Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Kilimo

Hon. Margaret Simwanza Sitta

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Urambo

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Kilimo

MHE. MARGARET S. SITTA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi ili nichangie hoja iliyopo mezani. Kwanza namshukuru Mwenyezi Mungu kwa kunipa uhai, lakini pia nawashukuru sana wananchi wa Urambo na familia yangu kwa jinsi ambavyo tunashirikiana nao. Nawaomba tuendelee kushirikiana kwa lengo la kuendeleza Wilaya yetu.

Mheshimiwa Spika, nachukua nafasi hii kuipongeza Serikali inayoongozwa na Mama yetu Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan kwa jinsi ambavyo wanachapa kazi kwa kuzingatia yaliyopo ndani ya Ilani ya Uchaguzi. Hongera sana kwao. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nachukua nafasi hii pikumpongeza Mheshimiwa Waziri, Profesa Mkenda pamoja na Naibu Waziri, Makatibu Wakuu na watendaji wote wa Wizara hii na naamini wanasikiliza yote ambayo Waheshimiwa Wabunge wameongea ili kesho tupate mrejesho mzuri. Ninapoongea kwa niaba ya wananchi wa Urambo siwezi kuacha kutaja tumbaku, tumbaku hoyee. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tumbaku ndio uhai wetu sisi kwa sababu ndio zao ambalo linatuingizia fedha na miaka ya nyuma wakati wa mauzo kama huu uliopo sasa hivi, mitaani kote watu wangekuwa wanafurahia kwa sababu tumbaku ilikuwa inauzwa tani kwa tani kadri ambavyo mkulima alivyokuwa akilima. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nachukua nafasi hii kuwapongeza wenzangu wote waliotangulia kwa kusema kwamba changamoto kubwa ya Wizara ya Kilimo ni masoko, masoko ndio ambayo yanaamua mkulima alime kiasi gani na kumpa ari pia. Tumbaku bado ina changamoto kubwa sana. Kwa sasa hivi bei ambayo ingeweza kutolewa kama tungekuwa na wanunuzi wengi ingekuwa dola 1.63 lakini mpaka sasa hivi ni JTI tu ambao wamefikisha angalau dola moja 1.54, wakifuatiwa na wenzao ambao ni akina Alliance na wengineo ambao wananunua kwa dola 1.45.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo suala la soko ni la muhimu sana, tunaomba wanunuzi zaidi, tunaomba soko liwe la uhakika Zaidi. Sasa hivi tumbaku inauzwa lakini bado haijafikia peak ambayo tutasema kweli mkulima anapata haki yake na jasho lake alilotoa. Namwomba Mheshimiwa Waziri atakapokuja mezani kuja ku-wind up yaani anapokuwa anahitimisha atuambie kama changamoto kubwa ni soko iweje TLTC waondoke ambao ndio walikuwa wananunua tumbaku nyingi Mkoa wa Tabora. Kwa hiyo tunaomba atakapokuja kueleza hapa atuambie TLTC wapo, wameondoka na kama wameondoka kweli imeshindikana kukubaliana nao ili waendelee kununua ili tupate wanunuzi wengi zaidi? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pia itakuwa ni vizuri kama Waziri atatuambia kwamba TLTC ndio waliokuwa wamenunua Kiwanda cha Tumbaku, TLTC ndio walikuwa wamechukua ma-godown yote, kama wanaondoka nini hatma ya ma- godown na kiwanda walichokuwa wanamiliki? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, la pili, ni suala la makisio, kutokana na kutokuwa na wanunuzi wengi, sasa hivi pamoja na kwamba mnasema Maafisa Ugani watembee, inasaidia nini Maafisa Ugani wakitembea, halafu baadaye unaambiwa wanunuzi wote wanataka kilo labda1,000,000 tu, lakini tungekuwa na wanunuzi wengi wangenunua nyingi.

Mheshimiwa Spika, fikiria, sasa hivi mkulima anaambiwa wewe lima mwisho labda kilogram 100 au 200 tu, why? Sasa kuna haja gani ya kuhimiza watu walime, halafu baada ya pale wanakosa soko au wanapewa makisio madogo. Kwa hiyo Mheshimiwa Waziri atusaidie tunafanyaje ili wakulima walime tani yao kadri wanavyopenda kutokana na jinsi wanafundishwa kilimo cha kisasa.

Mheshimiwa Spika, lingine ambalo ni la muhimu sana ni suala la mbolea. Wenzangu waliotangulia wameongea kwamba ni vizuri mbolea ikafika kwa wakati, Wizara wanajitahidi lakini bado wajitahidi zaidi ili mkulima anapoanza kuandaa shamba, sio anaanza kuuliza kwanza mbolea inakuja lini? Inabidi mbolea iwe tayari ipo nchini. Wizara imekuwa na utaratibu mzuri wanaleta katika bulky yaani nyingui, sawa, lakini kufika kwa wakati ili mkulima anapoandaa shamba lake mbolea iwe tayari imeshafika. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lingine ambalo naona ni matatizo makubwa, Bodi ya Tumbaku inatusaidia kuwasiliana kuhusu bei, lakini haina vitendea kazi. Kwa hiyo tunaomba Bodi ya Tumbaku wawe na vitendea kazi. Kwa mfano, kama kwangu hata gari hawana, wakitaka kuzunguka mpaka waombe gari ya Mkurugenzi ni aibu. Kwa hiyo nadhani Bodi ya Tumbaku ipewe vitendea kazi na vingine vyote ambavyo wanajua wao hawana ili waendelee kutekeleza majukumu yao.

Mheshimiwa Spika, lingine, wametaja mikoa mitatu ambayo itafanyiwa utafiti wa mazao ya alizeti na kadhalika, wametaja Dodoma, Singida na Simiyu lakini wamesahau Mkoa wa Tabora, Mkoa wa Tabora ni jirani ya Singida, tupo sawasawa na wao na cha ajabu kuhusu pamba, Igunga ndio ina shamba la mbegu. Sasa mkoa ambao una shamba la mbegu wameuacha katika haya majaribio ya mikoa mitatu! Kwa hiyo naiomba sana Serikali itusaidie kuirudisha au kuiingiza Tabora katika mikoa ile mitatu ili iwe mikoa minne; kwanza kwa sababu ardhi ni sawasawa, na sisi alizeti inakubali na kama nilivyosema shamba la mbegu yaani utafiti kuhusu mbegu upo Igunga ambao ni Mkoa wa Tabora. Kwa hiyo tunaomba kwa heshima na taadhima Mkoa wa Tabora uwekwe katika mikoa ile ya majaribio.

Mheshimiwa Spika, baada ya kusema hivyo…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa mzungumzaji)

SPIKA: Ahsante Mheshimiwa Margaret Sitta.

MHE. MARGARET S. SITTA: Mheshimiwa Spika, baada ya kusema hayo, naunga mkono hoja. Ahsante sana. (Makofi)