Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi

Hon. Benaya Liuka Kapinga

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mbinga Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

2

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi

MHE. BENAYA L. KAPINGA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana kwa kuwa mzungumzaji wa mwisho wa session hii ya asubuhi. Niungane na wenzangu kwa dhati kabisa, kumpongeza mtani wangu mla kale kanyama katamu, Mheshimiwa Lukuvi, hongera sana pamoja na Naibu Waziri, lakini na wataalam kule. Kwa kweli mmefanya kazi nzuri na hii inaonesha wachangiaji wamekuwa wachache tofauti na pale nyuma Wizara hii ilikuwa na wachangiaji wengi sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nachangia eneo moja eneo la migogoro. Nimshukuru sana Mheshimiwa Waziri, Jimboni kwangu kumekuwa na matatizo mengi ya migogoro kwa muda mrefu kuanzia mwaka 2017, nina orodha hapa zaidi ya watu 3,000, hawa wananchi wa Kata ya Maguu, Kijiji cha Mkuwani na vijiji vingine vya Jirani. Hawa wananchi kwa miaka zaidi ya minne wanahangaika na maeneo yao ambayo yalikuwa mashamba sasa yamechukuliwa na Wilaya ya Nyasa kufanya mradi wa panda miti kibiashara. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mradi huu ni mzuri sana, lakini utaratibu uliotumika ni wa hovyo mno, umesababisha tumefika mahali sasa hivi wanapigana risasi pale kijijini. Tumefika mahali wananchi hawa wanachukuliwa mali zao, tumefika mahali wananchi hawa hawawezi kufanya shughuli ya kiuchumi kwenye hayo, maeneo ambayo walikuwa wanayamiliki tangu wengine walivyozaliwa na wengine sasa hivi ni wababu, wana wajukuu na vitukuu, lakini imefika mtu mmoja tu ameamua huu mradi uanzishwe na kuwafukuza hawa wananchi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mwaka 2019 alienda Waziri Mkuu, wananchi wale walishika mabango tunadhulumiwa ardhi yetu, tunadhulumiwa ardhi yetu. Waziri Mkuu alitoa maelekezo kwa viongozi ambao leo pia Mheshimiwa Waziri ametoa maelekezo hapa kwamba, viongozi waliopo huku watatue kero za wananchi. Kwa bahati mbaya sana yale maelekezo viongozi wale hawakuyafanyia kazi, wananchi hawa wamehangaika ngazi zote katika mkoa wetu hawakupata masuluhisho, mwisho wa siku waliamua kuja hapa. Namshukuru sana sana Waziri, alipiga simu na sasa hivi angalau wanapumua. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nimwombe Mheshimiwa Waziri ile ahadi aliyoisema kwamba atakwenda kule kwenda kuona naomba aitekeleze, kwa sababu bila yeye hatutapata masuluhisho, kwa nini nasema hivi? Shida kubwa hao viongozi aliowaelekeza hapa na wao wana interest na maeneo hayo. Nimefuatilia nimegundua kwamba, maeneo yale viongozi wa maeneo ya kule nao wameamua kujiingiza kwenye hii miradi, sasa mwananchi akilalamika eneo langu linaporwa, hana masuluhisho hawezi kutoa utatuzi wa ile shida ikiwa yeye pia ni mmiliki wa mradi ule. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, inahitaji mtu mwingine kama alivyofanya Waziri. Nimesikia hapa wenzangu wanasema tuwaachie Mwenyekiti wa Kijiji, sijui na nani anayefuata na mwingine, wengine ndio wanufaika wa hii miradi sasa atatoaje masuluhisho? Kwa hiyo, mgogoro huu umeleta shida sana sana sana, leo hii ukifika Mbinga Mheshimiwa Waziri watakupa jogoo, mbuzi na ng’ombe kwa majibu aliyoyatoa hapa siku ile kwa wale wananchi wachache waliokuja kumwona. Kwa hiyo, nimpongeze sana sana. (Makofi)

Mheshimiwa Waziri, ninachosema ule mradi ni mzuri sana, ingewezekana kabisa. Kwa sababu, kwa maneno yao wanasema kwamba wameshauriwa kimazingira kwamba sasa eneo lile linatunza maji ya Ziwa Nyasa, kwa hiyo, ni lazima liwekwe vizuri, lipandwe miti, sawa. Kwa nini hawakufikia kuwashirikisha hawa wananchi wamiliki wa yale maeneo na kuwaambia sasa jamani mmekuwa hapa kwa muda mrefu, sasa hivi imefika mahalI hapa tunataka tupaboreshe tufanye mradi wa kimazingira. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa badala ya sisi wa eneo fulani au watu fulani kuwanyang’anya ninyi maeneo yenu, basi muwe sehemu ya huu mradi, kwani hili haliwezekani? Lingefanyika hili, pengine lisingeleta usumbufu ambao sasa hivi zaidi ya miaka minne wale watu hawana sehemu ya kulima. Kwa hiyo, ninachoshauri Mheshimiwa Waziri aje na maelekezo mazuri kuhusiana na hawa wananchi kwenye ardhi ambayo wamekuwa nayo, wamekufa nayo na wengine wanaendelea kuzeeka nayo mpaka leo hii, lakini sasa hawana haki nayo kabisa. Imefika mahali wamepigwa risasi watu pale kabisa kabisa, sasa unampigaje mtu mwenye haki yake risasi? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, hivi ni kweli Watanzania tuko hivyo? Kilichofanyika ni kwamba, kabla ya mwaka 2012, eneo lile lilikuwa Wilaya moja, sasa hivi Wilaya ile imegawanyika iko Wilaya ya Nyasa na Wilaya hii ya Mbinga.

T A A R I F A

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Stella Manyanya.

MHE. ENG. STELLA M. MANYANYA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kuwa mimi ni Mbunge ninayetoka Nyasa na kwa mchango huu unaotolewa na Mheshimiwa Mbunge, jirani yangu kuhusu mgogoro huu uliodumu kwa muda mrefu kidogo, ambao nakubaliana kwamba, mpango na mradi unaoendelea pale wa miti ni mzuri na kwa sababu mwekezaji sio lazima atoke sehemu za mbali tu na asiwe Jirani yetu. Kwa hiyo, jambo jema ni kwamba hata wao wanaweza kuendeleza katika misingi ya mradi ule lakini bila kuwa na migogoro. Kwa hiyo ninachoomba ni kwamba siku ikitokea Mheshimiwa Waziri anaenda huko, basi mimi Mbunge wa Nyasa niwepo pia, ili kuhakikisha kwamba haki zinatendeka katika pande zote mbili. Ahsante sana. (Makofi)

SPIKA: Mheshimiwa Benaya Kapinga, malizia mchango wako.

MHE. BENAYA L. KAPINGA: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru sana na taarifa yake naipokea, nilikuwa nasubiri aongee vile alivyosema, ahsante sana.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, kugawanyika kwa mipaka hakumwondolei mtu haki ya kumiliki mali, sisi wote ni Watanzania, tuna haki ya kufanya shughuli eneo lolote ili mradi hatuvunji sheria. Kwa hiyo, nimwombe Mheshimiwa Waziri, sikuwa na maneno mengi nilitaka nimwambie hili ili aendelee kutusaidia kama alivyotatua maeneo mengine na sisi akatutatulie huu mgogoro wetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. (Makofi)