomolewe. (Makofi)

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Kamguna, unapokea taarifa hiyo?

MHE. ALEKSIA A. KAMGUNA: Mheshimiwa Naibu Spika, nimeipokea hiyo taarifa. Nakubaliana naye kabisa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, hebu angalieni na mara nyingi wanaojenga pale ni wale walalahoi. Wale watu tunawachukuliaje? Mtu amejipigapiga akajikusanyakusanya akajenga pale kwenye bonde, tunamwachia, halafu akija kubomolewa tunasema hatukulipi compensation kwa sababu wewe umejenga sehemu ambayo haikutakiwa. Kwani mwanzo anajenga ninyi hamkumwona? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, katika hilo, kama mtakuwa mnatuachia hivyo, basi inabidi wale muwalipe. Ni wenyewe mnataka, kwani mwanzo hayakuwepo mabonde? Mbona yalikuwa hayazibwi?

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hayo machache naomba kuwasilisha. Naunga mkono hoja, ahsante. (Makofi)