Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi

Hon Ally Juma Makoa

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kondoa Mjini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

3

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi

MHE. ALLY J. MAKOA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi hii. Nianze kwa kumshukuru Mwenyezi Mungu lakini niwapongeze Waziri wa Ardhi, Naibu Waziri, Katibu Mkuu na hata Kamishna Mkuu wa Ardhi kwa kazi kubwa wanazozifanya. Pia nisiwe mchoyo wa fadhila kumpongeza Kamishna wa Mkoa ndugu yangu Kabonge kwa majukumu makubwa anayohudumia Mkoa wa Dodoma, katika kuhakikisha wananchi wanapata hati.

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kuyasema hayo, niendelee na mchango wangu kwamba ardhi ni bidhaa pekee ambayo kama tutaitumia vizuri Taifa letu litaendelea kupata kipato endelevu. Ni kipato ambacho hakiyumbi kwa sababu hatutegemei kwamba kuna mwaka mapato yanayotokana na ardhi yatapungua kwa sababu kila mwaka tunapima ardhi na watu wanaendelea kulipa kodi.

Mheshimiwa Naibu Spika, kama ni chanzo pekee cha uhakika cha mapato ya Taifa letu ni lazima sasa kuiwekea miundombinu rafiki Wizara hii ili kuhakikisha mapato yanayotokana na ardhi kila mwaka yanaendelea kupanda. Nyenzo mojawapo ni kusaidia Wizara hii kupata watumishi wa kutosha katika zoezi la kuhakikisha kwamba upimaji wa ardhi unafanyika kwa ufanisi.

Mheshimiwa Naibu Spika, halmashauri nyingi hazina Maafisa wa Ardhi. Unakuta halmashauri ina afisa mmoja huyo ndio apime, huyo ndio aandae ramani, maana yake utagundua kwamba hatuwezi kufikia malengo ya upimaji wa ardhi kama tunavyohitaji. Kwa hiyo Serikali iangalie, katika ajira ni vyema kuipa kipaumbele Wizara ya Ardhi kuajiri watendaji wa ardhi ili kuhakikisha kwamba zoezi hili la upimaji linakwenda kikamilifu.

Mheshimiwa Naibu Spika, hoja iliyo Mezani ni ardhi. Watanzania wengi vipato vyao ni vya chini sana. Mifumo ambayo inatumika kumilikisha ardhi ni mifumo ambayo si rafiki kwa Watanzania wengi ambao vipato vyao ni vya chini.

Mheshimiwa Naibu Spika, mfano, naweza nikasema kwamba, ardhi inaweza ikawa inauzwa milioni nne kwa kima cha chini na mnunuzi anatakiwa alipe kwa muda mfupi sana; miezi mitatu. Unajiuliza, ni Mtanzania wa aina gani huyu ambaye amelengwa kununua ardhi kwa bei kubwa kiasi hicho, hali ya kuwa kipato chao ni kidogo.

Mheshimiwa Naibu Spika, hapa nashauri sasa Wizara ya Ardhi ikishirikiana na TAMISEMI, kwa maana ya halmashauri, watafute miundombinu, watafute njia rahisi za kuhakikisha kwamba kila Mtanzania anamiliki ardhi kutokana na kipato chake alichonacho. Wanaweza wakaenda kupata wawekezaji. Mfano, wanaweza kuingia kwenye mabenki wakawa wanatoa hati, hati zinakwenda benki, Watanzania wenye kipato cha chini kidogo wakawa wanagomboa hati zao mabenki kwa kipindi hata cha miaka mitatu mpaka mitano, lakini kwa miezi mitatu Watanzania wachache sana wataweza kumiliki ardhi. Nina ushahidi; vijana wengi wamerudisha ardhi baada ya kushindwa kukamilisha malipo kwa sababu wameshindwa kutekeleza mkataba walioingia wa kulipa ardhi kwa kipindi cha miezi mitatu.

Mheshimiwa Naibu Spika, zoezi hilo la wananchi wengi kushindwa kununua ardhi linakwamisha mapato ya ardhi kwa sababu kama ardhi hainunuliwi maana yake hati hazitaandaliwa. Kama hati hazitaandaliwa maana yake Serikali itapoteza fedha nyingi kutokana na hati, lakini kama hati nyingi zitanunuliwa, Serikali itapata fedha nyingi sana. Kwa hiyo tuweke mfumo rahisi wa wananchi kupata hati mapema. Ikiwezekana, wananchi wauziwe hati na siyo wauziwe maeneo. Maandalizi ya hati yatangulie halafu ndipo watu watangaziwe kuuziwa viwanja ambavyo tayari vimekamilika hati. Hapo Ardhi itaendelea kupata fedha kupitia hati zake. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusiana na migogoro; nawapongeza sana Mheshimiwa Waziri na Naibu Waziri, wanashughulika kikamilifu sana kutatua migogoro ya ardhi. Sasa pale kwetu, nilizungumza na Mheshimiwa Waziri na Mheshimiwa Naibu Waziri, kuna migogoro mitatu ambayo inawasubiri wao tu ili iweze kukamilika. Hapa nimekubaliana na usemi wake wa kusema kwamba, maeneo yote ya wananchi yaliyochukuliwa hayakulipwa fidia, warejeshewe.

Mheshimiwa Naibu Spika, sisi tuna mgogoro ambao upo baina ya wananchi na halmashauri na wamiliki. Halmashauri imechukua maeneo ya mtu, ya wananchi, haikulipa fidia. Lakini imeyapima yale maeneo na maeneo yamekwishauzwa kwa wananchi na wananchi wamekwishalipa fedha zao. Sasa wananchi wenye maeneo hawakulipwa fidia, wamezuia shughuli yoyote ya maendeleo kama matamko ya Mheshimiwa Waziri. Kwa hiyo namwomba ile nia yake ya kwenda Kondoa kwa ajili ya kusaidia kutatua huu mgogoro kila mmoja apate haki yake, aendelee kuwa nao. Naomba baada ya zoezi hili tufuatane naye kwa ajili ya kwenda kutatua mgogoro huo.

Mheshimiwa Naibu Spika, upo mgogoro mwingine wa ardhi wa wananchi, kijiji pamoja na Hifadhi ya Swagaswaga. Wananchi wa Mongoroma na maeneo yanayopitiwa na hifadhi ile wao wanalalamikia mipaka. Najua siku atakayokuja Waziri, tutakwenda kutembea na kuwasikiliza wale wananchi. Zoezi hili la migogoro ya ardhi inayohusiana na mipaka ni matumaini yangu kwamba tutakwenda kulimaliza kama tutafika kwa wananchi kuwasikiliza halafu sisi wenye mamlaka, Mheshimiwa Waziri, viongozi pamoja na wananchi na mimi Mwakilishi wao, tukae tuone namna gani tunakwenda kuitatua hii migogoro ili wananchi waendelee na shughuli za maendeleo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mgogoro namba tatu upo kati ya wananchi wa Iyoli na maeneo yanayohusiana na mgogoro Kata ya Kingale kati ya wananchi na Magereza. Waliotoa viwanja kukaribisha Gereza la King’ang’a wapo. Wenye kumiliki gereza hilo wapo. Viongozi tupo na sisi wawakilishi pia tupo; tunashindwaje kwenda kumaliza mgogoro huu ili wananchi waendelee na shughuli za kilimo?

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo nina matumaini makubwa sana. Ahadi ya Waziri ya kwenda Kondoa kumaliza migogoro hii ikikamilika wananchi watakwenda kufanya shughuli zao za kujiongezea kipato na migogoro hii ambayo inaendelea itakuwa imekwisha.

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kuyasema hayo, naomba kuunga mkono hoja. Ahsante sana. (Makofi)