Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Kilimo

Hon. Kasalali Emmanuel Mageni

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Sumve

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Kilimo

MHE. KASALALI E. MAGENI: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa nafasi. Pia nitumie nafasi hii kuwapongeza viongozi wa Wizara ya Kilimo, Waziri na Naibu; na mahususi kabisa nampongeza na kumshukuru Naibu Waziri wa Kilimo, kaka yangu Mheshimiwa Hussein Bashe. Wakati sisi watu wa Sumve na Kwimba tulipokuwa tuna kilio chetu cha kupangiwa namna ya kuuza choroko, zao ambalo tulikuwa tunalilima bila usaidizi wa Serikali kwa asilimia 100, alilia pamoja na sisi. Namshukuru kwa hilo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nitumie nafasi hii kusema kwamba, sisi watu wa Sumve bado tunacho kilio chetu kikubwa katika Wizara hii ya Kilimo. Shida yetu kubwa…

SPIKA: Kwa hiyo, Mheshimiwa Kasalali Serikali iliingia hata kwenye choroko?

MHE. KASALALI E. MAGENI: Mheshimiwa Spika, iliingia.

SPIKA: Umesikia hayo maneno! (Kicheko)

MHE. KASALALI E. MAGENI: Mheshimiwa Spika, ni jambo la aibu kulisema hapa kwenye Bunge Tukufu namna hii kwa sababu, sisi Wasukuma tunalima choroko. Kwetu choroko ni kama benki. Yaani familia ambayo haina choroko ni familia ambayo haiheshimiki. Yaani tunamaanisha kwamba choroko ni kama benki zetu kwa sababu hatuko karibu na mabenki, sisi bado kule ni washamba, ni vijijini. Sasa mtoto anapougua, mimi nachukua kilo moja ya choroko naenda kwa mtu ambaye anajulikana kwamba huwa ananunua, ninampa napata pesa, naenda kununua dawa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sasa Serikali bila aibu, wakaweka choroko kwenye Stakabadhi Ghalani.

SPIKA: Aah, kwa hiyo, ni kangomba.

MHE. KASALALI E. MAGENI: Mheshimiwa Spika, mwaka 2020 watu wa Sumve wameteseka. Ninasema Mheshimiwa Bashe tumelianaye kwa sababu nimehangaikanaye kwenye kiti chake pale nikijitahidi kujieleza. Nimeeleza, lakini naye akichukua hatua, kuna mtu anaitwa mrajisi, sijui hawa watu wanatoka wapi? Nikafikiri labda mrajisi huyu inawezekana amezaliwa India au Denmark. Kama angekuwa amezaliwa kwetu, angeshangaa kama ulivyoshangaa wewe kuona choroko inaingizwa kwenye Stakabadhi Ghalani. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, wakulima wamenyanyasika, wanalazimishwa wapeleke hizo kilo moja moja…

MHE. TABASAM H. MWAGAO: Mheshimiwa Spika, taarifa.

SPIKA: Mheshimiwa Tabasam.

T A A R I F A

MHE. TABASAM H. MWAGAO: Mheshimiwa Spika, namwambia tu mzungumzaji kwamba choroko ili uipeleke katika Stakabadahi Ghalani, mtu analima eka moja anapata debe moja. Ili kujaa tani 10 mpaka uwe na wakulima 1,000. Sasa hii ni hatari sana na hao walioko kule au wale AMCOS na wenyewe ni majambazi hawana hata mtaji wa 2,000/=. (Makofi)

MHE. KASALALI E. MAGENI: Mheshimiwa Spika, taarifa hii ya heshima kutoka kwa Mheshimiwa Tabasam naipokea. Nasisitiza kwamba mimi nilikuwa natamani kumwona Mrajisi. Wakati unatambulisha wageni wa Wizara ya Kilimo, nilikuwa nime-concentrate, lakini inaonekana ulimjumuisha kwenye Maafisa. (Makofi/Kicheko)

Mheshimiwa Spika, hawa watu wanafikiria kama wako nje ya nchi. Aling’ang’ana, Mheshimiwa Naibu Waziri anatoa maelekezo mpaka akaandika barua, hawataki kuifuata. Tunalazimishwa; mwaka 2020 watu wa Sumve wamepata hasara ya mamilioni ya pesa. Kuna watu wamekamatwa, wamelipishwa fine zisizoelezeka.

Mheshimiwa Spika, Wizara ya Kilimo nitawaunga mkono bajeti yao tu endapo watakuja na maelezo ya kutosha ya kurudisha pesa zilizoibiwa kwa kutumia mgongo wa Serikali kwa wakulima wa choroko kwenye Jimbo la Sumve. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kuna kitu kinaitwa sijui TMX, sijui wanaita kitu gani. Mtu anakuja anaambiwa, kwamba sasa mwishoni waliposumbua sana; na ninamshukuru sana Mkuu wa Mkoa wa sasa wa Dodoma alikuwa Mkuu wa Mkoa wa Simiyu, kidogo alifanya ubunifu ambao ulirahisisha hili tatizo ingawaje lilibaki kuwa tatizo, lakini alilirahisisha akasema, sasa kwa sababu mnawalazimisha wakulima wote wakusanye mazao yao wakakopwe, yeye akasema wanunuzi nunueni, mkishanunua, basi hiyo sijui malipo yao ya TMX na nini na nini wachukue Serikali. Yaani wale Ushirika, zile AMCOS zilikuwa zinachukua pesa ambayo hazijaifanyia kazi. Huu ni ujambazi kama ujambazi mwingine. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, hawa watu wanatakiwa warudishe hela. Mheshimiwa Waziri tunataka hela za watu wa Sumve…

T A A R I F A

MHE. BONIPHACE M. GETERE: Mheshimiwa Spika, taarifa.

SPIKA: Mheshimiwa Getere nimekuona, taarifa.

MHE. BONIPHACE M. GETERE: Mheshimiwa Spika, ahsante. Wakati naendelea kumpa Taarifa mzungumzaji anayezungumza saa hizi, nikuombe hiyo sura uliyoingianayo asubuhi, uendelee kuwanayo hivyo hivyo. Mungu akusaidie hivyo hivyo; ya kukemea mambo ambayo yanaenda ovyo ovyo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, AMCOS katika nchi yetu, mimi sielewi. Mama mmoja ana miaka karibu 75 alinihoji siku moja. Wewe ni Mbunge wa nini? Kama mnakuwepo Bungeni miaka yote, sisi wakulima wa pamba kuna kitu kinaitwa AMCOS, hawana hela, wanachukua hela ya pamba ya mkulima wanakula; wanachukua ushuru wanakula; hawana hela ya kununua pamba. Ananiuliza ninyi ni Wabunge wa nini? Mbona mnazungumza mambo hayaishi?

Mheshimiwa Spika, ndiyo anayozungumza mzungumzaji hapa.

SPIKA: Taarifa hiyo Mheshimiwa Kasalali.

MHE. KASALALI E. MAGENI: Mheshimiwa Spika, naipokea na ninasisitiza, Mheshimiwa Waziri mimi sitaunga mkono hii bajeti, urudishe pesa. Hawa watu wanaitwa TMX na nani waliokuwa wanachukua pesa kwa wakulima wa Sumve bila kufanya chochote na kuwasababishia matatizo kwenye uuzaji wa choroko, pesa zirudi. Halafu pili, hiki kitu kinaitwa ushirika kwenye choroko kisije kikajirudia tena. Hatuwezi kuendelea namna hii, mnaleta vitu ambavyo havipo katika hali ya kawaida na bado sasa hivi tunavuna dengu, nasikia mna mpango huo huo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sisi watu wa Sumve huo mpango hatuutaki. Tunataka tuuze tunavyotaka kwa sababu wakati wa kulima hamtuletei chochote. Tunaanza kulima wenyewe, tunahangaika; sijawahi kuona Afisa Ugani anashauri kuhusu choroko. (Kicheko/Makofi)

SPIKA: Yaani Mheshimiwa Kasalali Serikali ina mpango wa kuingia kwenye dengu pia! (Kicheko/Makofi)

MHE. KASALALI E. MAGENI: Mheshimiwa Spika, wapo wamejipanga. Hawa watu wakati mwingine tuwe tunaona hata aibu, kwa sababu sisi ni viongozi na hawa wataalamu walioko huko, wanatushauri ovyo. Kwa sababu, hamwezi kushauri Serikali iweke Stakabadhi Ghalani choroko, kama kweli nyie ni watafiti. Kwa sababu, kuna wengine ni maprofesa, madokta, hizo elimu za Ph.D ni utafiti, sasa mnaingiaje kwenye jambo bila kulifanyia utafiti? Kwa sababu, wangefanya utafiti wasingetuletea hili tatizo. Sasa hivi wakulima wamefilisiwa, watu kule Sumve kwa kweli uchumi wetu umeyumba hapa katikati kwa sababu ya haya mambo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini nimalizie kwa suala la pamba. Mheshimiwa Waziri Bodi ya Pamba sisi wakulima wa pamba hatuitaki. Wewe ndio unaitaka. Sasa itaanza kushughulika na pamba ya Wizarani. Kwa sababu, hii bodi imeshindwa kabisa kuwasaidia wakulima wa pamba. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pamba imeshuka, bado tuna bodi na bado tuna wataalamu. Sasa hawa wataalamu ni wa nini? Tunaendelea kuwanao wa nini? Kwa sababu, hamji na mbinu za kumsaidia mkulima wa pamba apende kulima pamba. Wakulima wa pamba wakiniuliza jimboni kwangu nawaambia waache, kwa sababu, mwisho wa siku zinaniletea matatizo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sasa hivi kuna wakulima kwenye AMCOS kama za Kiminza, Lyoma, nakumbuka nikiwa Diwani, mpaka leo wanadai kuna hela; mpaka kuna wahasibu wamejinyonga. Sasa mnaendelea kuwa na Bodi ya Pamba ya nini? Hata hizi AMCOS, ni za nini? (Makofi)

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa mzungumzaji)

SPIKA: Ahsante.

MHE. KASALALI E. MAGENI: Mheshimiwa Spika, nafikiri kesho tutazungumza vizuri kama nitaunga mkono hoja au la, lakini haya mambo lazima yabadilishwe. Sisi watu wa Sumve kwa kweli hamjatutendea haki. (Kicheko/Makofi)