Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Kilimo

Hon. Daniel Baran Sillo

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Babati Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

2

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Kilimo

MHE. DANIEL B. SILLO: Mheshimiwa Spika, nashukuru sana kwa kupata nafasi hii ili niweze kuchangia katika Wizara hii muhimu ya Kilimo, Wizara ambayo inachangia asilimia 27 ya pato la Taifa, asilimia 25 ya fedha za kigeni lakini inaajiri Watanzania wasiopungua asilimia 65.

Mheshimiwa Spika, Sera ya Serikali sasa ni Serikali ya viwanda na ni ukweli kwamba raw materials au malighafi zaidi ya asilimia 60 zinatoka kwenye kilimo. Kwa hiyo, niiombe sana Serikali iwekeze kwenye kilimo, ikishawekeza kwenye kilimo maana yake tunapata viwanda vya kutosha, tukishapata viwanda tunaajiri Watanzania wengi, lakini pia Serikali inapata kodi. Ni ukweli usiopingika kwamba kilimo ni biashara ya chakula na ajira. Kwa hiyo niiombe sana Wizara iwekeze kwenye kilimo ili tupate na wigo wa kodi pia katika Taifa letu, (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naomba nizungumze kwa kifupi pia kuhusu wakulima wadogo hasa wa vijijini. Wakulima wa vijijini toka anaandaa shamba hadi anavuna hajawahi kutembelewa na Afisa Ugani hata mmoja. Hii ni changamoto kubwa sana kwa wakulima wa vijijini, watabaki kulima kilimo cha kujikimu, hawatapata kilimo cha tija. Kwa hiyo niiombe sana Wizara iangalie sana wakulima wa vijijini, wanateseka kweli kweli.

Mheshimiwa Spika, kuna mashamba yasiyoendelezwa; nchi yetu ina sera ya kubinafsisha mashamba kwa wawekezaji. Ni kweli kabisa tunawahitaji wawekezaji maana wakiwekeza watalipa kodi na wataajiri Watanzania, lakini kuna mashamba mengi katika maeneo mbalimbali nchini ambayo mtu amebinafsishiwa lakini anatumia labda robo tatu au robo tu ya eneo lote. Eneo lililobaki linabaki wazi wakati kuna wakulima wanaozunguka eneo hilo wanateseka hawana eneo la kulima. Naomba sana Wizara hii isaidiane na Wizara ya Ardhi, mashamba haya ambayo hayajaendelezwa Serikali iwagawie wananchi waweze kulima. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nina mifano kule kwangu Babati Vijijini; kuna Bonde la Kiru, Kata za Kisangaji na Magara, kwenye msimu huu wa kilimo juzi watu walikatana mapanga kwenye Kijiji cha Magara, shamba lilikuwa na mwekezaji, mwekezaji haonekani, watu wamevamia. Kwa hiyo niiombe sana Serikali itatue migogoro hiyo ili wananchi wapate maeneo ya kulima.

Mheshimiwa Spika, sasa nizungumzie masoko ya mazao. Wanachi wetu wanateseka sana na masoko ya mazao yao. Mfano mdogo tu wa kilimo kama cha mahindi, mbegu ya mahindi kilo mbili inauzwa Sh.13,000, lakini leo gunia linauzwa Sh.18,000 mpaka Sh.20,000 gunia la kilo 100. Niiombe sana Wizara ya Kilimo iwasaidie Watanzania hawa wanyonge hasa wa vijijini, wanateseka mno. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Halmashauri yangu ya Babati Vijijini kuna wakulima wazuri sana wa mbaazi. Mwaka jana msimu uliopita mbaazi zilibaki shambani, hakuna pa kuuza kilo Sh.200, sijui Sh.300, mkulima ameteseka mwaka mzima, kwanza hajashauriwa na wataalam wa kilimo na pia masoko asipatiwe. Kwa hiyo, naiomba sana Wizara ijielekeze kutafuta masoko ya mazao ya wakulima wetu.

Mheshimiwa Spika, kule kwangu kuna Vijiji vya Nar, Madunga, kuna wakulima wazuri sana wa vitunguu, lakini hawapati ushauri. Wanabaki kuhangaika na virobo heka vyao. Hii haiwasaidii, naomba sana Wizara iwasaidie wananchi hawa wa vijijini. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa kuwa kupanga ni kuchagua, niiombe Wizara hii ya Kilimo ijielekeze kuchagua kuwekeza kwenye kilimo, nchi hii itatoka hapa itasonga mbele, wananchi watasogea mbele katika mapato yao na umaskini utapungua kwa wananchi wetu hasa wa vijijini. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, baada ya kusema haya, nikushukuru kwa kunipa nafasi hii na naunga mkono hoja. (Makofi)