Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Kilimo

Hon. George Ranwell Mwenisongole

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mbozi

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Kilimo

MHE. GEORGE R. MWENISONGOLE: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa hii nafasi. Nianze mchango wangu kwenye hii Wizara kwa kuunga mkono hoja.

Mheshimiwa Spika, nimeingiwa na hofu sana baada ya kuisoma hii bajeti. Nimeingiwa na hofu kwa sababu hii ni bajeti ya kwanza tangu tutoke kuinadi Ilani yetu ya Chama cha Mapinduzi mwaka 2020 kwenye Uchaguzi ambao ulitupa ushindi wa kishindo sana kutoka kwa wananchi. Tuliwajaza matumaini makubwa sana wakulima na Watanzania masikini waishio vijijini kuhusu bei za mbolea na uhakika wa masoko; lakini katika hii bajeti ambayo nimeisoma zaidi ya mara tatu, sijaona hata mstari mmoja ambao unasisitiza kwamba Serikali itaweka mkazo kupunguza bei za mazao ya mahindi au kahawa. Sijaona mkazo wowote katika hii bajeti kuelezea uhakika wa soko la mahindi.

Mheshimiwa Spika, kwa sasa hivi kule kwetu Mbozi, debe la mahindi ni shilingi 3,000/=, gunia ni shilingi 18,000/= lakini mfuko wa mbolea ni shilingi 70,000/=. Sasa unategemea hawa wakulima ambao tumetoka tu kwenye uchaguzi wakatupa kura, watatuelewa vipi? Tunarudi tena mtaani hakuna solution ya bei za mbolea! (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kati ya vitu ambavyo Bunge hili linaweza kufanya ni kuishinikiza Serikali at least kutoa bei elekezi za mbolea. Shilingi 70,000/= kwa mfuko wa mbolea ni kubwa mno, huwezi kulia eka. Tutakuwa hatuwatendei haki wakulima masikini ambao wametuamini wakatupa kura zao, lakini miezi sita baadaye, Bajeti ya Kilimo ambayo walikuwa wakiisubiri, haina majibu ya matatizo yao. Kwa kweli hili ni suala ambalo ni lazima Mheshimiwa Waziri aliingilie na kulitilia mkazo sana kuhakikisha bei ya mbolea na uhakika wa haya masoko unakwenda kupatikana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kingine, nimpe pole Mheshimiwa Waziri, kwa sababu kama Wabunge wenzangu walivyoongea, uzoefu unaonyesha fedha za bajeti ya maendeleo zinatengwa nyingi, lakini zinazokuja ni chache. Sasa sijui kuna miujiza gani ya hizo baiskeli na pikipiki alizowaahidi Maafisa Ugani? Sijui atazipata vipi wakati fedha za maendeleo hazipati? Sijui atajigawa vipi? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa kweli hili ni suala ambalo kama kuna kitu ambacho Bunge hili linaweza kufanya, shilingi bilioni 200 ambazo ni bajeti nzima ya hii Wizara, ni hela ndogo sana kwa Serikali ambayo inakusanya zaidi ya shilingi trilioni moja kwa mwezi. Sasa kuna ugumu gani kupeleka hizo hela zote? Kwa nini kila mwaka hii Wizara hela inazoomba kwa maendeleo huwa hazikidhi vigezo vyao? Kwa nini hawapelekewi hela zao zote wanazoomba? What is billioni 200 kwa hii Serikali ambayo inakusanya zaidi ya shilingi trilioni moja kwa mwezi? Kwa nini wasipelekewe zote? Ugumu uko wapi? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lazima tuje na jawabu kuhakikisha hii bajeti, fedha zote walizoomba wanapelekewa kama kweli tuna nia ya kutaka kumsaidia mkulima masikini wa kule kijijini.

Mheshimiwa Spika, la mwisho, nataka niongelee hivi vyama vya msingi, AMCOS. Ni kweli kabisa kwamba vyama vya AMCOS ni Sera ya CCM na vilikuja kwa nia nzuri ya kutaka kumsaidia mkulima, especially wa kahawa kule kwetu Mbozi. Kwetu Mbozi hivi vyama vya ushirika vimegeuka kuwa kaburi kwa wakulima. Kwanza vinachukua mikopo benki bila wanachama wao kujua, unapofika wakati wa malipo, benki inakuja inakata hela zao na kuwafanya wakulima wale masikini kushindwa kupata malipo yao.

Mheshimiwa Spika, mpaka dakika hii ninapoongea hapa ndani ya Bunge lako Tukufu, kuna AMCOS zaidi ya tisa ndani ya Wilaya ya Mbozi hazijalipa wakulima wao. Watu wameshindwa kupeleka watoto wao shule, wameshindwa kulima, wametiwa umasikini wa ajabu na Serikali ipo, inaona.

Mheshimiwa Spika, siku moja nilishangaa hapa, posho zetu sisi Wabunge zilichelewa kwa siku mbili tatu, kulikuwa hakukaliki humu ndani. (Maneno Haya Siyo Sehemu ya Taarifa Rasmi za Bunge)

Mheshimiwa Spika, lakini wakulima wangu mimi Mbozi hawajalipwa mwaka sasa fedha zao za AMCOS na hakuna anayeshtuka.

SPIKA: Mheshimiwa Mwenisongole, hapo unamchokoza Spika. Unajaribu kuonesha kama kuna inefficiency hapa ndani, kitu ambacho siyo kweli. Futa hiyo kauli yako.

MHE. GEORGE R. MWENISONGOLE: Mheshimiwa Spika, okay, nafuta, lakini msisitizo wangu…

SPIKA: Hakuna cha lakini, unafuta halafu unaendelea kuchangia.

MHE. GEORGE R. MWENISONGOLE: Mheshimiwa Spika, okay, nafuta.

SPIKA: Eeh, endelea.

MHE. GEORGE R. MWENISONGOLE: Mheshimiwa Spika, point yangu ninayotaka kusema ni kwamba, suala hili la wakulima wa AMCOS kutokulipwa, nataka nitilie mkazo, kwa sababu hawa ni watu ambao wamepeleka mazao yao, wamepima, lakini mpaka leo hii hawajalipwa. Katika hali hiyo, suala hili hatuwezi kumsaidia yule mkulima.

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Waziri, kwa hiyo, ninachoomba ni kwamba utakapokuja kuhitimisha bajeti, uje na majibu ya kuhakikisha kwa nini hawa AMCOS mpaka sasa hivi bado hawajalipa fedha zao?

Mheshimiwa Spika, kwa kusema hayo, nakushukuru sana, naunga mkono hoja. (Makofi)